Jumanne, 9 Oktoba 2018

MAMLAKA YA ELIMU TANZANIA YATAKIWA KUTUMIA UTARATIBU WA FORCE AKAUNTI


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. William Ole Nasha ameitaka Mamlaka ya Elimu Tanzania, (TEA) kuanza kutumia utaratibu wa Force Akaunti katika utekelezaji wa miradi ya Elimu wanayoisimamia kwa kuwa utaratibu huo unawezesha kazi kukamilika kwa wakati, lakini pia kujenga majengo yenye ubora kwa gharama nafuu.

Ole Nasha ametoa agizo hilo mkoani Manyara wakati akikagua shughuli za ujenzi katika shule ya Sekondari ya wasichana Nangwa na ile ya Endasak zilizopo Wilayani Hanang ambazo kwa pamoja ujenzi wake unatekelezwa na Wizara hiyo kupitia Programu ya Lipa Kulingana na Matokeo (EP4R) na Mamlaka ya Elimu Tanzania.

“Nitawapeni mfano Shule ya Sekondari Endasak imejengewa bweni na Wizara ya Elimu kupitia Mamlaka ya Elimu Tanzania lenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 80 kwa zaidi ya shilingi milioni 170, huku miradi mingine inayotekelezwa na Wizara kupitia Programu ya Lipa Kulingana na Matokeo (EP4R) ikitumia kiasi hicho hicho kujenga mabweni mawili yenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 80 kila moja kwa utaratibu wa Force Akaunti,” alisema Naibu Waziri Ole Nasha.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akipata maelezo ya maendeleo ya ujenzi wa bweni katika Shule ya Sekondari ya wasichana Nangwa kutoka kwa Mhandisi wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang Sembua Faraja. Shule hiyo iko katika Wilaya ya Hanang Mkoani Manyara. 

Kiongozi huyo amesema mahitaji ya Taifa letu kwenye Sekta ya Elimu bado ni makubwa hivyo ni vizuri kurudi katika utaratibu wa kutumia Force Akaunti ili kuweza kuwapatia malazi wanafunzi wengi pamoja na kutatua changamoto nyingine zilizopo kwenye Sekta ya Elimu. 

Naibu Waziri huyo pia amewaagiza viongozi wa elimu mkoa wa Manyara kuhakikisha Shule ya Sekondari ya Endasak katika mwaka wa masomo 2019/20 inapangiwa wanafunzi wa kidato cha tano kwa kuwa tayari ina miundombinu inayotosheleza likiwemo bweni lililojengwa na Wizara hiyo.
Muonekano wa nje wa bweni lililojengwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia Mamlaka ya Elimu Tanzania katika shule ya sekondari Endasak iliyoko katika Wilaya ya Hanang mkoani Manyara.

Akizungunza na wanafunzi  wa Shule ya Sekondari ya wasichana Nangwa na ile ya Endasak Mheshimiwa Ole Nasha amewataka wanafunzi hao kuwa na bidii katika masomo, waadilifu lakini pia kuwa wazalendo kwa nchi yao kwani kwa kufanya hivyo wataweza kuitetea nchi yao na kutoshiriki katika vitendo viovu.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akiongea na wanafunzi katika shule ya Sekondari ya Wasichana Nangwa iliyoko katika Wilaya ya Hanang Mkoani Manyara. Amewataka wanafunzi kusoma kwa bidii, kuwa waadilifu na wenye uzalendo katika nchi yao ili kuepuka kujiingiza katika vitendo viovu.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni