Jumamosi, 9 Machi 2019

BODI YA MIKOPO YA WANAFUNZI WA ELIMU YA JUU YATAKIWA KUBORESHA MIFUMO YA UOMBAJI MIKOPO

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mh. William Ole Nasha ameiagiza Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu  (HESLB) kuweka mifumo itakayowezesha vijana wengi kuomba mikopo ya kuwaendeleza kitaaluma kiurahisi.

Naibu Waziri Ole Nasha ametoa agizo hilo alipofanya kikao na watumishi wa Bodi hiyo jijini Dar es Salaam ambapo amesema kumekuwa na changamoto katika ujazaji wa fomu za maombi ya mikopo na kupelekea wengi kukosa mikopo hiyo.

"Bodi imekuwa ikifanya kazi nzuri sana katika suala zima la utoaji na ukusanyaji wa mikopo lakini  kuna changamoto katika ujazaji wa fomu za maombi ya mikopo wengi wanakosea sijui ni tatizo la taarifa ama elimu" amehoji Naibu Waziri.

 Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mh. Wiliam Ole Nasha akiongea na watumishi wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu wakati wa kikao na watumishi hao ambapo amewaagiza kuweka mifumo rafiki ya uombaji mikopo ili kuwezesha vijana wengi zaidi kuomba mikopo.

Ole Nasha ameitaka Bodi hiyo kuendelea kutoa elimu na taarifa kwa umma kuhusu namna bora ya ujazji wa fomu hizo ili kupunguza changamoto hiyo na kuwezesha wanafunzi wengi zaidi kupata lakini na kuongeza ufanisi katika shughuli za kiutendaji katika Bodi.

Amesema pamoja na changamoto hiyo pia zipo changamoto kwa baadhi ya Maafisa mikopo katika vyuo ambao wamekuwa wakijifanya miungu watu jambo ambalo limekuwa likichelewesha upatikanaji wa mikopo kwa wanaostahili na kupelekea lawama kupelekwa kwa Bodi hiyo.

"Ni vyema pia kuangalia namna bora ya kuwapata Maafisa Mikopo katika vyuo kwani nao ni sehemu ya tatizo katika kutoa mikopo, kuna wengine wanawadai wanavyuo fedha ili washughulikie maombi yao" amesema Ole Nasha.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mh. Wiliam Ole Nasha akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya watumishi wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu wakati wa kikao na watumishi hao.

Aidha, Naibu Waziri Ole Nasha ameipongeza  bodi kwa kufanya kazi nzuri katika urejeshaji wa Mikopo kwa kukusanya zaidi ya Sh.Bilioni 108 katika kipindi cha Julai 2018 hadi Januari 2019 ambapo lengo lilikuwa ni kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 150 kwa mwaka 2018/19.

Awali Mkurugenzi wa Habari wa Bodi ya Mikopo Omega Ngolle alimweleza Naibu Waziri kuwa changamoto zinazokwamisha ama kuchelewesha utoaji wa mikopo ni kwa baadhi ya taasisi kuchelewa kuwasilisha taarifa za matokeo au kutoa taarifa zisizo sahihi kwa Bodi hiyo.

WIZARA YA ELIMU YAGAWA KOMPYUTA 300 KWA VYUO VYA ELIMU VYA UMMA


Kiasi Cha Shilingi bilioni 1.2 kimetumika  kununulia vifaa vya TEHAMA kwa ajili ya vyuo vya ualimu vya umma  18, kwa  lengo la   kuimarisha ujifunzaji na ufundishaji katika vyuo hivyo ili  kuzalisha walimu bora  na wanaoendana na ulimwengu wa Teknolojia.

Kauli hiyo imetolewa na Kaimu Katibu Mkuu Profesa James Mdoe kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia wakati wa halfa ya utoaji vifaa mbalimbali vya TEHAMA zikiwemo Kompyuta 300, UPS 300 na Projector 100 kwa ajili  vyuo hivyo vya Ualimu.

Kaimu Katibu Mkuu Prof. James Mdoe akigawa vifaa vya Tehama kwa Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Umma nchini kwa lengo la kuboresha elimu ya Ualimu, hafla hiyo imefanyikia mkoani Dodoma.

Katika hotuba yake, Profesa Mdoe amesema serikali ya Tanzania inawashukuru  washiriki wa maendeleo ambao ni serikali ya CANADA kwa kufadhili mradi wa kuendeleza na kuboresha Elimu ya Ualimu  (TESP ) kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Profesa Mdoe pia amewaasa Wakuu wa Vyuo kutumia vifaa hivyo kwa malengo yaliyo kusudiwa na ametoa onyo kwa Wakuu wa vyuo wote wanauhujumu jitihada za serikali za kuboresha miundombinu ya vyuo vya Ualimu kuacha mara moja tabia hiyo na kuwataka watumishi wote  kutanguliza maslahi ya Taifa ikiwa ni pamoja na kuacha kufanya kazi kwa mazoea.

 
Vifaa mbalimbali vya Tehama zikiwemo Kompyuta, UPS na Projector kwa ajili ya kugawiwa kwenye Vyuo vya Ualimu vya umma 18.

“Nipende kuwasihi watumishi wote wa Wizara ya Elimu na hasa Idara ya manunuzi   kuzingatia Sheria, Taratibu na Kanuni  wakati wa kutekeleza majukumu."

Vyuo vya Ualimu vya Umma ambavyo vimepata vifaa hivyo ni pamoja na Dawaka, Ilonga, Mandaka, Mhonda, Murutunguru, Mamire, Ndala, Singachini, Shinyanga na Vikindu.

Kaimu Katibu Mkuu Prof. James Mdoe akizungumza na watumishi wa Wizara (hawapo) pichani wakati wa hafla ya kugawa vifaa vya Tehema mkoani Dodoma.


Vyuo vingine ni Patandi, Tarime, Mpuguso, Sumbawanga, Mpwapwa, Tukuyu , Morogoro na Korogwe.




Kwa upande wake Mwenyekiti wa Wakuu wa Vyuo vya Ualimu nchini Augustino Sahili ameiomba serikali kuharakisha kukamilisha mpango wa kuunganisha vyuo vyote vya Ualimu vya umma na Mkongo wa Taifa.
Baadhi ya Wakuu wa Vyuo vya Ualimu wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi ambaye ni Kaimu Katibu Mkuu Profesa James Mdoe (hayupo pichani) wakati wa ugawaji wa vifaa vya Tehama kwa Vyuo vya Ualimu. Hafla hiyo imefanyikia mkoani Dodoma.