Jumamosi, 26 Septemba 2020

UZINDUZI WA MKAKATI WA KITAIFA WA KUKUZA NA KUENDELEZA KISOMO NA ELIMU KWA UMMA

 Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW) imezindua Mkakati wa miaka mitano wa Kitaifa wa Kukuza na Kuendeleza Kisomo na Elimu kwa Umma.

Uzinduzi wa Mkakati huo ambao unaanza kutumika mwaka 2020 hadi 2025 umefanywa na Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa James Mdoe Jijini Dar es Salaam katika Ofisi za Tasisi ya Elimu ya Watu Wazima.(TEWW)

Akiongea katika uzinduzi huo, Prof. Mdoe amesema kuwa anaamini Mkakati huo utapunguza au kumaliza kwa kiasi kikubwa idadi ya Watanzania wasiojua Kusoma, Kuandika na Kuhesabu.

“Naamini Mkakati huu uliozinduliwa leo utakwenda kumaliza au kupunguza kwa kiasi kikubwa idadi ya watu wasiojua kusoma, kuandika na kuhesabu," amesema Prof. Mdoe.

Naibu Katibu Mkuu Mdoe pia ameitaka TEWW kuhakikisha kuwa wanaendesha programu ambazo zinaendana na mahitaji ya jamii na mabadiliko ya teknolojia.

"Niwaombe Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima mjiongeze, muwe wabunifu, muendeshe programu zinazoendana na mahitaji ya jamii na mabadiliko ya teknolojia ambayo kwa sasa inakua kwa kasi," amesisitiza Prof. Mdoe.

Naye Mkurugenzi wa TEWW, Dkt. Michael Ng'umbi akiongea katika uzinduzi huo amesema Taasisi yake imeboresha mtaala ambapo sasa wanafunzi watakaosoma chuoni hapo watafanya mafunzo kwa vitendo kwa kipindi cha Semista nzima na watatakiwa kuanzisha vituo vya kufundisha vijana na watu wazima.

"Tumeboresha mtaala ambapo kwa sasa wataalamu wanaopata elimu hapa chuoni, kila mmoja atatakiwa kuanzisha kituo cha kufundisha elimu ya watu wazima. Hata kama kila mmoja atamfundisha mtu mmoja, tukiwa wanafunzi 6,000 tuna uhakika idadi kama hiyo ya watu wazima watapata mafunzo na kuondokana na kutokujua kuandika, kusoma na kuhesabu," amesema Dkt. Ng'umbi.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni