Jumatatu, 14 Septemba 2020

KATIBU MKUU DKT AKWILAPO AAGIZA KUFANYIKA TATHMINI YA MAZINGIRA NA MIUNDO MBINU YA SHULE ZOTE

 Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt Leonard Akwilapo amewataka Wathibiti Ubora wa shule nchini kufanya tathmini ya mazingira na miundombinu ya shule katika kudhibiti majanga ya moto yaliyokithiri katika siku za hivi karibuni.

 Dkt Akwilapo amesema hayo kufuatia tukio la moto lililosababisha vifo vya wanafunzi 10 na kujeruhi wengine lililotokea katika shule ya Msingi Byamungu Islamic iliyoko Kyerwa Mkoani Kagera.

Akwilapo amewataka Wathibiti ubora wa shule kushirikiana na wataalamu kubaini vyanzo vya moto katika shule  na amesema sheria zipo na pindi shule itakapogundulika kukiuka taratibu wasisite kuzichukulia hatua.

 “Asubuhi ya leo tumepokea taarifa ya kuungua kwa shule ya msingi ya Byamungu  na watoto wamepoteza maisha, lakini matukio haya yamekuwa yanaongezeka hivyo kama Wizara tunawajibu kuhakikisha hili linapatiwa suluhisho kwa kutumia wataalamu,"aliongeza Dkt. AKwilapo

Aidha Dkt.Akwilapo amesema Wathibiti Ubora wa shule zaidi ya 400 wameajiriwa mmepewa ofisi na vitendea kazi, nataka kuona mabadiliko ya namna tunavyosimamia shule”alisisitiza Dkt. Akwilapo.

Katibu Mkuu Akwilapo ametumia fursa hiyo kutoa pole kwa wazazi, walezi na Shule ya Msingi Byamungu iliyopo mkoani Kagera kwa kuondokewa na wanafunzi na kuwatakia uponyaji wa haraka majeruhi 6 ambao wanaendelea na matibabu.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni