Alhamisi, 6 Septemba 2018

ALIYOYASEMA WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA PROF. JOYCE NDALICHAKO LEO WAKATI WA MAHOJIANO NA TBC TAIFA KUHUSU MUSWADA WA SHERIA YA BODI YA KITAALAMU YA WALIMU


- Lengo la Bodi ni kuwa na Muundo na Chombo Cha Kisheria ili kutambua rasmi taaluma ya Ualimu kama zilivyo taaluma nyingine

- Ili kutimiza malengo yaliyowekwa na Serikali katika Elimu, thamani ya walimu ni jambo ambalo linapewa kipaumbele sana.

-Muswada wa Sheria ya bodi ya kitaalamu ya walimu umekuwa shirikishi katika hatua zote ikiwa ni pamoja na kuwashirikisha Walimu,Maafisa Elimu wa Wilaya, Mikoa,Wathibiti Ubora,Chama Cha Walimu Tanzania,Taasisi mbalimbali na Wizara ikiwemo ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI).

- Wadau wengine walioshirikishwa Kuanzia hatua za awali ni pamoja na Haki Elimu, CHAKAMWAKA, TAPIE, TAMONGSCO na Mtandao wa Elimu Tanzania(TEN/MET)

- Malengo ya Bodi hii ya walimu hayafanani na chombo kingine, vyama vingine vinaangalia maslahi ya walimu wakati bodi inaenda kuleta hadhi kwa kutambua walimu wote waliopo na wasiokuwepo madarasani.

-Tume ya Utumishi wa walimu imejikita katika utumishi kwa maana ya kuangalia orodha ya walimu walioajiriwa na serikali na uratibu wa masomo wakati bodi itaangalia mabadiliko mbalimbali katika dunia ikiwa ni pamoja na kuangalia nafasi za kuwaendeleza walimu.

-Bodi pia itasimamia vigezo kwa kuhakikisha mwalimu lazima awe amehitimu katika Chuo kinachotoa mafunzo, pia bodi itasimamia suala la maadili kwa walimu.

-Bodi ya kitaalamu ya walimu itakuwa na jukumu la kupokea malalamiko, kuchambua na kuyapatia ufumbuzi malalamiko ya Walimu wachache ambao wamekuwa wakifanya matendo ambayo ni kinyume na maadili ya Ualimu.

-Bodi itatoa fursa kwa walimu kujadili kwa kina masuala yao ya kitaalamu kwa lengo la kuyapatia ufumbuzi.

-Waziri Ndalichako pia amelaani vikali vitendo vinavyofanywa na baadhi ya walimu vya kutoa adhabu kwa wanafunzi na ameonya walimu kuacha kumalizia hasira zao kwa wanafunzi.

-Waziri amesema uchapaji  hovyo  wa viboko kwa wanafunzi ni kinyume na taratibu za Wizara, sasa kuwepo kwa Bodi ya kitaalamu itahakikisha inawabana walimu watakaokwenda kinyume na taratibu.

- Waziri amewataka walimu kuacha mara moja tabia za kuchapa wanafunzi hovyo na badala yake wawapende watoto na wahakikishe wanawasidia katika kuwakuza kwenye maadili na malezi yanayokubalika kwenye Taifa.

Jumanne, 4 Septemba 2018

RAIS MAGUFULI AWEKA JIWE LA MSINGI UJENZI WA CHUO CHA UALIMU MURUTUNGURU


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt John Magufuli leo ameweka jiwe la msingi kwa ajili ya upanuzi wa Chuo Cha Ualimu Murutunguru, kilichopo Wilayani Ukerewe mkoani Mwanza.

Rais Magufuli amesema Chuo Cha Murutunguru kwa sasa walimu wanaohitimu ni ngazi ya cheti, lengo la serikali ni kianze kutoa ngazi ya Diploma na baadae kikiongezewa miundombinu kiweze kutoa shahada.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dk. John Pombe Magufuli akiweka Jiwe la Msingi katika Chuo cha Ualimu Murutunguru Wilayani Ukerewe mkoani Mwanza ambapo amewapongeza Viongozi wa Wizara ya Elimu kwa kusimamia vizuri miradi inayotekelezwa na Wizara hiyo.

Rais Magfuli pia amewapongeza Viongozi wa Wizara ya Elimu kwa kusimamia vizuri miradi inayotekelezwa na Wizara hiyo.

Pia Rais amewashukuru  washirika wa Maendeleo hususan nchi ya Uingereza kwa kuendelea kufadhili miradi ya Elimu.
Baadhi ya Watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia wakishuhudia uwekaji wa jiwe la Msingi kwa ajili ya upanuzi wa Chuo cha Ualimu Murutunguru kilichopo Wilaya ya Ukerewe Mkoani Mwanza. 

Upanuzi wa ujenzi wa Chuo hicho unahusisha jengo la Utawala, vyumba vya madarasa, bwalo la Chakula, hosteli za wanafunzi, jengo maalumu la kupokelea umeme na ujenzi wa mifumo ya Maji na umeme.
Muda mfupi baada ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako kumpokea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dk. John Pombe Magufuli kwa ajili ya kuweka Jiwe la Msingi la upanuzi wa Chuo cha Ualimu Murutunguru. 

Ujenzi huo utagharimu takriban bilioni mbili nukta Tatu na inatarajia kukamilika oktoba mwaka huu.
Muonekano wa vyumba vya madarasa katika Chuo cha Ualimu Murutunguru, ambapo leo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dk. John Pombe Magufuli ameweka jiwe la msingi ambalo linahusisha ujenzi wa Jengo la utawala, bwalo la chakula, hosteli za wanafunzi, jengo maalum la kupokelea umeme na ujenzi wa mifumo ya maji na umeme.  

Ijumaa, 31 Agosti 2018

KATIBU MKUU WIZARA YA ELIMU AWATAKA WAKUU WA VYUO VYA UALIMU KUFUATA TARATIBU KATIKA UTENDAJI


Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Leonard Akwilapo amewataka Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali kuacha kufanya kazi kwa mazoea badala yake wafuate taratibu wakati wa kutekeleza majukumu yao ya kikazi ikiwa ni pamoja na kushirikisha watumishi na wanafunzi wa Chuo taarifa za mapato na matumizi ya fedha.

Dk. Akwilapo ameyasema hayo leo Jijini Dodoma wakati alipokutana na Wakuuu wa Vyuo hivyo kwa lengo la kujadili mafanikio, changamoto na mikakati waliyonayo katika kuhakikisha majukumu na uendeshaji wa vyuo yanatekelezeka bila changamoto ili waweze kufikia azma ya kuandaa walimu bora.
Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Leonard Akwilapo akizungumza na Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali (hawapo pichani) katika kikao kazi cha kujadili mafanikio, changamoto na Mikakati bora ya kuwezesha Vyuo  kutekeleza majukumu yake bila changamoto Mkoani Dodoma. 

Pia Katibu Mkuu huyo amewataka Wakuu wa Vyuo kuwasirikisha wale wanaowasimamia katika kuandaa mikakati ya utendaji ili waweze kutoa mchango katika kutekeleza mikakati hiyo na kufikia malengo mapana ya Wizara ambayo ni kutoa Elimu bora.

Katika hatua nyingine Dk. Akwilapo amewataka Wakuu wa Vyuo hao kuanisha mahitaji ya rasilimali watu ambayo inahitajika vyuoni inayoendana na kozi zinazofundishwa katika Chuo husika ili kuepuka kuwa na rasilimaliwatu isiyoendana na mahitaji ya Chuo. 
Baadhi ya Wakuu wa Vyuo wakifuatilia maelekezo ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Leonard Akwilapo wakati wa kikao cha pamoja kilichofanyika leo  Agosti 31, 2018 katika Chuo Kikuu cha Dodoma Jijini Dodoma.  

Naye Mwenyekiti wa Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali ambaye pia ni Mkuu wa Chuo cha Ualimu Morogoro Agustine Sahili amesema wanaishukuru Wizara kwa kuandaa vikao vya aina hiyo kwani vinawasaidia kuwakumbishia taratibu za kazi na kuahidi kutekeleza yale yote waliyoagizwa ili kuimarisha utendaji katika maeneo ya kazi.

Kikao kazi hicho kimeshirikisha Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali 35 vilivyopo hapa nchini.
Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali wakiwa katika picha ya pamoja na Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Leonard Akwilapo 

PROF. MDOE AITAKA ESPJ KUACHA ALAMA NA KUTEKELEZWA KATIKA MUDA ULIOPANGWA


Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa James Mdoe ameutaka Mradi wa Kukuza Ujuzi na Stadi za Kazi kwa lengo la kuzalisha ajira (ESPJ) kuhakikisha inatekeleza vizuri malengo ya mradi yaliyokusudiwa ikiwa ni pamoja na kuonyesha thamani ya fedha ili Taifa liweze kufikia malengo ya nchi ya kufikia uchumi wa viwanda hadi ifikapo mwaka 2025.

Profesa mdoe ametoa maagizo hayo mkoani Morogoro wakati wa kikao kazi cha waratibu wanaohusika na mradi wa ESPJ kutoka kwenye Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na sekta binafsi na kusisitiza kuwa mradi huo unatakiwa kufanya mambo ambayo yataacha alama ikiwa ni pamoja na  kuhakikisha unafanyika katika muda uliopangwa.

“Bado tuko nyuma katika utekelezaji, wadau na viongozi wanajiuliza umuhimu wa huu mradi, sasa tutekeleze vizuri mradi  ili thamani ya fedha ionekane. Mradi huu upo kwenye moyo wangu nitafurahi kuona unaacha alama na katika kujifunza tuangalie namna mradi wa EP4R ulivyoacha alama, sasa ESPJ na yenyewe ifanye hivyo hivyo,”amesema Profesa Mdoe.
Naibu katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa James Mdoe akizungumza na Waratibu wa Mradi wa Kukuza ujuzi na Stadi za Kazi kwa lengo la kuzalisha ajira (ESPJ), hawapo pichani ambapo ameutaka mradi huo utekelezwe na uwe na matokeo chanya.

Naibu Katibu Mkuu huyo pia amesema kuwa kiuhalisia mradi umechelewa kuanza sasa katika kuutekeleza lazima umakini uwepo ili matokeo chanya ya mradi huo yaweze kuonekana.

Kikao kazi hicho kinahusu uwasilishaji wa  ripoti mbalimbali zinazohusu utekelezaji wa mradi , ikiwa ni pamoja na kufanyika majadiliano ya pamoja kwa lengo la kujengeana uwezo kutoka Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Elimu, Idara ya Elimu ya juu, Kitengo cha Sheria, Idara ya Sera na Mipango, mratibu kutoka ofisi ya TPSF, pamoja na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini.
Waratibu wa Mradi wa Kukuza ujuzi na Stadi za Kazi kwa lengo la kuzalisha ajira (ESPJ) wakiwa katika kikao kazi cha kujengeana uwezo mara baada ya kuwasilishwa kwa ripoti mbalimbali kuhusu utekelezaji wa mradi huo. Kikao hicho kinafanyika kwa siku mbili, Agosti 31 mpaka Septemba 1 mkoani Morogoro.


MINISTRY OF EDUCATION, SCIENCE AND TECHNOLOGY

SCHOLARSHIP TENABLE IN BRAZIL FOR THE ACADEMIC YEAR 2018/2019
Call for Application
The General Public is hereby informed that, the Republic of Brazil under the Coordination of the Improvement of Higher Education Personnel (CAPES) is offering PhD Scholarships to Tanzanian Citizen.  Successful candidates will be required to pursue their studies in various public higher learning institutions in Brazil for the academic year 2018/2019.  For more information the modes of application and other requirements please follow the provided links.
Mode of Application

All Applicants are requested to complete application online on http://www.inscricao.copess.gov.br/individual.

Through which you will find link that will guide you to register and fill application form and upload all documents required and finally submit online.

The following are the documents required to be uploaded as attachments:-

i                      Page of your Passport;
ii                   Birth Certificate ;
iii                 Academic Certificates ;
iv                 Academic Transcripts;

NB: Detailed information regarding the Scholarships can be accessed from the following webpage: http://www.inscricao.copess.gov.br/individual/cooperacao
International/multinational/pec-pg
This is issued by




Permanent Secretary
Ministry of Education, Science and Technology
University of Dodoma
College of Business and Law
Block 10
P .O. Box 10
40479 Dodoma.
Deadline for applications is 31th August, 2018

Alhamisi, 30 Agosti 2018

DK. SEMAKAFU: WATHIBITI UBORA WA SHULE HAKIKISHENI ELIMU INAYOTOLEWA NCHINI INAKIDHI VIGEZO.


Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. AveMaria Semakafu amewataka Wathibiti Ubora wa Shule nchini kutumia taaluma zao kuhakikisha kwamba Elimu inayotolewa nchini ni ile inayozingatia vigezo, kanuni na taratibu za nchini na si vinginevyo.

Dk Semakafu ameyasema hayo Mkoani Morogoro wakati wa kufungua mafunzo ya Muongozo wa Huduma ya Maji, Afya na Usafi wa Mazingira Shuleni (SWASH) kwa wathibiti ubora wa Shule wa Wilaya ambapo amesema kwa kufanya hivyo kutasaidia kujua changamoto zinazokwamisha upatikanaji wa Elimu bora katika maeneo yao.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Ave Maria Semakafu akizungumza na Wathibiti Ubora wa Shule wa Wilaya (hawapo pichani) wanaoshiriki mafunzo ya Muongozo wa Huduma ya Maji, Afya na Usafi wa Mazingira Shuleni (SWASH) yanayofanyika katika Chuo Cha Ualimu Morogoro mkoani Morogoro kuanzia Agosti 27 hadi 31, 2018

Dk. Semakafu pia amewataka Wathibiti ubora kufanya utafiti, kuainisha changamoto zilizopo katika maeneo mbalimbali ya shule pamoja na kuandaa ripoti na mapendekezo ambayo wanadhani Programu ya SWASH itaweza kusaidia kutatua.

“Mafunzo haya mliyoyapata yaende kuwasaidia katika kufanya tafiti, kuanisha changamoto zilizopo katika maeneo mbalimbali ya shule pamoja na kuandaa ripoti na kutoa mapendekezo, ambayo yatasaidia kuimarisha utendaji na kuwashirikisha wale ambao hawajapata mafunzo hayo kwa kuwa sasa mmekuwa na uelewa mpana kuhusiana na masuala ya huduma ya Maji, Afya na Usafi wa Mazingira Shuleni,” amesema Semakafu


Baadhi ya Wathibiti Ubora wa Shule wa Wilaya wakifuatilia hotuba ya Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Ave Maria Semakafu wakati akifungua mafunzo ya Muongozo wa Huduma ya Maji, Afya na Usafi wa Mazingira Shuleni (SWASH), mafunzo ambayo yanafanyika  mkoani Morogoro kuanzia Agosti 27 hadi 31, 2018.

Amewataka pia kuhamasisha upatikanaji wa maji safi na salama katika maeneo wanayofanyia kazi ikiwa ni pamoja na kuhakikisha Elimu ya afya na mazingira safi yanapatikana Shuleni ili watoto waweze kupata Eimu bila changamoto yoyote.

Mafunzo ya Muongozo wa Huduma ya Maji, Afya na Usafi wa Mazingira Shuleni   yameshirikisha Wathibiti Ubora wa Wilaya 48 kutoka Mikoa ya Dar es Salaam, Mtwara, Lindi, Pwani, Morogoro, Iringa, Singida na Manyara.
Wathibiti Ubora wa Shule wa Wilaya wanaoshiriki mafunzo ya Muongozo wa Huduma ya Maji, Afya na Usafi wa Mazingira Shuleni (SWASH) wakiwa katika picha ya pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Ave Maria Semakafu mkoani Morogoro

Jumatano, 29 Agosti 2018

SERIKALI HAITAMVUMILIA ATAKAYEFANYA SHULE KUTOKUWA SEHEMU SALAMA KWA WANAFUNZI


Serikali imesema haitavumilia mtu yeyote ambaye atafanya matendo yatakayoashiria kwamba shule si mahala salama kwa mwanafunzi, pamoja na kuwatia hofu wazazi waogope kuwaruhusu watoto kwenda kupata Elimu.

Kauli hiyo ya Serikali imetolewa leo na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknlojia Profesa Joyce Ndalichako siku moja baada ya kuwepo kwa taarifa juu   mwalimu Respicius Patrick wa Shule ya Msingi Kibeta iliyopo mkoani Kagera kumpiga hadi kumsababishia kifo mwanafunzi Sperius Eradious mwenye umri wa miaka 13 wa darasa la tano.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akiwakabidhi sheria na kanuni Wajumbe wa Bodi mpya ya Baraza la Mitihani Tanzania katika uzinduzi wa Bodi hiyo uliyofanyika jijini Dar es Salaam

Waziri Ndalichako amesema Shule ni mahala salama kwa wanafunzi kujifunza, kitendo hicho kilichofanywa na mwalimu huyo ni kinyume na malengo ya serikali  ambayo imekuwa ikiboresha Elimu na kufanya kazi kubwa ya kuhakikisha watoto wanapata Elimu bora na tena kwenye mazingira mazuri.

“ Suala ambalo limefanywa na huyu Mwalimu ni kinyume kabisa na maadili ambayo Mwalimu anatakiwa kuwa nayo, kwa umri ambao mwanafunzi alikuwa nao Mwalimu ndiyo alitakiwa awe msaada mkubwa wa kumuelimisha na kumfundisha mwanafunzi,niendelee kuwaomba Watanzania waendelee kuwa watulivu, wakati vyombo vya Sheria vinaendelea kufanya kazi yake,” alisema Waziri Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na wataalamu wa waandaaji wa walimu wa somo la hesabu (hawapo pichani) jijini Dar es Salaam, ambapo amewataka walimu kuangalia namna nzuri ya kumuandaa mwanafunzi kupenda somo la hesabu.

Katika hatua nyingine Waziri Ndalichako amewataka wataalamu wa somo la hesabu kuangalia namna bora ya kuimarisha ufundishaji wa somo la hilo ili kuwezesha walimu  kufundisha na kuhamasisha wanafunzi kupenda somo hilo.

Waziri Ndalichako amesisitiza hilo katika kongamano la tano la wataalumu wanaoandaa walimu wa somo la hesabu Barani Afrika kuwa ni muhimu kuangalia mbinu wanazopewa walimu wanaofundisha somo hilo kama zinawasaidia kufundisha kwa kutumia njia shirikishi.
Kongamano linalowakutanisha wataalamu wa hesabu linafanyika jijini Dar es Salaam kwa kwa lengo la kuimarisha ufundishaji wa somo la hesabu ambapo mgeni rasmi katika kongiomano hilo ni Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako.  

Kupitia kongamano hilo amewataka kuangalia pia namna nzuri ya kuwezesha walimu wa hesabu kuondoa dhana potofu kwa wanafunzi kuwa somo hilo ni gumu, na kusisistiza kuwa mwanafunzi akielewa hesabu inamuwezesha kumudu masomo mengine vizuri kutokanana kutumia zaidi mantiki katika kutatua hesabu.

Akiwa jijini Dar es salam Waziri Ndalichako pia amezindua bodi ya Baraza la Mitihani la Tanzania ambapo amewataka wajumbe wa Baraza hilo kuhakikisha mitihani inaandaliwa katika ubora unaotakiwa na wahakikishe wanakuwa  na umakini katika uendeshaji wa Kazi zote zinazohusiana na mitihani.