Jumatatu, 1 Oktoba 2018

NAIBU WAZIRI OLE NASHA AITAKA KAMPUNI YA UJENZI KUWASILISHA MICHORO NDANI YA WIKI MOJA


Naibu waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha ametoa wiki moja kwa mtaalamu Elekezi wa Kampuni ya Archquants Service Limited kuhakikisha inawasilisha michoro ya kazi za nje ya Chuo cha ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi Namtumbo kilichopo Mkoani Ruvuma ili ujenzi wa chuo hicho uweze kukamilika.

Mheshimiwa Ole Nasha ametoa agizo hilo wakati wa kukagua maendeleo ya ujenzi wa chuo hicho ambapo amesema ucheleweshwaji wa michoro hiyo unapelekea kuchelewesha ukamilishaji wa mradi huo.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akipokea taarifa ya Elimu ya Mkoa wa Ruvuma kutoka kwa Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Pololet Mgema wakati wa ziara ya kukagua miradi ya Elimu Mkoni huko.

Katika hatua nyingine Naibu Waziri Ole Nasha ameitaka Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi VETA kuhakikisha   wanaanzisha kozi ya ufundi wa zana za kilimo (Agro mechanics) katika Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi kilichopo Songea ili kupata vijana wengi watakaosomea fani hiyo.

Naibu Waziri amesema ukanda wa Nyanda za Juu Kusini unategemea sana kilimo, hivyo kuanzishwa kwa kozi hiyo kutasaidia wananchi wengi kupata uelewa wa kina kile wanachokisoma na baadae kutekeleza kwa vitendo.

 “Serikali inatilia mkazo Elimu ya ufundi na imejielekeza katika kuhakikisha inapanua fursa ya vijana wengi kupata Elimu ya ufundi na ndio maana  Serikali ya awamu ya Tano imeamua kuweka Vyuo vya VETA katika kila Wilaya na Mkoa,” alisisitiza Naibu Waziri Ole Nasha
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akipata maelezo kutoka kwa mwalimu wa somo la uchomeleaji (welding) Onesmo Pela katika Chuo cha Ufundi Veta Songea namna anavyotekeleza majukumu yake.

Naibu Waziri Ole Nasha yuko mkoani Ruvuma kwa ziara ya kikazi ya siku mbili kwa ajili ya kukagua miradi ya Elimu inayotekelezwa na Wizara ya Elimu, Sayasni na Teknolojia.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akikagua maendeleo ya ujenzi wa Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi cha Namtumbo kilichopo katika Wilaya ya Namtumbo Wilayani Ruvuma

DKT. SEMAKAFU AFUNGUA MAFUNZO YA FORCE AKAUNTI NA KUWATAKA WASHAURI ELEKEZI KUTIMIZA WAJIBU WAO

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ave Maria Semakafu amewataka washauri elekezi ( consultant) kuhakikisha wanatimiza wajibu  katika kutekeleza majukumu yao pindi wanapokabidhiwa miradi ya kusimamia, na kuwa haipendezi miradi inapoenda kukaguliwa kuwa na masuala ya kutumbuliwa.

Dkt. Semakafu amesema hayo leo mkoani Morogoro wakati akifungua mafunzo ya matumizi ya Force Akaunti ambao ni utaratibu unaotumika kwenye ujenzi au ukarabati kwa kutumia malighafi za ujenzi na mafundi waliopo eneo husika.



Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ave Maria Semakafu akizungumza wakati akifungua mafunzo ya matumizi ya Force Akaunti yanayofanyika mkoani Morogoro ambapo amewataka washiriki wa mafunzo kuwa wazalendo wanaposimamia miradi ya ujenzi inayotekelezwa na Serikali.

Dkt. Semakafu amesema Force Akaunti ikitumika vizuri inaonyesha thamani ya Fedha lakini pia utaratibu huo hauna mabadiliko ya gharama wakati wa kutekeleza ujenzi au ukarabati tofauti na kutumia mkandarasi katika kutekeleza miradi ya Serikali.

“Force Akaunti ipo kisheria na kinachohitajika ni uzalendo, pia fedha inayotengwa kwa ajili ya ujenzi haiguswi na kuwa  hii inatakiwa ioneshe thamani ya Fedha kwa maana matokeo makubwa kwa fedha kidogo,” alisisitiza Dkt. Semakafu.



Washiriki wa mafunzo wakiwemo Wakurugenzi wa Halmashauri, Wakurugenzi  na Wakurugenzi wasaidizi wa VETA, Maafisa VETA wakifuatilia  mafunzo ya Force Akaunti.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi Dkt. Noel Mbonde   amezitaka Mamlaka za Ufundi Stadi  VETA kuhakikisha zinaleta mabadiliko ili nchi iweze kufikia malengo ya uchumi wa viwanda.

Mafunzo hayo ya siku mbili yanaratibiwa na mradi wa kukuza Maarifa, Stadi na ujuzi (ESPJ) yanahusisha Wakurugenzi wa halmashauri za Kasulu,Ngorongoro,Kongwa,Nyasa, Wakurugenzi wa  Kanda VETA, Wakurugenzi wasaidizi kutoka Makao Makuu VETA, Maafisa kutoka VETA.


Picha ikimuonesha Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ave Maria Semakafu baada ya kuwasili katika ukumbi wa mkutano mkoani Morogoro akiwa ameongozana na  Mkurugenzi wa Ufundi na mafunzo ya Ufundi Stadi Dkt. Noel Mbonde, na mratibu wa mradi wa kukuza Maarifa, stadi na Ujuzi (ESPJ) Dkt. Keneth Hosea

Jumapili, 30 Septemba 2018

WAZIRI NDALICHAKO AAGIZA KUONDOLEWA KATIKA NAFASI ZAO VIONGOZI WA IDARA YA UALIMU

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara hiyo  Dkt. Leonard Akwilapo kuwaondoa mara moja Kaimu Mkurugenzi wa Ualimu Basiliana Mrimi na Mratibu wa Miradi wa idara hiyo  Fredrick Shuma katika nafasi zao kwa kushindwa kusimamia majukumu yao kwa weledi.

Waziri Ndalichako ametoa agizo hilo Wilayani Nzega mkoani Tabora alipokuwa akikagua maendeleo ya upanuzi wa Chuo cha Ualimu cha Ndala ambapo amesema viongozi hao wameshindwa kuzisimamia kampuni za ujenzi za Sky Ward na United Builders zilizopewa kazi ya kufanya upanuzi katika chuo hicho.


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na wanafunzi na watumishi wa chuo cha ualimu Ndala mara baada ya kukagua upanuzi wa Chuo hicho.

Waziri Ndalichako amesema kampuni ya Sky Ward ilipewa kiasi cha shilingi milioni 600 za awali kwa ajili ya kujenga majengo katika Chuo hicho toka mwezi wa saba lakini mpaka sasa hakuna kilichofanyika na wala hakuna taarifa yeyote inayoelezea kwa nini kazi hiyo imekwama.

Waziri Ndalichako amesema serikali haitaongeza muda uliowekwa katika Mkataba  ambapo ameagiza kampuni hizo  kufanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha kazi hizo zinakamilika kwa wakati.


“Sitaki kusikia maneno ninachotaka ni kuona kazi inayofanyika hapa ilingane na thamani ya fedha ambazo tumeshawalipa na baada ya siku 30 nitakuja kukagua kama kweli kazi imeanza,”alisisitiza Waziri Ndalichako.



Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akikagua moja ya nyumba iliyojengwa katika Chuo cha Ualimu Ndala ambapoo hajaridhishwa na kasi ya Wakandarasi wa ujenzi huo na ameagiza mradi huo ukamilike katika muda uliopangwa.



 Waziri huyo alisema Serikali haitasita kuvunja mkataba na Mkandarasi yeyote atakaeonekana hana uwezo wa kutekeleza mradi kwa mujibu wa mkataba.

Katika hatua nyingine Waziri Ndalichako alimtaka Mhandisi Mshauri kuhakikisha anawasimamia wakandarasi hao ili waweze kutimiza wajibu wao na kuhakikisha  kazi hizo inafanyika kwa viwango  na kwa wakati, endapo atashindwa  kuwasimia wakandarasi hao Serikali italazimika kumfukuza kazi.




Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akipokelewa na wakufunzi na watumishi wa Chuo cha Ualimu Ndala mara baada ya kuwasili chuoni hapo kwa ajili ya ziara ya kikazi

Jumatano, 26 Septemba 2018


UNITED REPUBLIC OF TANZANIA
MINISTRY OF EDUCATION, SCIENCE AND TECHNOLOGY

STUDY OPPORTUNITY TENABLE IN THE REPUBLIC OF KOREA FOR ACADEMIC YEAR 2019


1.0 Call for Application
The general Public is hereby informed that, the National Institute for International Education (NIIED) under the Ministry of Education of the Republic of Korea is offering one undergraduate study opportunity to a Tanzanian citizen for 2019 undergraduate Global Korea Scholarship (GKS).

2.0 Mode of Application
All applicants are required to complete application form and attach all requested documents. Instructions for this Scholarship are obtained in the following website http://www.studyinkorea.go.kr.

Application forms and attached documents should be submitted to the Korean Embassy not later than Tuesday 2nd October, 2018
PHYSICAL ADDRESS
19TH Floor Golden Jubilee Tower,
Ohio Street, City Centre,
P. O. Box 1154,
DAR ES SALAAM.




Issued by
Permanent Secretary,
Ministry of Education, Science and Technology,
College of Business Studies and Law,
Universities of Dodoma (UDOM) Building No. 10,
P. O. Box 10,
40479 DODOMA.

Jumanne, 25 Septemba 2018

WAZIRI NDALICHAKO ASISITIZA WADAU KUTUMIA TAKWIMU SAHIHI KATIKA MACHAPISHO YAO.


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amewataka wadau wa Elimu kuhakikisha wanatumia takwimu sahihi zilizotolewa na Mamlaka husika wakati wa kuandaa machapisho yao ili kuepuka kupotosha umma.


Waziri Ndalichako amesema hayo leo wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa mwaka wa kutathmini Sekta ya Elimu unaoshirikisha wadau wa ndani na nje ya nchi kuwa kipaumbele cha Serikali ya awamu ya Tano ni Elimu na ndio maana Wizara hiyo imekuwa ikitengewa bajeti ya kutosha na bajeti ya Wizara hiyo haijawahi kushuka.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akifungua Mkutano Mkuu wa mwaka wa kutathmini Sekta ya Elimu uliofanyika Jijini Dodoma. Waziri Ndalichako amewataka washiriki wa mkutano huo kujadili kwa kina mafanikio, changamoto na kuwa na mikakati ya pamoja itakayosaidia Serikali kufikia malengo waliojiwekea katika Sekta ya Elimu.

Waziri Ndalichako amesema kumekuwa na upotoshwaji wa takwimu zinazotolewa kwenye machapisho mbalimbali kuwa bajeti ya Wizara ya Elimu imeshuka hadi kufikia asimilia 56 suala ambalo Waziri Ndalichako amelikanusha na kueleza kuwa bajeti ya Wizara hiyo haijawahi kushuka na mpaka Juni 2018 bajeti ya Wizara hiyo ni asilimia 86.5.

“Bajeti ya Wizara ya Elimu haijawahi kushuka kwa kuwa kipaumbele cha serikali ya awamu ya Tano inayoongozwa na Rais John Magufuli ni Elimu, hivyo takwimu ambazo zimekuwa zikitolewa kwenye machapisho mbalimbali sio sahihi  na badala yake takwimu sahihi za bajeti ya Wizara ya Elimu ni asilimia 86.5 hadi kufikia Juni 2018,” alisisitiza Waziri Ndalichako.
Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa mwaka wa kutathmini Sekta ya Elimu unaofanyika Jijini Dodoma. 

Waziri Ndalichako amewaambia wadau wa Mkutano huo wa AJESR unaofanyika Jijini Dodoma kuwa Elimu ndio nyenzo muhimu inayotoa dira na muongozo ili kuhakikisha Taifa linakuwa na watu walioelimika kwa maendeleo ya Taifa katika kufikia uchumi wa viwanda na uchumi wa kati ifikapo 2025.

Waziri Ndalichako amewataka washiriki wa mkutano huo kujadili kwa kina mafanikio, changamoto na kuwa na mikakati ya pamoja itakayosaidia Serikali kufikia malengo waliojiwekea katika Sekta ya Elimu.
Wadau wa Elimu walioshiriki Mkutano Mkuu wa mwaka wa kutathmini Sekta ya Elimu wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako wakati wa Ufunguzi wa mkutano huo uliofanyika Jijini Dodoma.  

Mkutano huo wa mwaka wa kutathmini  Sekta ya Elimu umekuwa ukishirikisha wadau mbambali wa ndani nan je ya nchi  ulianza mwaka 2008 na umekuwa ukifanyika kila mwaka.

Kauli mbiu ya Mkutano huo ni “Upatikanaji wa Elimu bora kufikia Tanzania ya Viwanda” umeanza leo  na utakamilika Septemba 28, 2018. 

Alhamisi, 20 Septemba 2018

OLE NASHA: TCU NA BODI YA MIKOPO SHIRIKIANENI WANAFUNZI WAPATE MIKOPO KWA WAKATI

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia mheshimiwa William Ole Nasha ameiagiza Tume ya Vyuo Vikuu nchini  (TCU) kuhakikisha  inakamilisha uratibu wa udahili wa wanafunzi wa Elimu ya Juu ili kuwezesha zoezi la upangaji wa mikopo kufanyika  katika muda uliopangwa.

Naibu Waziri ametoa agizo hilo alipokutana na viongozi wa TCU  jijini Dar es Salaam ili kupata taarifa ya maendeleo ya udahili huo ambapo amesema kukamilika mapema kwa taratibu za udahili itawezesha Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB)  kupanga na kutoa mikopo kwa wanafunzi hao mapema.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe.Wiliam Ole Nasha akizungumza na viongozi wa Tume ya Vyuo Vikuu nchini alipokutana nao Jijini Dar es Salaam ili kupata taarifaya uratibu wa udahili wa wanafunzi wa Elimu ya juu.
“TCU mkifanya vibaya katika uratibu wa udahili Bodi ya Mikopo ndio inayoathirika kwani lawama zote huishia huko na  siyo TCU, hivyo ili kuweka utaratibu mzuri ni vyema mkafanyakazi kwa ukaribu na kushirikiana ili kuepuka changamoto zinazoweza kujitokeza,” amesisitiza Naibu Waziri huyo.

 Katika hatua nyingine,  Naibu Waziri amekutana na watendaji wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu na kuwataka kuhakikisha wanashughulikia kwa haraka upangaji na utoaji wa mikopo kwa wanafunzi ikiwa ni pamoja na kuwasadia wanafunzi pale zinapotokea changamoto .
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu Abdul Razaq Badru akizungumza na Naibu Waziri wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Wiliam Ole Nasha wakati wa kikao kilichofanyika jijini Dar es Salaam.

Jumatano, 19 Septemba 2018

PROF MDOE AMESEMA TANZANIA IKO TAYARI KUSHIRIKIANA NA IAEA KATIKA KUENDELEZA MATUMIZI SALAMA YA NGUVU ZA NYUKLIA


Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa James Mdoe ameongoza ujumbe wa Tanzania kwenye mkutano Mkuu wa 62 wa kimataifa wa kuendeleza matumizi salama ya nguvu za nyuklia unaofanyika mjini Vienna nchini Austria.

Akizungumza katika mkutano huo mjini Vienna Profesa Mdoe ameishukuru IAEA kwa kuisaidia nchi ya Tanzania mashine ya kuchunguza na kutibu saratani ambayo inatumika katika hospitali ya Bugando iliyopo mkoani Mwanza na misaada ya kiufundi katika hospitali ya Saratani ya Ocean Road iliyopo jijini Dar es salama pamoja na misaada ya kuwasomesha  wataalam kwenye eneo la Teknolojia  ya nguvu za nyuklia. 
     
Naibu Katibu Mkuu Profesa James Mdoe akizungumza katika mkutano wa kimataifa unaofanyika mjini Vienna, nchini Austria kuhusu matumizi salama ya nyuklia.

Profesa Mdoe pia amekieleza kikao hicho cha kimataifa kuwa nchi ya Tanzania iko tayari  kushirikiana na IAEA katika kuendeleza matumizi salama ya nguvu ya nyuklia. 

Balozi wa kudumu kwenye Mashirika ya Umoja wa Mataifa mjini Geneva nchini Uswis James Msekele naye anashiriki mkutano huo.

Mkutano huo ulioanza Septemba 17 utahitimishwa Septemba 21, 2018 huko mjini Vienna nchini Austria.