Jumatatu, 17 Desemba 2018

WAZIRI NDALICHAKO AZITAKA TAASISI ZA UFUNDI KUFUNDISHA KWA VITENDO.


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako ameziangiza taasisi zote zinazotoa Elimu ya Mafunzo ya Ufundi zilizo chini ya Wizara hiyo kuwafundisha wanafunzi kwa vitendo ili kuwawezesha wanafunzi hao wawe wabunifu na waweze kujiajiri.

Waziri Ndalichako ametoa agizo hilo wakati wa Mahafali 12 ya Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam ambapo amekagua miradi mbalimbali iliyobuniwa na wanafunzi wa taasisi hiyo pamoja na kuzindua jengo la mradi wa wanafunzi linalojengwa na wanafunzi kupitia mafunzo kwa vitendo.


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akimkabidhi mfano wa hundi mmoja wa wanafunzi wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam aliyeshinda katika kuandaa mradi wa ubunifu wakati wakati wa Mahafali ya 12 ya Taasisi hiyo.

Waziri Ndalichako amesema lengo la serikali kutoa Mafunzo ya Ufundi ni kwa ajili ya kuwaandaa wanafunzi kwa kuwapa ujuzi utakaowasaidia kutatua changamoto zilizopo katika Jamii na kuwawezesha kuchangia katika ukuaji kwa uchumi nchini pamoja na kushiriki katika kujenga uchumi wa viwanda.

"Nimepata fursa ya kutembelea miradi mbalimbali iliyobuniwa na kutengenezwa na wanafunzi wakati wa mafunzo kwa vitendo inatia moyo kwani bunifu zote zimelenga kutatua matatizo yaliyopo katika jamii." alisema Waziri Ndalichako
 Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na Wahitimu wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam wanalojenga kupitia mafunzo kwa vitendo wakati wa Mahafali ya 12 ya Taasisi hiyo iliyofanyika jijini Dar es Salaam.


Waziri Ndalichako pia amewataka wahitimu hao kuwa na nidhamu wanapokwenda kwenye soko la ajira na kuhakikisha bunifu zao zinawafikia wananchi na kutatua changamoto zilizopo badala ya kuishia katika maonesho.

Akizungumza katika Mahafali hayo Mkuu wa Taasisi hiyo Prof. Preksedis Ndomba amesema Taasisi ya DIT inajivunia bunifu mbalimbali ambazo taasisi hiyo  imezibuni, pia zimesaidia kuondoa  kuondoa changamoto katika Jamii ikiwemo mradi wa taa za barabarani ambazo zimewekwa katika baadhi ya mikoa ikiwemo Simiyu na Dar es Salaam.

Kabla ya kushiriki sherehe za Mahafali hayo Waziri Ndalichako alizindua jengo la mradi wa wanafunzi wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam wanalojenga kupitia mafunzo kwa vitendo.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizindua jengo la mradi wa wanafunzi wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam wanalojenga kupitia mafunzo kwa vitendo wakati wa Mahafali ya 12 ya Taasisi hiyo iliyofanyika jijini Dar es Salaam.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni