Ijumaa, 14 Desemba 2018

OLE NASHA ASEMA KUSTAAFU SIYO ADHABU NI MAFANIKIO


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mheshimiwa William Ole Nasha ameitaka Wizara hiyo kuweka mkakati endelevu wa kutoa mafunzo kwa watumishi kuhusu masuala ya kustaafu na sio kusubiria kutoa mafunzo hayo wakati mtumishi anakaribia kustaafu.

Mhe. Ole Nasha ametoa agizo hilo jijini Dodoma wakati akifunga mafunzo kwa watumishi wa Wizara hiyo wanaotarajia kustaafu ambapo amesema kustaafu ni mchakato ambao unaanza pale mtumishi anapoajiriwa hadi anapofikia umri wa kustaafu.

“Idara ya Utawala na Rasilimali watu mnapaswa kutambua kustaafu ni mchakato unaoanza tangu mtumishi anapoajiriwa.  Kama unataka kumtayarisha mtumishi aweze kustaafu vizuri au kumpa maarifa ya kumwezesha kuishi vizuri baada ya kustaafu unapaswa kuanza mapema na sio kusubiri kutoa mafunzo wakati mtumishi amebakiza mwaka mmoja au miezi sita kustaafu,”  alisisitiza Naibu Waziri Ole Nasha.


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akimkabidhi cheti mmoja wa washiriki wa mafunzo ya kustaafu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Mafunzo hayo yameandaliwa na Wizara hiyo ili kuwapatia maarifa ya ubunifu na uendeshaji wa miradi ya uzalishaji mali baada ya kustaafu.

Ole Nasha ameitaka Idara ya Utawala ya Wizara hiyo kuhakikisha inaweka kumbukumbu za watumishi vizuri na kwa usahihi ili kuepuka ucheleweshaji wa mafao unaosababishwa na kutotunza kumbukumbu za watumishi hao ipasavyo.

Naibu Waziri huyo pia amewataka watumishi kuelewa kuwa kustaafu siyo adhabu ni mafanikio hivyo wanapaswa kujitambua na kutumia taaluma waliyo nayo na maarifa waliyoyapata katika mafunzo kuendeleza maisha yao baada ya kustaafu.


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akizungumza wakati wa kufunga mafunzo ya watumishi wanaotarajia kustaafu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Mafunzo hayo yamefanyika Jijini Dodoma.

Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Utawala na Rasilimali Watu, Gaudencia Mmasi amesema mafunzo hayo yamehusisha watumishi wanaotarajia kustaafu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na wale walio kwenye Vyuo Vya Ualimu, Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi na Ofisi za Uthibiti Ubora wa Shule.

Akizungumza kwa niaba ya Washiriki wa Mafunzo hayo. Katibu wa washiriki wa mafunzo ya kustaafu, Peter Kyabwazi aliiomba Wizara kuyafanya mafunzo hayo kuwa endelevu ili kuwasaidia wastaafu.

Mafunzo hayo kwa watumishi ambao wanatarajiwa kustaafu yamefanyika kwa siku tano kuanzia Desemba 10 na kuhitimishwa leo.
Washiriki wa mafunzo ya kustaafu wakifuatlia hotuba ya Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha wakati wa kufunga mafunzo kwa watumishi wa Wizara hiyo wanaotarajia kustaafu.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni