Jumapili, 19 Januari 2020

NDALICHAKO AKABIDHIWA MAGHOROFA YA NSSF KWA AJILI YA HOSTELI

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako Jumamosi Januari 18, 2020  amekabidhiwa rasmi maghorofa 32 ya NSSF yatakayotumika kwa ajili ya kutoa huduma ya Hosteli kwa Wanafunzi wa Elimu ya Juu nchini.

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Ajira, Vijana, Kazi na Watu wenye Ulemavu Mheshimiwa Jenista Mhagama amesema mpango huo wa NSSF umetokana na maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt John Pombe Magufuli ambapo Wizara yake ilisimamia utekelezaji wake huku akieleza kuwa awamu ya pili NSSF watakamilisha majengo ambayo yatawezesha wanafunzi wengine zaidi ya 4000 kuishi.

Nae Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa  Joyce Ndalichako amemshukuru na kuwapongeza  Rais kwa uamuzi huo na kuongeza kuwa hiyo ni moja tu ya hatua kubwa anazoendelea kuchukua katika kuboresha Sekta ya Elimu.
Profesa Ndalichako amesema hatua hiyo itapunguza changamoto ya uhaba wa Hosteli za wanafunzi wa Elimu ya juu hapa Dar es Salaam na ameishukuru na kupongeza Bodi na Uongozi wa NSSF kwa utekelezaji wa haraka wa agizo hilo na kukamilisha mahitaji muhimu ya miundo mbinu katika Majengo hayo kwa wakati.

Majengo hayo yako eneo la Mtoni Kijichi, Wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam na yatahudumia wanachuo  4,317 kutoka Chuo cha Kumbukumbu  ya Mwalimu Nyerere, Chuo cha Usimamizi wa fedha IFM, Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu (DUCE), Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA)Chuo cha Diplomasia  na Taasisi ya Teknolojia  Dar es Salaam.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni