Jumatatu, 22 Oktoba 2018

WAZIRI NDALICHAKO AWATAKATA WAHASIBU WA WIZARA ANAYOINGOZA KUACHA “WIZI WA KISHAMBA”


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amesema kuwa kuna baadhi ya wahasibu wa Wizara hiyo na Taasisi zake ambao wamekuwa wakitumia vibaya nafasi zao kwa kughushi nyaraka mbalimbali wakati wa kufunga mahesabu kwa lengo la kujipatia fedha ambazo si halali yao.

Waziri Ndalichako ametoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam wakati akifungua mafunzo ya siku tano ya uandaaji wa hesabu za Fedha za Serikali kwa wahasibu wa Wizara hiyo na Taasisi zake.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na Wahasibu wa Wizara hiyo na taasisi zake wakati akifungua mafunzo ya uandaaji wa hesabu za fedha za serikali jijini Dar es Salaam, ambapo Waziri amesisitiza suala la uadilifu, uzalendo na kuwataka wahasibu kuacha kushughushi nyaraka kwa lengo la kujipatia fedha ambazo siyo halali yao.

Waziri Ndalichako amesema Wahasibu wa Wizara lazima wawe mfano katika kuonesha nidhamu kwa kuwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ndiyo Wizara mama kwani kada zote zinafundishwa na walimu ambao msingi wao ni Wizara hiyo hiyo anayoiongoza.

Waziri Ndalichako ameeleza kuwa kuna dalili kuwa kuna baadhi ya wahasibu katika Wizara hiyo wanachezea fedha za Umma, hivyo amewaeleza Wahasibu hao  kuwa hivi sasa kuna ukaguzi unaendelea kwenye Wizara hiyo na matokeo ya ripoti hiyo yatakapokamilika umma utajulishwa.

“Kuna misemo kuwa eti mbuzi anakula kwa urefu wa kamba yake, sasa kamba inakatika, tuwe makini na kanuni za kazi, Fedha za serikali katika awamu hii ya Tano ni sumu, nyaraka nyingi ambazo zimekuwa zikitumika kwenye kufunga hesabu ni za kughushi, majina yamekuwa yakijirudia katika semina ambazo zimekuwa zikifanyika, saini tofauti jambo linaloashiria kuwa kuna wahasibu wanachezea fedha za serikali na huo ni wizi wa kishamba, amesisitiza Waziri Ndalichako.
Mhasibu Mkuu wa Wizara ya Elimu CPA (T) Rose Waniha akizungumza na wahasibu wakati wa mafunzo ya uandaaji wa fedha za serikali mkoani dar es salaam
                                                                                                                  
Waziri huyo ameeleza kuwa zipo pia baadhi ya Taasisi za Wizara hiyo zinapokusanya fedha za ada hawaziingizi kwenye mfuko wa serikali.

Hivyo ameielekeza Wizara hiyo na Taasisi zake zote kuhakikisha kuwa hadi itapofika Novemba moja mwaka huu ziwe zimejiunga na mfumo wa serikali wa malipo ya kielektroniki (GePG- Government e - payment Gateway Systeam) ili kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato ya serikali.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na Mhasibu Mkuu wa Wizara hiyo CPA(T) Rose Waniha wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya uandaaji wa hesabu za Fedha za Serikali, mafunzo hayo ya siku Tano yameanza leo na yatakamilika oktoba 26, 2018 

Kwa upande wake Mhasibu Mkuu wa Wizara hiyo CPA (T) Rose Waniha amesema kuwa lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo wahasibu kuwa na uelewa wa pamoja wa namna bora ya uandaaji wa hesabu za fedha za serikali.

Mafunzo hayo ya siku Tano yaliyoanza leo yatahitimishwa oktoba 26, 2018.
Baadhi ya wahasibu wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya uandaaji wa hesabu za Fedha za serikali, mafunzo yanayofanyika jijini Dar es salam.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni