Ijumaa, 24 Mei 2019

BALOZI FINLAND AIPONGEZA WIZARA YA ELIMU KWA UTEKELEZAJI WA MIRADI


Balozi wa Finland Pekka Makka ameipongeza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa utekelezaji wa miradi ya Sekta ya Elimu inayofadhiliwa na Finland ambayo imewezesha uboreshaji katika maeneo mbalimbali  ya sekta hiyo.

Balozi Makka ametoa pongezi hizo jijini Dodoma alipofika ofisi za Wizara na kukutana na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha kwa lengo la kushukuru kwa ushirikiano pamoja na kuaga baada ya kumaliza muda wake ambapo amesema kupitia utekelezaji wa miradi hiyo wameiona sekta ya elimu ikiboreshwa.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Wiliam Ole Nasha akisalimiana na Balozi wa Finland Pekka Makka  alipofika ofisi za Wizara kwa lengo la kushukuru kwa ushirikiano pamoja na kuaga baada ya kumaliza muda wake.
Makka amesema Wizara ya elimu imeboresha miundombinu katika shule mbalimbali nchini na kuweka mazingira mazuri ya wanafunzi kujifunza, huku akipongeza walimu kwa kuboresha mbinu za ufundishaji.  

Balozi huyo amesema Finland itaendelea kushirikiana na Tanzania katika uboreshaji wa sekta ya elimu hususan katika maeneo ya Elimu ya Ufundi, Sayansi, Teknolojia na Ubunifu ili kupanua wigo wa upatikanaji wa mafunzo nchini.

“Tumeona maboresho makubwa katika sekta ya elimu, nasi kama wafadhili tumefarijika na hakika tunaendelea kushirikiana na Tanzania katika kuendelea kuboresha sekta hii muhimu, na ninaahidi kuwa Balozi anayekuja kunipokea ataendeleza ushirikiano huu,” amesema Makka.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Wiliam Ole Nasha akizungumza na Balozi wa Finland Pekka Makka  alipofika ofisi za Wizara kwa lengo la kushukuru kwa ushirikiano pamoja na kuaga baada ya kumaliza muda wake ambapo ameipongeza wizara kwa kutekeleza vyema miradi mbalimbali.

Naye Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha ameishukuru Finland kwa ufadhili  wa Euro milioni 52 kwa ajili ya miradi, ambapo amesema kupitia ufadhili huo Tanzania imeshirikiana na Finland kuongeza fursa za elimu na mafunzo kwa  elimu ya watu wazima na elimu nje ya mfumo rasmi kupitia Taasisi ya Elimu ya Watu  Wazima, hususan kwa kuwajengea uwezo watekelezaji wa mpango wa ‘Intergrated Post Primary Education (IPPE)’ na mpango wa ‘Intergrated Programme for Out of School Adolescents (IPOSA)’.  

Miradi mingine aliyoitaja ambayo imefadhiliwa na Finland ni pamoja  elimu ya afya na michezo katika vyuo vya ualimu ambayo ililenga kuwajengea maarifa na ujuzi wakufunzi  na walimu tarajali waweze kufundisha shuleni kwa kuzingatia umuhimu wa michezo shuleni na kwa maendeleo ya taifa, mradi wa Tehama, (TANZAICT) unaotekelezwa na Tume ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), mradi ambao umewezesha kuwepo na mifumo ya kukuza ubunifu na kuwezesha mfuko wa kufadhili wabunifu wadogo.

Aidha, Naibu Waziri amesema ushirikiano kati ya Wizara na Finland utakaoendelea unalenga zaidi katika Mafunzo ya Ufundi na Ubunifu na kwamba umekuja kwa wakati sahihi ambapo nchi inaelekea katika uchumi wa kati kupitia viwanda.

“Ili kufikia uchumi wa kati  kupitia viwanda ni lazima tuwe na rasilimaliwatu ya kutosha iliyoelimika na yenye maarifa na ujuzi kwa ajili ya viwanda na pia itakayoweza kujiajiri,” amesisitiza Ole Nasha.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Wiliam Ole Nasha, Balozi wa Finland Pekka Makka  wakiwa katika picha ya pamoja na maafisa wa wizara mara baada ya kikao na Balozi huyo.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni