Jumatatu, 6 Mei 2019

WATANZANIA WATAKIWA KUTHAMINI ELIMU INAYOTOLEWA NCHINI

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ave Maria Semakafu amesema Elimu inayotolewa nchini ina ubora unaokubalika ambapo amewataka wale wanaoibeza na kuidhalilisha kuacha kufanya hivyo.

Dkt. Semakafu ametoa kauli hiyo Jijini Dodoma wakati wa hafla ya kutunuku vyeti kwa wanafunzi washindi wa kitaifa ambao wameshiriki uandishi wa shindano la Insha za Jumuiya ya Maendeleo nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) na zile za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).

“Yapo mengi yanasemwa kuhusu Elimu yetu, tuache kujidhalilisha maana wanafunzi wetu ambao wanawakilisha nchi nje ya Tanzania katika masuala ya kielimu wamekuwa wakifanya vizuri,” alisema Dkt. Semakafu.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. AveMari Sekafu akizungumza wakati wa hafla ya kutunuku vyeti kwa washindi wa Kitaifa wa shindano la uandishi wa Insha za Jumuiya ya Maendeleo nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) na zile za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC). Amewataka walimu kuwasaidia wanafunzi  kufuata taratibu wakati wa uandishi wa insha.

Kiongozi huyo amesema mashindano hayo ni sehemu ya mkakati mkubwa wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika katika kujenga uelewa kwa wanafunzi juu ya kazi na mipango ya Jumuiya hizo.

Aliongeza kuwa uandishi wa insha unawapa wanafunzi hamasa ya kutafiti na kupata taarifa zaidi, kuelewa na kuwawezesha kujadili masuala mbalimbali kwa kina.

Kwa upande wake Mratibu wa mashindano hayo ambaye ni Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Ithibati ya shule Sylivia Chingwile ametoa wito kwa walimu na wazazi kuwahimiza wanafunzi kushiriki mashindano hayo ya insha na mengine yanayojitokeza, kwani uzoefu unaonesha wanafunzi wanaoshiriki katika mashindano hayo wamekuwa wakifanya vizuri katika mitihani yao ya mwisho.

Mshindi wa kwanza kikanda wa shindano la uandishi wa  Insha za Jumuiya ya Afrika Mashariki Innocent Shirima ambae ni mlemavu wa macho kutoka shule ya Sekondari  Moshi iliyoko Mkoa wa Kilimanjaro akipokea zawadi  na cheti wakati wa hafla ya kutunuku washindi  wa shindano la insha, hafla hiyo hao imefanyika jijini Dodoma.

Naye Mwanafunzi mshindi wa insha za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kikanda kwa mwaka 2018 Innocent Shirima kutoka shule ya Sekondari ya Moshi, iliyopo mkoani Kilimanjaro ameshauri mashindano ya insha ya Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) ziwe zinatoa fursa kwa wanafunzi kuchagua aina ya lugha wanayoweza kuitumia wakati wa kuandika insha hizo.

“Ili tuendelee kufanya vizuri katika masuala mbalimbali ya kijamii, nashauri kama ilivyo kwenye mashindano ya Insha za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) wanatoa machaguzi ya lugha kama vile Kifaransa, Kiingereza au Kiswahili, hivyo hivyo ningeomba ifanyike kwa mashindano mengine kwa lengo la kutangaza lugha zetu hususan Kiswahili, ili siku moja tuje kuona Sudan Kusini wanaandika insha kwa lugha ya Kiswahili,” alisisitiza mwanafunzi Innocent Shirima.

Kwa maelezo zaidi kuhusu  taarifa za  mashindano hayo ya uandishi wa insha na namna ya kushiriki tembelea tovuti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia (www.moe.go.tz).

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ave Maria Sekafu akiwa katika picha ya pamoja na washindi wa Kitaifa wa shindano la uandishi wa Insha za Jumuiya ya Maendeleo nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) na zile za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).

Jumamosi, 4 Mei 2019

RAIS DKT. MAGUFULI AWEKA JIWE LA MSINGI UJENZI MAKTABA YA CHUO KIKUU CHA SAYANSI NA TEKNOLOJIA MBEYA NA KUZUNGUMZA WANAFUNZI WA VYUO VIKUU VILIVYOKO MBEYA


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa Maktaba ya Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST) itakayokuwa na uwezo wa kuchukua wanafunzi 2500 kwa wakati mmoja na inayogharimu shilingi bilioni 5.5.

Akizungumza na wafanyakazi na wanafunzi wa  Vyuo Vikuu vyote vilivyoko  jijini Mbeya baada ya kuweka jiwe la msingi Rais Dkt. Magufuli ameipongeza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na uongozi wa MUST kwa kuenzi mawazo ya Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kwa kukiendeleza  Chuo hicho ambacho kilianza mwaka  1986 kama Chuo cha Ufundi na hatimaye mwaka 2012 kuwa Chuo Kikuu pekee cha Sayansi na Teknolojia nchini.

Mhe . Dkt. Joh Pombe Pombe Joseph Magufuli ,Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiongozana na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof.Joyce Ndalichako kuelekea eneo la uwekaji jiwe la Msingi ujenzi wa Maktaba Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya  (MUST).

Rais Magufuli pia amekipongeza chuo kwa kutoa mchango mkubwa kwa jamii ikiwemo kushiriki katika kusimamia kama wataalamu elekezi katika mradi wa  ukarabati wa shule kongwe, Vyuo vya Ualimu na ujenzi wa Mji wa Serikali Dodoma.

Pamoja na pongezi Rais Magufuli ameutaka uongozi wa Chuo hicho na Wizara kuhahakikisha jengo la Maktaba linakamilika kwani limechelewa na amewahakikishia kutoa fedha zilizobaki kiasi cha shilingi bilioni 2.9 mwezi wa huu wa tano ili kukamilisha kazi hiyo kwa haraka. Katika hatua ingine ametoa shilingi Bilioni 5 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni huku akiagiza chuo kutumia wataalamu wake wa ndani kufanya kazi hiyo.
Mhe . Dkt. Joh Pombe Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwasalimu wanafunzi na wananchi waliofika katika viwanja vya Chuo Kikuu cha  Sayansi na Teknolojia Mbeya  (MUST) kumsikiliza wakati akiingia uwanjani hapo kushoto ni Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof.Joyce Ndalichako.

“Nawapongeza lakini jengo hili limechukua muda mrefu sana miaka saba, sasa hakikisheni linakamilika na Chuo Kikuu Mzumbe jengeni kwa spidi kubwa majengo yakamilike kwa uwakati na ubora.”  

Aidha, Dkt. Magufuli ametoa wito kwa Vyuo Vikuu nchini kuendelea kujiimarisha kutoa elimu bora hasa katika zama hizi ambapo nchi yetu inaeleka Uchumi wa kati kupitia viwanda ambapo sayansi na teknolojia ndio msingi wa maendeleo hayo na kuwataka  wanafunzi kusoma kwa bidii na kujiepusha masuala yasiyo na msingi ili kuepuka kufeli na kupata maradhi ikiwemo ugonjwa wa ukimwi.

Awali akizungumza Waziri wa Elimu Syansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amempongeza na kumshukuru Rais kwa kuipa Elimu kipaumbele na Kuwekeza kiasi kikubwa ikiwemo fedha za ujenzi wa Maktaba MUST, uwekezaji wa ,Shilingi Bilioni 3.8 kwa ajili ya ujenzi wa Jengo la Utawala na Madarasa Chuo Kikuu Mzumbe Kampasi ya Mbeya, Shilingi  Bilioni 6.3 ujenzi wa hosteli za wanafunzi 1,024 Mzumbe Kampasi kuu Morogoro na shilingi Bilioni 9 kwa ajili ya ujenzi wa maabara mtambuka itokayochukua wanafunzi 1600 kwa wakati mmoja katika Chuo Kikuu Sokoine cha kilimo.

Ndalichako amesema fedha nyingine zilizotolewa lwa ajili ya sekta ya Elimu ni Shilingi bilioni 12 za ujenzi wa kituo cha umahiri cha magonjwa ya moyo na mishipa ya damu kikubwa katika Afrika Mashariki kinachojengwa katika Chuo kikuu cha Afya na Sayansi  Shirikishi Muhimbili  Kampasi ya  Mlonganzila.   Waziri Ndalichako amemuhakikishia Mhe. Rais kuwa Wizara yake itasimamia kikamilifu miradi hiyo.

Wanafunzi wa Vyuo vikuu vilivyoko Mbeya wakifurahia hotuba ya Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli akizungumza nao katika viwanja vya Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST).

Wakitoa salamu, wakuu wa Vyuo Vikuu vya Mzumbe na MUST wameishukuru Serikali na kuahidi kuendelea kutoa mafunzo na kozi zinazoendana na wakati , huku changamoto kubwa ikiwa ni kuchelewa kupata idhibati ya kuendesha programu mbalimbali walizoomba kutoka Kamisheni ya Vyuo Vikuu (TCU).

Kufuatia hali hiyo Rais Magufuli  amemuagiza Waziri kuhakikisha ndani ya siku 10 Mwenyekiti wa Bodi ya Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania na wataalamu wake kutembelea Chuo cha Sayansi na Teknojia Mbeya  ili kutoa majibu ya ithibati za kozi zilizoombwa.

Katika hatua ingine Rais Mhe. Dkt. Magufuli  amemuagiza Mkuu wa Mkoa wa Mbeya kufuatilia ujenzi wa barabara kuelekea katika Chuo cha MUST ijengwe kwa haraka ili kulinda hadhi ya Chuo hicho.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akimpongeza Waziri wa Elimu Profesa Joyce Ndalichako mara baada ya kuweka jiwe la msingi ujenzi wa Maktaba ya chuo hicho cha MUST.

Ijumaa, 3 Mei 2019


UNITED REPUBLIC OF TANZANIA
MINISTRY OF EDUCATION, SCIENCE AND TECHNOLOGY

SCHOLARSHIP TENABLE IN EIGHT COUNTRIES IN EASTERN AND SOUTHERN AFRICA 2019-2020

Call for Application
The General Public is hereby informed that, The Inter-University Council for East Africa (IUCEA) in partnership with the World Bank invites female applicants to apply for the IUCEA-World Bank Masters Fellowships for 2019. Eligible candidates must obtain an admission from an Africa Center of Excellence (ACE) that isKenya, Ethiopia, Rwanda, Malawi, Zambia, Mozambique and Uganda to study full-time in any of the priority disciplines of the ACE II Project: (i) STEM (Science, Technology, Engineering and Mathematics) or Industry (ii) Agriculture (iii) Health (iv) Education and (v) Applied Statistics.

For further information about the scholarship, the fellowship award, eligibility criteria, pleasevisit the following links: https://iucea.org/index.php?option=com_content&view=article&layout=edit&id=543

Application Process and Procedures
Interested candidates are advised to fill in the application form found at ace2.iucea.org or www.iucea.org, attach all requested documents, and send by e-mail to exsec@iucea.org with a copy to ace2rfu@iucea.org.

Applications must be received not later than 5.00 PM East African Time on June 30, 2019.

Issued by:
Permanent Secretary,
Ministry of Education, Science and Technology,
University of Dodoma,
College of Business and Law,
Block 10,
P .O. Box 10,
40479 Dodoma.

Jumatano, 1 Mei 2019

WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA YAPONGEZWA KWA KUBORESHA CHUO CHA UALIMU MPUGUSO


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. John Pombe Joseph Magufuli amefurahishwa na mradi wa ujenzi na ukarabati wa Chuo cha Ualimu Mpuguso kilichopo katika Wilaya ya Rungwe Mkoani Mbeya na ameipongeza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa mradi huo.

Rais Magufuli amesema hayo wakati wa hafla ya uwekaji jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa majengo mapya na ukarabati katika Chuo hicho kwa lengo la kuboresha na kuongeza miundo mbinu ili kuongeza nafasi na kuweka mazingira bora ya ufundishaji na ujifunzaji.

“Niwapongeze Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kukiboresha Chuo hiki ambacho ni cha zamani kilianza mwaka 1926 ikiwa ni shule ya awali hadi mwaka 1975 kilipobadilishwa kuwa Chuo cha Ualimu na sasa kuna wanafunzi zaidi ya 900,” amesema Rais Magufuli.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akivuta utepe pamoja na viongozi wengine kuashiria uwekaji wa jiwe la msingi ujenzi wa Majengo mapya ya Chuo cha Ualimu Mpuguso Rungwe mkoani Mbeya. 

Katika hatua nyingine akizungumza na wananchi baada ya uwekaji jiwe la msingi amesema Serikali yake imeamua kuboresha Vyuo vya Ualimu ili viweze kuandaa walimu bora na kusisitiza kuwa ajira za waalimu watumishi wengine kwenye sekta ya elimu zinaendelea kutolewa ambapo zaidi ya watumishi 19,000 wenye sifa wameajiriwa mwaka huu,  huku akiwataka waalimu wanafunzi kuongeza juhudi katika masomo na kutembea kifua mbele kwani Serikali iko pamoja.

Rais Magufuli pia amewataka Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia, pamoja na Mkandarasi anaejenga Chuo hicho kuhakikisha kazi inakamilika kwa wakati na kwa ubora unaolingana na thamani ya fedha ya mradi. Aidha ameagiza Barabara inayoingia katika Chuo hicho kurekebishwa na baadae kutengewa fedha ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami.

Awali akitoa taarifa ya mradi wa Mpuguso, Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leornard Akwilapo amesema unagharimu shilingi Bilioni 9.6 na unahusisha ujenzi wa vyumba vya madarasa 16, maktaba, maabara 2 za sayansi, kumbi za mihadhara 2, bwalo la chakula, mabweni 2 ya wanafunzi 154 kila moja na nyumba za walimu zinazochukua familia 13.  Amesema mradi huo pia unahusisha ukarabati wa nyumba 4 za walimu, mabweni 2 , vyoo na mabafu7.

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akiwasalimia wananchi wa Mpuguso Rungwe mkoani Mbeya mara baada ya kuweka jiwe la msingi msingi ujenzi wa Majengo mapya ya Chuo cha Ualimu Mpuguso.


Mradi wa Ukarabati na ujenzi wa majengo mapya katika Vyuo vya Ualimu unagharamiwa na Serikali ya Tanzania na Canada, ambapo unahusisha vyuo vya ualimu 4 kikiwemo Mpuguso.  Vingine ni Kitangali Mtwara, Shinyanga na Ndala kilichopo Tabora. Kwa ujumla Mradi huu utagharimu shilingi Bilioni 36.4

Nae Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe (Mb) amepongeza wana Mpuguso kwa  kupata mradi huo mkubwa na kuwaasa kuhahakikisha wanatumia vizuri majengo hayo na kuyatunza.

Hafla hiyo ilihudhuriwa mamia ya wananchi wa Rungwe na viongozi akiwemo Mhe. Dkt. Tulia Akson Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano Tanzania, Mhe. Suleiman Jafo(Mb) Waziri wa TAMISEMI, Mhe. Japhet Hasunga(Mb) Waziri wa Kilimo, Mhe Joseph Kakunda(Mb) Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Mary Mwanjelwa(Mb) Naibu Waziri Utumishi na Mh Elias Kwandikwa(Mb) Naibu Waziri wa Ujenzi.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akiimba pamoja na wananchi waliokusanyika katika viwanja vya Chuo cha Ualimu Mpuguso mara baada ya kuwasili chuoni hapo.