Jumanne, 31 Oktoba 2017

Waziri Ndalichako ashiriki mkutano wa UNESCO, nchini Ufaransa.


Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni -UNESCO -IRINA BOKOVA amesema Tume hiyo   ina nguvu kwa sababu ya ushirikiano inaoupata kutoka kwa nchi wanachama, hivyo ameziomba  nchi hizo kuendelea kufanya kazi kwa ushirikiano ili kufikia malengo waliyojiwekea.

Bukova ameyasema hayo hii leo wakati wa ufunguzi wa mkutano mkuu wa 39 wa UNESCO unaohusiha nchi wanachama duniani kote ambapo amesisitiza pia suala la kudumisha amani, upendo miongoni mwa nchi hizo.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako pamoja na Balozi wa Tanzani nchini Ufaransa balozi Samweli Shelukindo wameshiriki mkutano huo.


Alhamisi, 19 Oktoba 2017

Mradi wa kuwawezesha watoto wa kitanzania kupata elimu wazinduliwa


Kaimu Mkurugenzi mafunzo ya Ualimu Basiliana Mrimi  amezindua mradi wa shilingi milioni 500 utakaosaidia kuimarisha Ufundishaji na ujifunzaji kwenye Chuo cha Ualimu, Patandi kilichopo mkoani Arusha.

Akizundua Mradi huo kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Mrimi amesema  mradi huo utasaidia Kupima macho watoto wa shule za msingi na kuwapatia vifaa wanafunzi wenye uoni hafifu, Kutoa mafunzo kazini kwa wakufunzi 12 na walimu 4 wa shule za msingi zilizopo kwenye mradi.

Pia mradi huo utasaidia Kusomesha mkufunzi 1 kwa ngazi ya Shahada ya Uzamivu (PhD), Kusomesha wakufunzi 4 kwa ngazi ya Shahada ya Uzamili (Masters) na kuwa mradi huo unatekelezwa kwa ushirikiano wa Tanzania na Norway.


Jumatano, 18 Oktoba 2017

Waziri Ndalichako azindua ufadhili wa wanafunzi unaotolewa na Barclays


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amewataka wanafunzi kutumia mitandao ya kijamii kwa ajili ya kupata taarifa zitakazowasaidia kutekeleza fursa mbalimbali za kujiletea Maendeleo.
Waziri Ndalichako ameyasema hayo leo  wakati wa uzinduzi wa Twende kazi na Balozi mwanafunzi unaohusu ufadhili wa masomo kwa wanafunzi  23 wa shahada ya kwanza ya Chuo Kikuu cha Dar es salaam na kusisitiza kuwa taasisi nyingine ziige mfano huo wa Barclays wa kufadhili wanafunzi.

Pia Barclays imewasaidia vijana 32 Kati ya 200 kuwatafutia ofisi ili kufanya kazi kwa vitendo kwa ajili ya kuwajengea uwezo wa kuwa tayari kwa kazi.

Uzinduzi huo pia umehudhuriwa na Mkurugenzi wa Elimu ya Juu, Profesa Sylivia Temu.



Ijumaa, 13 Oktoba 2017

Waziri: Ndalichako: Shule ya nyasi zitabaki kuwa historia

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako leo amekagua na kufungua ujenzi wa vyumba vya madarasa katika shule ya msingi kilole, Matondoro,  na Kilimani na kuweka jiwe la msingi bweni la wasichana katika shule ya Sekondari Semkiwa  Wilayani Korogwe Mkoani Tanga.

Akizungumza Mara baada ya kukagua utekelezaji wa miradi hiyo Waziri Ndalichako amesema  suala la nchi kuwa na shule au vyumba vya madarasa vya nyasi litabaki kuwa historia kwa kuwa serikali ya awamu ya Tano inahitaji wanafunzi wapate Elimu bora inayoenda sambamba na uboreshaji wa miundombinu na hicho ndicho kinachofanyika hivi sasa.

Akizindua bweni moja la wasichana katika shule ya Sekondari Semkiwa waziri Ndalichako ameahidi kutoa kiasi cha shilingi milioni kumi kwa ajili ya kununulia vitanda na magodoro ili bweni hilo lianze  kutumika mara moja.

Pia amewataka watanzania kwa ujumla kuendelea kumuunga mkono Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli kwa namna anavyojitoa  katika kuwatumikia Wananchi wanyonge kwa lengo la kuliletea Taifa Maendeleo.

Ujenzi wa vyumba hivyo vya madarasa,na  vyoo umetekelezwa  na Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia kupitia mradi wa Lipa kulingana na matokeo, (EP4R).




TANGAZO


Jumatano, 11 Oktoba 2017

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa Dkt. Hussein Mwinyi wampokea Mtukufu Agha Khan


Mtukufu Aga khan muda mfupi Mara baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa kimataifa jijini Dar es Salama na amepokelewa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako pamoja na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa Dkt. Hussein Mwinyi.



Mtukufu Aga Khan akikagua gwaride lililoandaliwa kwa ajili yake muda mfupi  baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa Kimataifa jijini Dar es salaam.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolonia Profesa Joyce Ndalichako, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa Dkt. Hussein Mwinyi wakiwa katika picha ya pamoja  na Mtukufu Aga Khan ambaye amewasili leo.




Jumanne, 10 Oktoba 2017

Mradi wa TEHAMA wazinduliwa Mkoani Pwani


Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo amezindua mradi wenye thamani ya  zaidi ya shilingi bilioni 4 wa ujifunzaji na ufundiashaji wa TEHAMA kwa shule za Sekondari.
Akizindua mradi huo mkoani Pwani hii leo Dkt. Akwilapo amsema Serikali inahitaji kuona mradi huu unakuwa  endelevu na usiishie katika mkoa wa Pwani pekee bali usambae kwa nchi nzima.
Pia amewataka waratibu wa mradi huo - gesci -  kuhakikisha mpango huu unafanikiwa kwa kushirikisha  wadau wote wa Elimu ili mradi  ufanikiwe.
Dkt. Akwilapo amesema TEHAMA ni nyenzo muhimu katika ulimwengu wa mawasiliano, na kwa sasa ndiyo nyenzo kuu ya utoaji na usambazaji wa taarifa kwa umma.
Katibu Mkuu Akwilapo amewataka wale wote wenye miradi au mipango ya namna hiyo wawasiliane na wizara ili miradi yao iweze kuratibiwa na  kutekelezwa kwa taratibu za Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.
Mradi huo unatekelezwa katika baadhi ya nchi za Afrika ikiwemo Tanzania, Kenya, na Cotedvoire