Jumatatu, 23 Juni 2014

CHINA KUFADHILI WANAFUNZI WA ELIMU YA UFUNDI NCHINI

Mjumbe wa Baraza la Ushauri wa Kisiasa la China (Chinese Peoples Political Consultative Conference – CPPCC) Dkt. Annie Wu amesema kuwa atatoa ufadhili wa nafasi za masomo kwa wanafunzi wa Kitanzania kwenda kusoma elimu ya ufundi nchini China kwa lengo la kukuza na kudumisha  mahusiano mazuri yaliyopo kati ya Tanzania na China.
Dkt. Wu amekuja nchini kwa mwaliko rasmi wa Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo amefanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Sifuni Mchome ofisini kwake na kusema kuwa anatimiza ahadi yake aliyotoa awali ya kusaidia kuinua Elimu ya Ufundi nchini.
 Dkt. Wu alitoa ahadi ya ufadhili wa nafasi za masomo kwa wanafunzi wa Kitanzania kwenda kusoma elimu ya ufundi nchini China wakati Profesa Mchome alipofanya ziara ya kikazi mwezi huu nchini China na kukutana na kufanya mazungumzo na vingozi mbalimbali  wa nchi hiyo wa namna ya kuimarisha uhusiano uliopo kati ya Tanzania na China katika masuala ya elimu.
Kutokana na ufadhili huo uliotolewa na Dkt. Wu, Profesa Mchome amesema ufadhili huo umekuja wakati muafaka ambapo Serikali inaimarisha elimu ya Ufundi ili kuwaandaa vijana katika kujiajiri wenyewe pindi wanapomaliza masomo yao ya ufundi.

“Ni wakati sasa vijana wachangamkie fursa hii, wasome masomo ya Ufundi  ili wapate ufadhili na hatimaye wanapomaliza masomo yao waweze kujiajiri badala ya kusubiri kuajiriwa” Alisema Profesa Mchome. 

Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi Dkt. Primus Nkwera amepokea ufadhili huo kwa furaha na kuwataka wanafunzi kuchangamkia nafasi hizo zitakapotangazwa. 
“Dkt. Wu ni mmoja kati ya marafiki wa Tanzania ambao wanakuja mara kwa mara  nchini na kuhamasika na  kujali Elimu ya Ufundi, wengi wao hutoa vipaumbele katika elimu Msingi na Elimu ya Juu,” anasema Dkt. Nkwera, anaendelea kusema pia ”Mahusiano ya Tanzania na China yametimiza miaka 50 hivyo kuja kwake kunaonyesha urafiki wa kweli tulio nao kati ya Tanzania na China”.
Pamoja na kushika nafasi za juu katika Baraza la Ushauri wa Kisiasa la China Dkt. Annie Wu ni mfanyabiashara ambaye amesaidia kuanzishwa kwa Jumba la Sanaa (Culture House) lililoko Beijing ambalo pamoja na mambo mengine jumba hilo linatumika kuuza vinyago kutoka kwa Wafanyabiashara wa Tanzania.
Kuanzia Jumatatu wiki Hii Tanzania itapokea ugeni kutoka nchini China utakaoongozwa na Makamu wa Rais wa Nchi hiyo ambapo mambo mbalimbali yanayozihusu nchi hizi mbili yatajadiliwa


Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Profesa Sifuni Mchome (katikati)akikabidhi zawadi ya kinyago kwa Mjumbe wa Baraza la Ushauri wa Kisiasa la China (Chinese Peoples Political Consultative Conference – CPPCC) Dkt. Annie Wu

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni