Jumatatu, 18 Machi 2019

KAMATI YA BUNGE YAHITIMISHA ZIARA YA KUKAGUA MIRADI ILIYO CHINI YA WIZARA YA ELIMU


Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Huduma na Maendeleo ya Jamii imekamilisha ziara ya kukagua utekelezaji wa Miradi mitatu mikubwa inayogharimiwa na Serikali kupitia bajeti ya Mwaka 2018/19 katika baadhi ya Vyuo vilivyo chini ya Wizara ya Elimu , Sayansi na Teknolojia na kuridhishwa na utekelezaji wa Miradi hiyo.

Kamati hiyo imetembelea Chuo Kikuu kishiriki cha Elimu (DUCE) katika mradi wa upanuzi na ukarabati wa jengo la Utawala ambalo linagharimu shilingi  Bilioni 3.2 ambapo kazi hiyo inaendelea na litakapo kamilika litaongeza nafasi kwa ajili ya ofisi za watumishi na vyumba vya mikutano.

 Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii (Hawapo Pichani) walipofanya ziara katika Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere kukagua mradi wa upanuzi na ukarabati wa Chuo hicho.

Aidha kamati imetembelea mradi wa upanuzi wa vyumba vya mihadhara
katika Chuo Kikuu Ardhi kazi ambayo imekamilika kwa hatua ya kwanza na
itagharimu shilingi  Bilioni 2.5 hadi kukamilika kwake.

Kamati imekamilisha ziara yake katika Chuo Cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, ambapo Wajumbe watembelea Jengo la jipya la Mihadhara linalojengwa kwa mapato ya ndani ya Chuo hicho, ambalo linauwezo wa kuchukua wanafunzi zaidi ya 300 kwa wakati mmoja.  Aidha kamati imepongeza wizara na uongozi wa Chuo kwa kazi nzuri na kubwa iliyofanyika katika kusimamia ujenzi huo. Jengo hilo limekamilika kwa asilimia 95.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Wiliam Ole Nasha akijadiliana jambo katika kikao na wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii (Hawapo Pichani) walipofanya ziara katika Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere kukagua mradi wa upanuzi na ukarabati wa Chuo hicho.


 Aidha  Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Mh. Prof. Joyce Ndalichako amepongeza uongozi wa Chuo kwa kusimamia vema matumizi ya fedha za zinazotokana na Mapato ya ndani na kutumika kwa kutekeleza miradi yenye tija  kwa Chuo. Ametumia nafasi hiyo kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh Dkt. John Pombe Magufuli kwa kusimamia suala la kubana matumizi na kuelekeza fedha katika kazi zenye faida kwa jamii kama ilivyo kwa Chuo Cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere.

 Mwenyekiti wa  Bodi ya Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Stephen Wasira akitoa maelezo kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii (Hawapo Pichani) walipofanya ziara katika Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere kukagua mradi wa upanuzi na ukarabati wa Chuo hicho


Katika majumuisho ya ziara hiyo, Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumuya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii  Mh. Oscar Mukasa(Mb) ameipongeza wizara na taasisi zilizotembelewa kwa kusimamia utekelezaji wa miradi na kushauri taasisi hizo kujikita katika kusimamia Dira na dhima za uanzishwaji wake. Kamati pia imeshauri Serikali kupitia Wizara kuhahakisha inatoa fedha za miradi kwa wakati kulingana na bajeti. 


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akiongoza wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii wakati wa kukagua maendeleo ya ujenzi wa ukumbi wa kisasa wa Mihadhara unaojengwa kwa mapato ya ndani ya Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere.


Mkuu wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Prof. Shadrack Mwakalila (Mwenye Tai Nyekundu) akitoa maelezo kuhusu mradi wa ujenzi wa ukumbi mpya wa mihadhara wa Chuo chicho uliyojengwa kwa fedha zinazotokana na mapato ya ndani kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jami.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni