Jumanne, 21 Agosti 2018

MAPENDEKEZO YA MUSWADA WA SHERIA YA BODI YA KITAALAMU YA WALIMU YAWASILISHWA KWENYE KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE


Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imewasilisha mapendekezo ya Muswada wa Sheria ya Bodi ya Kitaalamu ya Walimu Tanzania kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii.

Akiwasilisha mapendekezo hayo Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mheshimiwa William Ole Nasha amesema Bodi hiyo itasimamia usajili, weledi na maadili ya kitaalamu ya walimu katika sekta ya umma na binafsi.

Naibu Waziri amesema kupitia bodi hiyo Pia itainua  hadhi ya taaluma ya ualimu kwa kusajili walimu wote kulingana na viwango vya ubora wa ualimu na kuwapa leseni ya kufundisha katika ngazi stahiki.

 Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. William Ole Nasha akiwasilisha Mapendekezo ya Muswada wa Sheria ya Bodi ya Kitaalamu ya Walimu kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Jijini Dodoma


Pia kupitia bodi hiyo ya kitaalamu itakuwa na jukumu la kuimarisha utaalamu wa walimu kwa kuchochea ari ya kujiendeleza kitaalamu miongoni mwa walimu na kuongeza fursa  za ajira katika soko la ndani na nje ya nchi.

Naibu Waziri Ole Nasha amesema utaalamu wa ualimu hapa nchini umekuwa ukisimamiwa na vyombo mbalimbali ambavyo vililenga kwenye ajira, maslahi ya walimu na maadili ya walimu kiutumishi huku masuala ya usimamizi na maendeleo ya utaalamu wa ualimu kutokuwa na sheria na chombo mahususi cha kuyasimamia. 

Amesema  kuundwa kwa Bodi mahsusi ya kusimamia Utaalamu wa Walimu ni suala la msingi katika kuinua ubora wa Elimu nchini na suala hili limezingatiwa kwenye Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 iliyotamka bayana kuwa Serikali itahuisha Mfumo na Muundo wa Uongozi, Usimamizi na Uendeshaji katika Sekta ya Elimu ili uwe na tija na uwajibikaji.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. William Ole Nasha akiwasilisha Mapendekezo ya Muswada wa Sheria ya Bodi ya Kitaalamu ya Walimu kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Jijini Dodoma

Pia Sera hiyo imetamka kuwa Serikali itahakikisha kuwa maadili na haiba ya ualimu na watumishi wengine yanazingatiwa katika ngazi zote za Elimu na mafunzo hivyo kuanzishwa kwake kuna tija katika usimamizi wa Utaalamu wa Ualimu.

Walengwa wa Bodi ya Kitaalam ya Walimu Tanzania inayopendekezwa itamhusu mtu yeyote aliyefuzu mafunzo ya ualimu katika Chuo cha Ualimu au Chuo Kikuu kinachotambuliwa na mamlaka husika katika ngazi ya Astashahada, Stashahada, Shahada, Shahada ya Uzamili na  Uzamivu.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. William Ole Nasha akiwa na Viongozi Wakuu wa Wizara, Wakurugenzi na watumishi wengine wa Wizara wakiwasili katika viwanja vya Bunge kwa ajili ya kuwasilisha Mapendekezo ya Muswada wa Sheria ya Bodi ya Kitaalamu ya Walimu kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni