Jumanne, 1 Septemba 2020

WALIMU 100 NCHINI KUFUNDISHWA MBINU ZA KUFUNDISHIA LUGHA YA KIFARANSA

Serikali za Tanzania na Ufaransa zimeingia makubaliano ya kutoa mafunzo ya mbinu za kufundishia lugha ya Kifaransa kwa walimu 100 nchini ambao watakuwa na uwezo wa kufundisha wanafunzi 5,000 wa Kitanzania katika ngazi ya sekondari.

Makubaliano hayo yamefikiwa katika kikao kati ya Balozi wa Ufaransa nchini, Mhe. Frederic Clavier na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi Teknolojia, Dkt. Leonard Akwilapo kilichofanyika Jijini Dar es Salaam ambapo jumla ya Dola za Kimarekani 250,000 zitatumika ili kufanikisha mpango huo.
Katika kikao hicho wamekubaliana kufanyika kwa vikao vya kitaalamu kati ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Kituo cha Ubalozi wa Ufaransa (Alliance Francais) ili kupanga utekelezaji wa mafunzo hayo ya walimu.

Aidha, Balozi Clavier ameonesha kuwepo kwa fursa za Watanzania kusoma programu zisizopungua 2,000 za Kiingereza nchini Ufaransa. Ameeleza kuwa  Ufaransa inaandaa Maonesho ya Elimu ya Juu (Higher Education Fair) yatakayofanyika nchini Mei 2021 ambapo vyuo 20 vya Ufaransa vitashiriki kutafuta ushirikiano na Vyuo Vikuu vya Tanzania na Sekta binafsi. 
Akizungumza katika kikao hicho, Katibu Mkuu Akwilapo ameushukuru Ubalozi wa Ufaransa kwa kuendeleza ushirikiano katika kukuza na kuimarisha elimu ya Juu nchini kupitia ufadhili wa mafunzo hayo na kuagiza wahusika katika Wizara anayoisimamia kuhakikisha vikao vya kitaaluma vinafanyika ili mafunzo hayo yaweze kuanza kwa wakati uliopangwa.

Katibu Mkuu Akwilapo pia ameahidi kuweka wazi kwa Watanzania kuhusu kuwepo kwa fursa hiyo ya kusoma programu za Kiingereza nchini Ufaransa ili Watanzania waweze kuchangamkia fursa hiyo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni