Jumatatu, 18 Agosti 2014

Serikali yaipongeza VETA kwa Mafanikio


Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dkt. Shukuru Kawambwa ameipongeza Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi nchini (VETA)  kutokana na mafanikio mbalimbali yaliyopatikana katika kipindi cha miaka mitatu kati ya mwaka 2011 na  2014. Mafanikio hayo ni pamoja na kuongezeka kwa wanafunzi waliojiunga na mafunzo ya ufundi stadi kutoka 102, 700 mwaka 2011 hadi 159, 345 mwaka 2014, kuongezeka kwa ushirikishwaji wanawake katika nafasi mbalimbali  katika elimu ya ufundi stadi kutoka asilimia 35 mwaka 2011 hadi asilimia 42 mwaka 2014 na kuongezeka kwa udahili kwa walimu wa mafunzo ya ufundi stadi ngazi ya cheti kutoka  276 mwaka 2011 hadi  939 mwaka  2014 na ngazi ya stashahada kutoka walimu 34 mwaka 2011 hadi  89 mwaka 2014.


Waziri Kawambwa alitoa pongezi hizo mwishoni mwa wiki iliyopita wakati wa hafla fupi iliyofanyika jijini Dar es Salaam ya kuwaaga Wajumbe wa Bodi ya Ufundi Stadi ya Taifa iliyomaliza muda wake ambapo aliyataja mafanikio mengine kuwa ni pamoja na kukamilika na kuanza kutekelezwa  kwa Mpango  Mkakati wa Miaka Mitano (2012/13 -2016/17) wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi na kuimarika kwa mifumo mbalimbali ya Uongozi na Usimamiaji wa Fedha. 



Aidha, Dkt. Kawambwa alisema VETA katika kipindi hicho imeweza kujenga vyuo vipya vya Mikoa vya Manyara, Lindi, na Pwani.  Pia, kukamilisha ujenzi wa Chuo cha Ufundi Stadi - Kipawa ICT na Chuo cha Ufundi Stadi cha Wilaya cha Makete na  Chuo cha Hoteli na Utalii cha Arusha (VHTTI).

VETA pia imekamilisha maandalizi ya msingi katika maeneo patakapojengwa  vyuo vipya vya Mkoa vya Simiyu, Geita, Njombe na Rukwa.

Mafanikio mengine yaliyopatikana ni pamoja na kukamilika na kuanza kutekelezwa kwa sera na miongozo mbalimbali ya kuwezesha kutolewa elimu na Mafunzo ya ya ufundi stadi yaliyo bora, kuanzishwa kwa viwango 53 vya stadi za kazi      na kuhuishwa kwa mitaala mbalimbali na kuanzishwa kwa mahusiano na makubaliano mbalimbali kitaifa na kimataifa katika kuendeleza na kuimarisha elimu na mafunzo ya ufundi stadi. 

Pamoja na kutoa pongezi kwa Menejimenti ya Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kwa mafanikio yote yaliyopatikana wakati ikiwa chini ya usimamizi wa Bodi iliyomaliza muda wake, Waziri Kawambwa aliwaasa kuongeza bidii zaidi ili kupata mafanikio makubwa zaidi ya yale waliyofikia. 
“Naiasa Menejimenti ya VETA  kuipa ushirikiano mkubwa Bodi mpya nitakayoiteua muda si mrefu ili kuelekeza nguvu zao kutatua changamoto zilizopo,” alisema Dkt. Kawambwa. 

“Aidha, bado ufumbuzi unatakiwa wa jinsi ya kuwapata wakufunzi wenye umahiri wanaotakiwa kutoa mafunzo katika vyuo vyetu kulingana na hali ya sasa ya mabadiliko ya mara kwa mara ya Sayansi na teknolojia.  Hali ya sasa ya kutegemea walimu wenye "trade test" au ngazi ya aina moja kufundisha ngazi ile ile inabidi iepukwe. Lazima mikakati maalumu iandaliwe ya kupata wakufunzi walio mahiri kutoka vyanzo mbalimbali,” alisema Waziri Kawambwa. 
Bodi ya Ufundi Stadi ya Taifa iliyomaliza muda wake ilikuwa inaongozwa na Profesa Idrisa Bilal Mshoro na iliingia madarakani tarehe 1 Agosti, 2011 ilipoanza kazi rasmi.
 

  

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni