Jumanne, 4 Desemba 2018

OLE NASHA AWATAKA WALIMU KUBADILI MBINU ZA UFUNDISHAJI

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha amewataka walimu nchini kote kuachana na aina ya zamani ya ufundishaji na badala yake watumie mbinu za kisasa ili kusaidia kumuandaa mwanafunzi aweze kuendana na mabadiliko ya Sayansi na Teknolojia.

Mheshimiwa Ole Nasha ameyasema hayo mkoani Morogoro wakati wa ziara ya kikazi ya kukagua miradi ya Elimu na kuongea na Viongozi wa Elimu ngazi ya Mkoa ambapo amesisitiza kuwa Elimu ya sasa ni ile ambayo inaendeshwa na matumizi ya Tehama, uongozi mzuri na kubadili mtizamo wa Elimu kutoka katika utaratibu ule ambao mwanafunzi anakuwa mtu wa kupokea na kwenda kwenye mfumo ambapo mwanafunzi anategemewa kushiriki zoezi la ufundishaji.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akikagua samani katika Majengo ya Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima yaliyojengwa Wamo Mkoani Morogoro.

Naibu Waziri huyo pia amesema katika vyuo mfumo unaotumika ni ule wa kumuandaa mwanafunzi kwenda kuajiriwa badala ya kujiajiri mwenyewe hali ambayo inabidi kubadilika ili vijana waweze kumaliza wakiwa wenye maarifa ya kwenda kutatua changamoto zilizopo katika jamii.

“Katika vyuo vyetu, mfumo wa sasa unaotumika unawafundisha wanafunzi kama watu wa kwenda kufanya kazi baadae badala ya kufundisha watu wa kwenda kutengeneza ajira na ndio maana mwanafunzi akimaliza chuo anakuja ofisini anasubiri umpe kazi, hiyo siyo sawa lazima Elimu yetu iwe ni ya kujenga maarifa ya kujitegemea“ alisisitiza Mhe. Ole Nasha
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akizungumza na wanafunzi wanaosoma katika Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima iliyoko Wamo mjini Morogoro.  

Naibu Waziri Ole Nasha pia amewataka viongozi wa mkoa wa Morogoro kufuatilia kwa karibu miradi ya Elimu inayotekelezwa katika mkoa huo ili kuhakikisha inakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyokubalika.

Kwa upande wake Afisa Elimu Mkoa wa Morogoro Joyce Balavuga alimweleza Naibu Waziri wa Elimu kuwa mkoa wa Morogoro uko mstari wa mbele kuhamasisha matumizi ya Tehama katika ujifunzaji na ufundishaji katika shule zake ili kuinua kiwango cha ufaulu, kutunza kumbukumbu na takwimu mbalimbali za Elimu.

Naibu Waziri Ole Nasha yuko mkoani Morogoro kwa ziara ya kikazi ya kukagua miradi ya Elimu ambapo kwa leo ametembelea Chuo cha Ufundi na mafunzo ya Ufundi Stadi VETA Kihonda na Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima iliyoko Mkoani Morogoro

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknoloji William Ole Nasha akikagua mradi wa ujenzi wa karakana za ufundi umeme zilizojengwa katika Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi VETA Kihonda mjini Morogoro.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni