Jumamosi, 13 Aprili 2019

WAZIRI NDALICHAKO AMUAGIZA KAMISHNA WA ELIMU KUREJESHA MAFUNZO YA UFUNDI

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amemuagiza Kamishna wa Elimu kushirikiana na Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kuhakikisha ifikapo mwaka 2020 mafunzo ya ufundi yanaanza kutolewa kikamilifu katika shule saba za ufundi ambazo Serikali imezikarabati.

Pia amemuagiza kuhakikisha ifikapo 2020 michepuo inayoendana na mwelekeo wa Serikali kama kilimo inaanza kufundishwa lakini pia kuwepo na somo la Teknolojia ya Habari na Mawasiliano kwa tahasusi za wanafunzi wa kidato cha tano.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akiangalia panya ambao wana uwezo wa kubaini vimelea vya ugonjwa wa TB wakati alipotembelea mabanda ya maonesho katika viwanja vya Chuo Kikuu cha Sokoine Mkoani Morogoro wakati wa kufunga wiki ya kumbukizi ya Hayati Edward Moringe Sokoine
Waziri Ndalichako ametoa maagizo hayo mkoani Morogoro wakati wa kufunga Wiki ya Kumbukizi ya Hayati Edward Moringe Sokoine ambapo amesema tukitaka watoto wetu waweze kuingia katika soko la ushindani hatuwezi kuacha nyuma masomo hayo.

Profesa Ndalichako aliongeza kuwa Serikali imetumia takribani shilingi bilioni moja kukarabati shule hizo za ufundi na kwamba ni vyema zikaanza kutoa mafunzo kwa wanafunzi ili nchi iweze kuneemeka na matunda ya utaalamu wa wanafunzi hao pindi watakapomaliza.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akipata maelezo ya namna mashine za kuvunia mpunga zinavyofanya kazi kutoka kwa mtaalamu anayesimamia mashine kutoa Chuo Kikuu cha Sokoine.
Katika hatua nyingine Waziri Ndalichako ameeleza kufurahishwa na namna Chuo Kikuu cha Sokoine kinavyoendelea kumuenzi na kumpa heshima kubwa Hayati Edward Moringe Sokoine ambaye alikuwa shujaa, mchapakazi, mzalendo na mtu ambaye alijitoa katika kulitumikia Taifa na kwamba mpaka mauti yanamkuta alikuwa kazini.

“Tuna wajibu wa kuyaishi mazuri ambayo yamefanywa na kiongozi huyu, SUA nafurahi kuona mnawashirikisha wanafunzi katika midahalo hii ni vizuri wakajua Taifa limetoka wapi, nchi hii imetulia kwa kuwa kuna watu walifanya kazi usiku na mchana ya kujenga amani, umoja na mshikamano ni rahisi sana kufanya kitu kimoja cha kuvuruga amani na mshikamano lakini ikivurugika kuijenga inaweza kuchukua karne kuirudisha kwa hiyo tuendelee kuwaenzi waasisi wa Taifa hili kwa kuyaishi waliyoyafanya,”  alieleza Waziri Ndalichako.

Amesema Serikali ya Awamu ya Tano inatambua kuwa asilimia kubwa ya Watanzania ajira zao ni kilimo na katika kuenzi mazuri yaliyofanywa na Hayati Edward Moringe Sokoine Serikali imeendelea kukiimarisha Chuo kikuu cha Sokoine ikitambua kilimo bora kinatakiwa kuwa na utaalamu bora.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akiangalia shamba darasa la zao la zabibu lililopo katika Chuo Kikuu cha Sokoine mkoani Morogoro.
Kufuatia umuhimu huo Serikali imetumia zaidi ya bilioni 2 kujenga na kununua vifaa vya maabara ya sayansi katika Chuo Kikuu cha Sokoine yenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 400, pia katika mwaka wa fedha 2018/19 Serikali imetoa fedha zaidi ya shilingi billioni 7 kwa ajili ya ujenzi wa maabara mtambuka pamoja na bweni la wanafunzi lenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 700 pindi litakapokamilika.

Pia kupitia Tume ya Sayansi na Teknolojia Chuo kimepatiwa shilingi milioni 400 kwa ajili ya kuboresha maabara ya udongo itakayowasaidia wakulima kujua aina ya udongo na mazao yanayostahili kupandwa kwani wakati mwingine mazao yanaweza yasiwe na tija kwa sababu wakulima wanajipandia bila ya kuwa na utaalamu wa kujua afya ya udongo na kile kinachostawi na kupelekea kuathiri uzalishaji.

Wakizungumzia utendaji wa Hayati Edward Moringe Sokoine wakati wa uhai wake baadhi ya viongozi waliowahi kufanya nae kazi akiwemo Mhe. Getrude Mongela na Mzee Paul Kimiti walisema Kiongozi huyo alikuwa mchapakazi, muadilifu na mzalendo aliyetumia muda wake kuipigania nchi yake bila kuchoka.


 Muonekano wa shamba darasa la zao la zabibu lililopo katika Chuo Kikuu cha Sokoine mkoani Morogoro.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni