Jumanne, 20 Februari 2018

Waziri Prof. Ndalichako aziagiza Taasisi za Elimu kufuata Taratibu, Kanuni na Sheria za nchi


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amezitaka Taasisi zinazotoa Elimu ya Juu hapa nchini kufuata taratibu, Sheria na kanuni za nchi katika kuendesha Taasisi hizo.

Waziri Ndalichako ametoa kauli hiyo hii leo jijini Dar es Salaam alipofanya ziara ya kushtukiza katika Chuo Kikuu cha Kampla kilichopo Gongo la Mboto  ambapo amebaini kuwepo kwa idadi kubwa ya watumishi ambao hawana vibali vya Makazi  na Ajira.
Waziri Ndalichako amesema Chuo hicho kumekuwa na udanganyifu wa taarifa za kiutumishi ambapo watu walioajiriwa kama madereva na wahudumu wamekuwa wakiingizwa katika orodha ya watumishi  ambao ni Walimu huku wakijua watumishi hao hawana sifa za kuwa Walimu.

Waziri Ndalichako amesema baadhi ya walimu katika chuo hicho kutoka nje ya nchi wanakuja kama wanafunzi lakini wakifika Chuoni hapo wanahalalishwa na kuwa walimu ambao wanafundisha wanachuo bila kuwa sifa stahiki.

Profesa Ndalichako pia amekitaka chuo hicho kuhakikisha kinafuatilia kwa karibu nidhamu ya wanafunzi wanaosoma Chuo hapo kwa kuhakikisha wanazingatia na kufuata taratibu, kanuni na sheria za nchi.

“Nidhamu ni jambo la msingi sana, sasa hakikisheni wanafunzi wanaomaliza katika chuo hiki wanakuwa na nidhamu ikiwa ni pamoja na kuzingatia kanuni na taratibu za ndani  na nje ya nchi na siyo vinginevyo, maana kuna baadhi ya wanafunzi ambao nyaraka zinaonyesha wamemaliza kwenye Chuo hiki na wako nje ya nchi lakini hawana maadili, liangalieni hili kwa umakini,”alisema Profesa Ndalichako.

Kwa upande wake  Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Dk. Anna Makakala  amezitaka Taasisi zote za Elimu nchini kuhakikisha zinatoa ushirikiano kwa ofisi hiyo ili kuepuka kukiuka taratibu na miongozo iliyowekwa na nchi.




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni