Jumamosi, 6 Julai 2019

NAIBU WAZIRI OLE NASHA ATAKA CHUO CHA UALIMU BUTIMBA KUREJESHA MASOMO YA SANAA


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha amekitaka Chuo cha Ualimu Butimba kilichopo Wilaya ya Nyamagana Mkoani Mwanza kufanya tafakari ya namna gani kinakuwa chachu ya mabadiliko katika kuandaa walimu wanaoendana na mahitaji ya sasa.

Naibu Waziri Ole Nasha ameyasema hayo Jijini Mwanza wakati wa maadhimisho ya kumbukizi ya miaka 80 ya kuanzishwa Chuo hicho ambapo amesema mijadala itakayoendeshwa ijikite zaidi katika kujua ni namna gani wanabadili mfumo wa kufundisha ili wanafunzi waweze kuwa wabunifu na wanaojiamini.

“Nimeona katika maonesho yenu mna jaribu kufanya masuala ya ubunifu, ubunifu unaanza mwanafunzi akiwa mdogo na ndio maana tunasema lazima kufanya ufundishaji ambao toka mwanzo unampa mwanafunzi nafasi ya kuwa mbunifu. Usimbane mwanafunzi jaribu kumfungulia fursa mbalimbali kwani anapozaliwa anakulia katika mazingira mbalimbali ya ubunifu hapo utatoa nafasi ya kuweza kuendeleza ubunifu alio nao,” alisema Naibu Waziri Ole Nasha.
Naibu waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William ole Nasha akizungumza katika Kumbukizi ya Miaka 80 ya Chuo cha Ualimu Butimba iliyofanyika katika  chuoni hicho  Jijini Mwanza.

 Alisema Chuo cha Butimba pamoja na kwamba ni chuo cha ualimu historia yake hasa iko katika ualimu ule wa Sanaa za maonesho, Sanaa za ufundi ni vizuri kuangalia ni namna gani Chuo hicho kinarudi katika msatri na kuendelea kutoa walimu ambao watasaidia katika kufundisha masomo hayo.

“Kwa bahati mbaya kuna mahali tulikosea kufikiri kwamba music, ufundi, Sanaa za maonesho hazina nafasi katika elimu, sio vibaya tukarekebisha sababu kama unataka kumfundisha mwanafunzi ubunifu huwezi kukwepa kutumia Sanaa za maonesho, music na tamaduni zake zote kwani zinamsaidia kuwa mwanafunzi kamilifu anaeweza kubuni,” aliongeza Naibua Waziri Ole Nasha.
Washiriki wakifuatilia hotuba ya Naibu waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha wakati wa kuadhimisha kumbukizi ya miaka 80 ya Chuo cha Ualimu Butimba kilichopo Wilaya ya Nayamagana  Jijini Mwanza

Akizungumzia Jitihada zinazofanywa na serikali katika kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia Ole Nasha amesema Serikali ya Awamu ya Tano imeweka historia ya kufanya uwekezaji mkubwa kwenye sekta ya elimu kwa kujenga, kukarabati na kununua vifaa vya kufundishia na kujifunzia kwenye shule.

Aliongeza kuwa pamoja na mambo mengine Serikali kuanzia mwaka 2016 inatekeleza Mpango wa Elimu bila malipo, mpango ambao haujawahi kuwepo ni mara ya kwanza katika historia ya nchi yetu ambapo inatumia zaidi ya shilingi bil. 20 kila mwezi kugharamia elimu bila malipo.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akipata maelezo  kutoka kwa wakufunzi wa Chuo cha Ualimu Butimba ya  namna wanavyotumia vifaa vinavyopatikana katika mazingira wanayoishi kufundishia.

Nae Mkuu wa Chuo cha Ualimu Butimba Huruma Mageni amesema katika kuadhimisha miaka 80 ya Chuo hicho kinajivunia mambo mengi ikiwemo eneo la chuo kupimwa na kwamba rasimu ya hati ya chuo iko tayari. Pia inajivunia kuwa na vitengo ambavyo vinachangia kuboresha elimu nchini.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni