Jumapili, 2 Juni 2019

CHUO KIKUU MZUMBE CHATIKIWA KUWEKA UTARATIBU MZURI ILI KUWEZESHA WANAFUNZI KUPATA MIKOPO KWA WAKATI


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako ameanza ziara za kukutana na wanafunzi wa Elimu ya Juu ili kupokea na kusikiliza maoni, mapendekezo na changamoto za wanafunzi hao kwa ajili ya kuzitafutia ufumbuzi.
Waziri Ndalichako ameanza ziara hiyo katika Chuo Kikuu Mzumbe akiwa ameambatana na viongozi kutoka Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu ambapo ameuagiza uongozi wa Chuo Kikuu Mzumbe kuandaa utaratibu utakaohakikisha wanafunzi wanaojitokeza kusaini nyaraka za mikopo mapema kuwezeshwa kupata fedha zao kwa wakati.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungmza na Wanafunzi wa Chuo Kikuu Mzumbe wakati wa ziara yake ya kutembelea vyuo Vikuu na kuzungumza na wanafunzi
“Hili jukumu la kuhakikisha wanafunzi wanasaini kwa wakati nakupa Rais wa wanafunzi, uwahamasishe wenzako kusaini mapema ili wapatiwe fedha kwa kuwa serikali haina tatizo la fedha na ndio sababu zinapelekwa kwa wakati katika Vyuo,” alisisitiza Waziri Prof. Ndalichako.
Awali, baadhi ya wanafunzi walimweleza Waziri kuwa wanachelewa kupokea fedha za mikopo zinazopelekwa chuoni hapo na serikali kupitia Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) kutokana na kutokuwepo kwa utaratibu mzuri wa kupata taarifa.
Ili kutatua changamoto zilizopo katika kupatikana kwa mikopo kwa wakati wanafunzi hao walipendekeza kuwepo kwa mikutano ya mara kwa mara kati ya Serikali ya Wanafunzi wa Vyuo vya Elimu ya Juu, Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) pamoja na Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) ili kujadili kwa pamoja changamoto zilizopo na kuzitafutia uvumbuzi kwa pamoja.
Baadhi ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu Mzumbe wakimsikiliza Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako (Hayupo Pichani) wakati wa ziara yake ya kutembelea vyuo Vikuu na kuzungumza na wanafunzi
Akitoa ufafanuzi, Makamu Mkuu wa chuo Prof. Lugano Kusiluka amesema Menejimenti ya chuo hicho imekua ikikutana na changamoto ya baadhi ya wanafunzi kutojitokeza kusaini nyaraka zinazohitajika kuthibitisha uwepo wao chuoni licha ya kukumbushwa mara kwa mara.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB Abdul-Razaq Badru na Katibu Mtendaji wa Tume ya Vyuo Vikuu (TCU) Prof. Charles Kihampa wameahidi kutoa ushirikiano kwa menejimenti za vyuo ili kuhakikisha wanafunzi wanapata mikopo kwa wakati.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni