Alhamisi, 7 Machi 2019

WAZIRI NDALICHAKO ASEMA SAYANSI NA TEKNOLOJIA NI MUHIMU KATIKA UKUAJI WA UCHUMI


Serikali imewataka  wabunifu nchini kujikita katika  kuangalia shughuli za ambazo zinafanyika katika mazingira yao na wabuni jinsi ya kuzirahisisha kwa kutumia Sayansi na kiteknolojia ili kuchangia katika ukuaji wa uchumi nchini.
Mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Ilboru Maximillian Masesa akitoa maelezo kwa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako  juu ya kifaa cha kubaini wanafunzi ambao wanatumia simu shuleni alichobuni.

Kauli hiyo ya serikali imetolewa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako katika kilele cha Mashindano ya kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu mjini Dodoma. Waziri Ndalichako  pia aliongeza kuwa eneo la Sayansi na Teknolojia ni muhimu kwa taifa na likitumika vyema litasaidia  kuongeza uzalishaji na Kurahisisha utekelezaji wa mambo mbalimbali ya kijamii na kiuchumi.

“Kwa muda mrefu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imekuwa ikisimamia zaidi Elimu kuliko masuala ya Sayansi na ubunifu hivyo ni vyema wabunifu waendelee kujitokeza  zaidi na wajikitike katika  ikubuni mbinu za kurahisisha mifumo ya shughuli mbalimbali za kijamii  ikiwemo Kilimo, ufugaji na njia bora za upatikanaji wa maji”, alisema Waziri Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akiangalia ubunifu wa injini ya Ndege  uliofanywa na Emmanuel Chibula kutoka Musoma, Mkoani Mara wakati wa kilele cha mashindano ya kitaifa ya sayansi, teknolojia na Ubunifu yaliyofanyika Jijini Dodoma.

Kwa upande wake Kaimu Katibu Mkuu Profesa James Mdoe amesema  lengo  la Mashindano hayo yaliyohusisha wabunifu kutoka  ngazi mbali za Elimu ni kuibua ubunifu, umahiri, kuchochea ugunduzi kwa lengo la kukuza matumizi ya Sayansi na Teknolojia katika maendeleo.
Wanafunzi mbalimbali wa Shule za Msingi na baadhi ya Wananchi wakifuatilia Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu yaliyofanyika katika Viwanja vya Mwalimu Nyerere.

Mashindano hayo  yalifunguliwa rasmi na Naibu Waziri Mhe. William Ole Nasha Machi 5, 2019 na leo yamefikia kilele ambapo washindi mbalimbali walipata zawadi za fedha na kutunukiwa vyeti.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na washiriki mbalimbali hawapo pichani wakati wa kufunga mashindano ya kitaifa ya kitaifa ya sayansi, teknolojia na Ubunifu yaliyofanyika Jijini Dodoma.

Kauli mbiu ya mashindano hayo kwa mwaka huu ni " kukuza ujuzi na ubunifu kwa uchumi wa viwanda".
Wanafunzi wa Chuo cha Usafirishaji nchini NIT wabuni gari lisilotumia injini, na badala yake linatumia umeme kuendesha mifumo yake. Pichani Waziri akiwa kwenye gari hilo akipewa maelezo ya namna gari hilo linavyofanya kazi.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni