Jumapili, 27 Oktoba 2019

WIZARA YA ELIMU YAPONGEZWA KWA KUREJESHA MASHINDANO YA UMISAVUTA


Serikali imeipongeza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kutekeleza agizo la kurudisha mashindano ya Michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu (UMISAVUTA) huku ikiitaka kuhakikisha kuwa michezo na Sanaa vinapewa kipaumbele katika mipango endelevu ya Wizara.

Pongezi hizo zimetolewa Mkoani Mtwara. na Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe kwa niaba ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Mjaliwa wakati wa ufunguzi wa mashindano ya UMISAVUTA.
Mgeni rasmi Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe akipiga mpira kuashiria uzinduzi rasmi wa mashindano ya michezo na sanaa kwa vyuo vya ualimu nchini katika viwanja vya Nangwada Sijaona mkoani Mtwara.

Dkt. Mwakyembe amesema eneo la michezo na Sanaa ni sehemu muhimu katika makuuzi ya watoto kwani yanajenga na kuimarisha afya ya mwanadamu lakini pia yanaimarisha mahusiano baina ya raia.

“Kwa sasa nchi imeonesha mafanikio makubwa katika michezo hivyo ili Taifa lipate wataalamu na vipaji sahihi katika michezo na Sanaa hatuna budi kuanza ngazi za awali za elimu, “alisema Dkt. Mwakyembe.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. leonard Akwilapo amesema Wizara imejipanga vyema katika kuendeleza michezo ili kuongeza furaha kwa wananchi wa Tanzania kwa kuziona timu zinashiriki na kushinda mashindano makubwa ya kimataifa.

“Kama Wizara tunasema muda wa kushiriki sasa umetosha tunataka kuwa washindani na mashindano haya ni sehemu ya maandalizi ya kutekeleza azma hiyo,” alisema Katibu mkuu Akwilapo.
Mgeni rasmi Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe akisalimiana  na washiriki wa mashindano ya michezo na sanaa kwa vyuo vya ualimu nchini wakati wa ufunguzi wa mashindano hayo mkoani Mtwara.

Katibu Mkuu Akwilapo alisema kupitia mashindano haya washiriki wataongeza ujuzi  katika michezo na kuwa walimu ambao wataimarisha michezo wakati watakapokuwa kazini huku wengine wakiendeleza vipaji vyao na kuwa hazina ya Taifa kwa siku za usoni.

Michezo inayoshindaniwa ni pamoja na mpira wa Pete, mpira wa miguu, wavu kikapu, riadha, mashindano ya uchoraji, Sanaa za maonesho, ngoma pamoja na kwaya. Mingine ni pamoja na ile ya kutengeneza zana za kufundishia na kujifunzia kwa lengo la kumjengea mwalimu umahiri wa kuandaa na kutumia zana nzuri za kufundishia.
Baadhi ya Walimu Tarajali wakiingia  katika uwanja wa Nangwanda mkoani Mtwara wakati wa ufunguzi wa mashindano ya michezo na sanaa kwa vyuo vya ualimu nchini mapema hii leo mkoani Mtwara.

Nae Kaimu Mkurugenzi Msaidizi kutoka Seksheni ya Mafunzo ya Ualimu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Agusta Lupokela amesema mashindano hayo yaliyoanza Oktoba 25, 2019 yanatarajiwa kuhitimishwa Oktoba 31, 2019 na yameshirikisha Kanda saba ambazo ni Kanda ya Kati, Kusini, Mashariki, Magharibi, Kanda ya Ziwa, Kaskazini na Kusini ambazo zimeundwa kulingana na vyuo vya ualimu.

Juni 10, 2019 katika Viwanja vya Nagwanda Sijaona mkoani Mtwara wakati Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anafungua mashindano ya UMISSETA na UMITASHUMTA alitoa agizo kwa Wizara ya Elimu kuhakikisha kuwa mashindano ya michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu yanarejeshwa.
Baadhi ya Walimu Tarajali wakiandamana kuelekea katika uwanja wa Nangwanda mkoani Mtwara wakati wa ufunguzi wa mashindano ya michezo na sanaa kwa vyuo vya ualimu nchini mapema hii leo mkoani Mtwara.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni