Jumanne, 1 Septemba 2020

SEMAKAFU: VYUO VYA FDC TOENI MAFUNZO YENYE UHITAJI NA AJIRA

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu amevitaka Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi (FDCs) kujikita katika kutoa mafunzo ya fani zinazopendwa na zinazotoa ajira badala ya kuendelea kuwa na fani ambazo hazina wanafunzi katika eneo husika.


Dkt. Semakafu ametoa agizo hilo alipofanya ziara ya kukagua ukarabati na uendeshaji wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Same kilichopo Mkoani Kilimanjaro ambapo amesema ni vizuri vyuo  vikajiimarisha kwenye utoaji mafunzo kwa fani zenye wanafunzi  wengi na kuachana na zile zenye wanafunzi wachache.
Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu akizungumza na baadhi ya watumishi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Same baada ya kukagua ujenzi na ukarabati wa miundombinu chuoni hapo.

“Kuanzia mwaka huu, kila chuo cha wananchi kitafundisha fani ambazo zinahitajika katika maeneo husika kwa maana ya kuwa na wanafunzi wa kutosha, hakuna chuo chochote kusajili fani ambazo zina wanafunzi wachache ama chini ya kumi na mbili, Serikali haiajiri walimu kufundisha wanafunzi wawili hivyo hakuna haja ya kuweka fani ambazo hazina wanafunzi wa kutosha,” amesisitiza Dkt. Semakafu.

Aidha, Naibu Katibu Mkuu huyo amesema mpango wa 'Elimu haina mwisho' unaotolewa katika vyuo hivyo ni utaratibu wa kutoa fursa kwa watoto waliokatisha masomo kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo za kiuchumi na kijamii ili kuwasaidia kupata elimu na ujuzi wa kuwawezesha kuendelea na masomo na kuendesha maisha yao pindi watakapohitimu hivyo wanapaswa kufundishwa kama wanafunzi wengine bila kuwatenga.  
Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu akitoa maelekezo ya namna ya kuboresha eneo la utoaji wa mafunzo ya umeme wa magari kwa Kaimu Mkuu wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi, Edward Mdee.

Amesema Serikali iliamua watoto hao wasome katika vyuo hivyo kupitia mfumo usio rasmi bila malipo yoyote kwa lengo la kuhakikisha wanapata fursa nyingine ya kuendelea na masomo na kuutaka Uongozi wa chuo cha Maendeleo Same  kuwarudisha chuoni wanafunzi wote walioacha masomo kwa sababu mbalimbali ili waweze kumaliza masomo yao.

“Tumeanza programu hii kwa lengo la kupata watoto wote walioacha shule na ndio maana unaona hata wasichana walioacha shule kutokana na changamoto mbalimbali tumewarudisha katika mfumo huu ili waje waendelee na masomo na na wale wenye watoto hata tuna shule za chekechea kwa ajili ya watoto wao,” amesema Dkt. Semakafu.

Naibu Katibu Mkuu Dkt. Semakafu amekagua miundombinu iliyokarabatiwa na kuboreshwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ambapo ameuagiza uongozi wa chuo hicho kufanya marekebisho katika baadhi ya miundombinu ambayo haikukarabatiwa vizuri.
Kaimu Mkuu wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii Same, Edward Mdee akitoa taarifa  ya chuo hicho kwa Naibu Katibu Mkuu, Dkt. Ave Maria Semakafu alipofika chuoni hapo kukagua maendeleo ya chuo hicho.
Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Same, Edward Mdee  ameishukuru Wizara kwa ukarabati ambao umefanyika chuoni hapo, na kusema kuwa chuo hicho chenye wanafunzi 301 kipo katika mkakati wa kuboresha utoaji wa mafunzo ili kuhakikisha kinatoa vijana wenye ujuzi na maarifa yatakayowawezesha vijana wa Same kujiajiri ama kuajiriwa.
Muonekano wa baadhi ya majengo ya miundombinu ya Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Same yaliyojengwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni