Jumamosi, 6 Julai 2019

SERIKALI YAENDELEA KUBORESHA MAZINGIRA YA KUFUNDISHIA NA KUJIFUNZIA KWA WANAFUNZI WENYE MAHITAJI MAALUM.


Serikali imesema inatambua changamoto zinazowakabili wanafunzi wenye mahitaji maalum na ndio maana inachukua juhudi za makusudi kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia ili yawe rafiki kwao kupata elimu.

Kauli hiyo ya Serikali imetolewa jijini Mwanza na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha wakati akizungumza na wanafunzi wenye ulemavu wa ngozi walio katika Kambi ya Joto (Summer Camp) inayoratibiwa na Taasisi ya Under the Same Sun.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akizungumza na wanafunzi wenye ulemavu wa ngozi walio kwenye ‘summer camp’ katika Chuo cha Ualimu Butimba Jijini Mwanza. Ametumia fursa hiyo kuelezea juhudi ambazo Serikali imekuwa ikizifanya katika kutatua changamoto za watoto wenye ulemavu ili waweze kupata elimu.

Naibu Waziri Ole Nasha alisema katika kuendelea kutatua changamoto zinazowakabili wanafunzi wenye mahitaji maalumu kwa sasa Wizara anayoiongoza inatekeleza Programu ya Elimu Jumuishi ambayo inamuweka shuleni mtoto mwenye ulemavu na yule asie na ulemavu kwa lengo la kuondoa fikra za kunyanyapaliwa lakini pia kujenga umoja upendo na urafiki baina yao utakaowawezesha kulindana kwani siku zote mlinzi mzuri ni rafiki na ndugu hivyo inasaidia kuondoa changamoto zilizopo.

Aidha, Serikali pia inatoa mikopo kwa asilimia mia moja kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum wanaosoma elimu ya juu kwa lengo la kuwasadia waweze kupata elimu zaidi kwani watu wenye ulemavu wakipata elimu wanaweza sio tu kujikomboa wenyewe lakini kuwasaidia watu wengine wenye changamoto hizo.

“Ninyi wenyewe mtakuwa mashahidi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli katika Serikali yake kuna viongozi ambao wana ulemavu lakini kutokana na umahiri na uwezo walio nao katika utendaji wameteuliwa katika nafasi hizo. Tambueni kuwa watu wote wana haki sawa na hilo liko wazi,” alisema Naibu Waziri ole Nasha.

Kiongozi huyo amewataka wanafunzi hao kutambua kuwa wao ni watoto wa kitanzania hivyo wanatakiwa kuwa huru kwenye nchi yao na kwamba Serikali itaendelea kuwalinda  ili waweze kuishi lakini pia kusoma kama watu wengine bila kudhuriwa na kitu chochote.

”wote ni mashahidi kwamba kwa  sasa Serikali imefanya jitihada mbalimbali za kuhakikisha kwamba mnakuwa na usalama wa maisha yenu, sidhani kama kuna kosa ambalo sasa ukipatikana nalo unachukuliwa hatua kubwa zaidi kama kujaribu kuwadhuru watu wenye ualbino, na ndio maana sasa mnapata ulinzi kaeni mkiwa huru kwa kuwa serikali inawajali,”aliongeza Naibu  Waziri Ole Nasha.

Katika hatua nyingine Naibu Waziri Ole Nasha amelitaka Shirika la Under The Same Sun   kutambua kuwa Serikali inathamini mchango mkubwa wanaoutoa katika kuwasaidia  wanafunzi na watoto  wenye mahitaji maalum hasa watoto ambao wana changamoto ya ulemavu wa ngozi na kuwataka kuhakikisha mafunzo wanayoyatoa katika kambi za joto (summer camp) kila wanapokutana  pamoja na mambo mengine yalenge katika kuwaonesha watoto hao kuwa jamii inawajali na sio vinginevyo.
Wanafunzi wenye ulemavu wa ngozi wakimsikiliza Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William ole Nasha wakati alipokutana nao kuzungumzia juhudi ambazo Serikali imekuwa ikizifanya kutatua changamoto za watoto wenye ulemavu katika kupata elimu.

Nae Afisa kutoka Idara ya Elimu ya Shirika la Under the Same Sun Omary Mfaume amesema Shirika hilo linafadhili wanafunzi wenye ulemavu wa ngozi kupitia programu za elimu zinazojihusisha na ufadhili wa elimu na ile ya uhamasishaji jamii ambayo inayowafundisha kwanini mtu anazaliwa na ualbino, changamoto zake na namna ya kuzikabili changamoto hizo.

Akizungumza kwa niaba ya wanafunzi wenzake Clara Maliwa ameiomba Wizara kuwa na utaratibu wa kuwatambua Wanafunzi wenye ulemavu wa ngozi wanaofanya vizuri katika masomo ili kutoa changamoto kwa wengine ili waweze kufanya vizuri zaidi.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni