Jumanne, 5 Desemba 2017

Chuo cha Ufundi Arusha chatakiwa kukamilisha ukarabati ili kuwezesha vifaa vilivyonunuliwa kutumika.
Naibu waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha amekitaka chuo cha Ufundi cha Arusha kukamilisha ukarabati na upanuzi wa karakana  zake ili kuwezesha vifaa vya kisasa vilivyonunuliwa vianze kutumika.

Naibu waziri Ole Nasha ametoa agizo hilo alipofanya ziara katika Chuo hicho kilichopo mkoani Arusha ili kujionea utendaji kazi, ambapo amesisitiza kuwa serikali ya awamu ya tano imejielekeza katika kuboresha elimu ya ufundi ili kufikia malengo ya Tanzania kuwa nchi ya viwanda.

Ole Nasha amesema kutokana na umuhimu huo serikali nimeamua kuwekeza katika uboreshaji wa vyuo vinavyotoa Elimu ya ufundi kwa kununua  vifaa vya kisasa na kukarabati miundombinu ya vyuo hivyo ili viweze kuzalisha raslimali watu watakaowezesha nchi kujenga uchumi wa viwanda.

 Naibu waziri amesema chuo hicho kimepata vifaa vya kufundishia na kujifunzia vya kisasa vilivyogharimu kiasi cha shilingi bilioni 14 kutoka nchini Australia ikiwa ni  sehemu ya jitihadi zinazofanywa na serikali ya kuboresha namna ya utoaji wa elimu ya Ufundi kwa lengo kusaidia kuzalisha vijana wengi wenye taaluma ya kisasa katika ufundi.

Ole Nasha amevitaka vyuo vyote vya ufundi kutambua kuwa vina jukumu kubwa la kuwatengeneza vijana watakaokuwa na weledi na umahiri katika kuchangamkia fursa za kazi zitakazokuwa zikipatikana katika miradi mikubwa ya maendeleo.


Kwa upande wake  Kaimu Mkuu wa Chuo Dkt. Erick Mgaya amesema vifaa vya kisasa vilivyonunuliwa vitawezesha kurahisisha zoezi zima la ujifundishaji na ujifunzaji kutokana na kuongezeka kwa udahili. 



Vijana watakiwa kuwa na hofu ya Mungu.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amesema  Mipango ya Taifa haliwezi kufanikiwa bila kuwa na vijana waadilifu,wachapakazi na wenye hofu ya mungu  hivyo amewataka vijana kuzingatia masomo ili kuweza kufikia malengo yanayikusudiwa Katika Taifa.

Waziri Ndalichako amesema hayo mwishoni mwa wiki wakati wa ibada maalumu iliyifanyika katika kanisa la City Christian Center lililopo Upanga Jijini Dar es Salaam ambapo amesema ili mtu yeyote afanikiwe katika maisha lazima hofu ya mungu iwepo katika maisha ya kila siku.

Waziri Ndalichako amesema vijana wengi wamekuwa wakitumia muda wao mwingi kufanya mambo ambayo siyo msingi wa maisha kama vile kujiingiza  kwenye makundi ya utumiaji wa dawa za kulevya, uporaji, unywaji wa pombe vitendo ambavyo havina faida na matokeo yake ni kijana kuangamia.

Kwa upande wake Askofu Mkuu wa Kanisa hilo la City Christian City Dkt. Reinwell Mwenisongole amepongeza juhudi zinazofanywa na serikali UA awamu ya Tano katika kusimamia Elimu ikiwa ni pamoja na kuongeza udahili katika vyuo vikuu, kujenga na kuboresha miundombinu ya vyuo vikuu kwa lengo la kusaidia kuongeza wataalamu ili kutimiza azma ya serikali ya kufikia uchumi wa viwanda.

Askofu Mwenisongole amesema kanisa la kanisa la Christian Center lilianzishwa mwaka 1978 kwa lengo la kuwasaidia vijana kuwa na hofu ya mungu.




Jumapili, 3 Desemba 2017

Naibu Waziri Ole Nasha aelekeza kuwekwa vituo vya upimaji katika mipaka yote nchini

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha ameiagiza Tume ya Nguvu za Atomiki kuhakikisha inaweka vituo vya ukaguzi wa viwango vya mionzi kwa bidhaa zote zinazoingia na kutoka nchini katika mipaka yote kwa lengo la kudhibiti mionzi katika bidhaa hizo. 

Naibu Waziri ametoa rai hiyo jijini Arusha alipotembelea Tume hiyo ili kujionea jinsi inavyofanya kazi, ambapo amesema ni muhimu vituo hivyo kuwekwa katika mipaka  ili  kuhakikisha bidhaa zinazoingia na kutoka nchini zinakuwa na viwango vya mionzi inayokubalika kimataifa.

Naibu Waziri Ole Nasha ameitaka Tume hiyo kutokuishia katika kutekeleza majukumu ya kudhibiti na kuhamasisha matumizi bora ya mionzi bali inapaswa kuanza kuangalia namna bora ya kuhamasisha matumizi chanya ya nyuklia kwa maendeleo ya taifa katika nyanja za Afya,  Kilimo,  maji  na teknolojia.

Naibu Waziri Nasha pia  alitembelea na kukagua  maendeleo ya ujenzi wa maabara ya kisasa kwa ajili ya upimaji wa ubora wa vifaa mbalimbali vya mionzi ikiwemo vifaa tiba vya Tume hiyo, maabara hiyo inajengwa na fedha za serikali kiasi cha shilingi bilioni mbili.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya nguvu za Atomiki Brigadia Jenerali Fulgence Msafiri amesema kutokana na upungufu mkubwa wa watumishi walio na weledi katika Teknolojia ya nyukulia imefanya Taasisi  hiyo kukosa  watumishi kutokana na kuanzishwa kwa vituo vya kudhibiti uingizwaji wa bidhaa katika mipaka ya Rusumo,  Mtukula,  Kabanga, Kigoma,  Tunduma,  Kasumulu na Daraja la Mkapa. 




Jumamosi, 2 Desemba 2017

Dkt. Semakafu: Simamieni Mfumo wa menejimenti ya viashiria hatarishi.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Avemaria Semakafu amewataka wakurugenzi wa Idara,  wakuu wa Vitengo na Taasisi zilizo  chini ya Wizara kuhakikisha wanasimamia  mfumo wa menejimenti ya viashiria hatarishi ili kudhibiti vishiria hatarishi vinavyoweza kukwamisha malengo ya Wizara kufikiwa.

Dkt Semakafu amesema hayo mjini Morogoro wakati wa kufunga mafunzo ya menejimenti ya viashiria hatarishi yaliyoendehswa na Wizara hiyo kwa lengo la kuwajengea uwezo  watumishi wa wizara hiyo wa ili kuwa na  uelewa wa namna ya kutambua vikwazo vinavyoweza kukwamisha utekelezaji wa majukumu yao.

Naibu Katibu Mkuu Semakafu amesema mafunzo hayo  yataiwezesha Wizara  kuwa na mfumo thabiti wa kushughulikia viashiria hatarishi na hatimae kuwa na daftari linaloainisha viashiria hatarishi pamoja na mikakati ya udhibiti.

Aidha Dkt. Semakafu amewataka Washiriki wote kuhakikisha wanafanyia kazi kikamilifu maudhui yaliyopatikana katika mafunzo hayo ikiwa ni pamoja na kuzingatia miongozo ya Serikali katika kutekeleza shughuli mbalimbali za Wizara.

Pia amemtaka mkaguzi mkuu wa ndani Anna Mhere kuhakikisha anaweka vigezo vya uchaguzi wa waratibu wa viashiria hatarishi katika idara na vitengo ili kupata waratibu ambao kweli watakwenda kutekelezamajukumu yao.

Mafunzo ya menejementi ya Viashiria hatarishi yalianza Novemba 27 na kukamilika Desemba 2, 2017  ambayo yalihusisha Wakurugezi wa Idara, Wakuu wa  Vitengo ndani ya Wizara pamoja na Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Wizara, na Wakurugenzi wasaidizi wa Wizara.

Wengine walionufaika na mafunzo hayo ni Wakuu wa Vyuo vya Elimu ya Ualimu, Wathibiti Ubora wa shule  Kanda, Wakaguzi wakuu wa ndani wa Wizara na Taasisi, Wakuu wa Miradi na wajumbe wanne kutoka kila idara na  Vitengo vya Wizara.






Alhamisi, 30 Novemba 2017

Chuo Kikuu Huria chatakiwa kupanua wigo wa udahili.


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kassim Majaliwa amekitaka Chuo kikuu Hiria nchini kuhakikisha kinaongeza ubora wa utoaji Elimu na kupanua wigo wa udahili kwa wanafunzi wa chuo hicho.

Waziri Mkuu Majaliwa ametoa kauli hiyo wakati wa mahafali ya 33 ya Chuo hicho ambayo yamefanyikia mkoani Singida na kusisitiza kuwa Umuhimu wa Chuo kikuu huria uko bayana katika kuhakikisha malengo ya serikali ya kutekeleza sera ya uchumi wa viwanda inafikiwa kupitia wataalamu wanaomaliza chuoni hapo.

Waziri Majaliwa amesema Serikali ya awamu ya Tano inatambua na inaunga mkono juhudi zinazofanywa na uongozi wa chuo hicho huku wakisisitizwa kuzingatia vigezo, taratibu za utoaji wa Elimu iliyo bora ili wapatikane wataalamu ambao ni bora kwa maslahi ya Taifa.
Kwa upande wake Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amesema Serikali inatambua mchango wa Chuo hicho katika kipindi cha miaka 25 ambapo kimekuwa kikitoa  Elimu katika masafa ya mbali hali ambayo inahitaji mwanafunzi kuwa na nidhamu ya hali ya juu ili kifikia malengo.

Kutokana na juhudi hizo Waziri Ndalichako ameahidi Serikali itaendelea Kuimarisha miundombinu ya Tehama ili Elimu hiyo ya masafa iweze kuwafikia watu wengi zaidi.
Waziri Ndalichako amewataka wahitimu kutumia vyema ujuzi na kuhakikisha wanaimarisha utendaji kazi katika serikali na hata Sekta binafsi.

Pia amewataka wahitimu kujenga nadhani pamoja na kuwa na ari katika  uwajibikaji ikiwa ni pamoja na kuwa mabalozi katika Shughuli ambazo watakuwa wanazifanya.






Jumatatu, 27 Novemba 2017

Waziri Ndalichako: Watendaji wajibikeni acheni kulipana stahili ambazo hazifuati miongozo na nyaraka za Serikali

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amezitaka Taasisi zilizochini ya Wizara yake kuwajibika katika nafasi zao za uongozi na siyo kusubiria mpaka kiongozi wa juu aibue changamoto zinazojitokeza katika maeneo yao.

Waziri Ndalichako amesema hayo leo mkoani Morogoro wakati wa Kikao kazi kilichohusisha  Menejimenti ya Wizara na Taasisi zake cha kujadili na kujengeana uwezo kuhusu namna  bora ya kubaini na  kukabiliana na viashiria hatarishi katika maeneo ya kazi.(Risk Identification and Risk Managment).
Waziri Ndalichako amesema kupitia kikao kazi hicho watendaji wataweza kujifunza na kubaini mapema viashiria ambavyo vitaonekana kukwamisha utekelezaji wa mipango ya wizara.
"lengo  hapa ni kuzuia madhara badala ya kusubiri madhara yatokee, hivyo kupitia kikao kazi hiki watendaji watajifunza kwa lengo la kuzuia na kutekeleza malengo ya Wizara kama yalivyokusudiwa,"amesema Waziri Ndalichako
Waziri Ndalichako pia amezitaka Taasisi na Watendaji wa Wizara hiyo kuanzia leo kuacha mara moja kulipana stahili ambazo hazifuati miongozo na nyaraka za serikali.
Profesa Ndalichako ametaja baadhi ya stahili ambazo zimekuwa zikilipwa bila kufuata taratibu na miongozo hiyo kuwa ni pamoja na posho za kujikimu, Nyumba,  umeme na simu.
Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Elimu ,  Sayansi na Teknolojia Dkt.  Leonard Akwilapo amesema mkutano huo umelenga kuondoa viashiria hatarishi ambavyo vimekuwa vikikwamisha ufanisi katika utendaji kazi wa wizara na kuwataka washiriki wa mkutano huo kuandaa mpango mkakati wa kuweza kutambua mapema viashiria hatarishi na kuvifanyia kazi ili kufikia malengo  ya wizara.
Kikao kazi hicho ambacho kimeanza leo kitahusisha pia  Wakurugenzi wasaidizi, waratibu wa miradi na wasaidizi wa miradi, wathibiti ubora wa shule kanda, wakuu wa vyuo vya Elimu ya Ualimu, na watumishi kutoka kila Idara wa wizara hiyo.



Rais Magufuli azindua hospitali ya Mloganzila

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amezindua rasmi hospitali ya Taaluma na Tiba ya chuo kikuu cha afya na sayansi shirikishi MAMC, kilichopo wilaya ya Ubungo mkoani pwani ambapo amewataka Wakala wa Majengo ya Serikali (TBA) kuhakikisha wanakamilisha mara moja ujenzi wa mabweni, madarasa na kumbi za mihadhara katika Chuo hicho.

Rais Magufuli ametoa rai hiyo wakati wa uzinduzi wa hospitali hiyo ambapo amesema  tayari serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 13 kwa ajili ya ujenzi huo na kuwa Kati ya fedha hizo tayari  kiasi cha shilingi bilioni Nne kimelipwa kwa TBA  ili kuanza ujenzi huo na kwamba ujenzi utakapokamilika utawezesha udahili wa wanafunzi 15,000 wa afya na tiba kwa mara moja tofauti na ilivyokuwa awali wanafunzi 4500 Pekee ndiyo walioweza kudahiliwa. 

Rais Magufuli pia ameitaka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknojia na wizara ya Afya kushirikiana kwa pamoja ili kuhakikisha hospital hiyo inatekeleza majukumu yake kwa weledi ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Wakati wa uzinduzi huo Rais Magufuli amesifu na kupongeza jitihada zilizofanywa na Serikali ya awamu ya Nne chini ya uongozi wake Rais mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete za kuhakikisha eneo la ujenzi linapatikana na ujenzi unafanyika na hatimaye wananchi kupata huduma za afya.

Naye Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia profesa Joyce Ndalichako amesema uwepo wa Chuo hicho chenye mitambo na vifaa vya kisasa kutalisaidia Taifa kupata wataalamu wenye uwezo ambao itsaidia kuondoa changamoto ya uhaba wa wataalnu wa afya hapa nchini.