Ijumaa, 21 Juni 2019

NAIBU WAZIRI OLE NASHA ATAKA WATOTO KULINDWA NA KUWEZESHWA ILI WAWEZE KUSHIRIKI FURSA MBALIMBALI ZA ELIMU

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha amesema Serikali  inatambua  na kuthamini umuhimu wa mtoto wa kitanzania na ndio maana imekuwa ikizifanyia kazi haki za msingi za mtoto ili aweze kuishi katika mazingira mazuri ikiwa ni pamoja na kupata elimu. 

Naibu Waziri Ole Nasha ameyasema hayo Jijini Dar es Salaam wakati wa maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika yaliyoandaiwa na Shirika la Wanawake katika Sheria na Maendeleo Afrika (WiLDAF) ambapo amesema watoto wanapaswa kulindwa na kuwezeshwa ili waweze kushiriki katika  fursa mbalimbali zilizopo kwenye elimu. 


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afirika yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam Juni 20, 2019.
 Amesema maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika yanatoa fursa ya kujadili changamoto na fursa katika kuhakikisha kuwa haki za mtoto zinalindwa na kwamba  Serikali imefanya jitihada kubwa na za makusudi katika kuhakikisha kuwa watoto wanapata haki zao za msingi katika jamii zetu za kitanzania.


Ole Nasha amezitaja jitihada hizo kuwa ni pamoja na kuridhiwa kwa mikataba mbalimbali ya Kimataifa inayolinda haki za watoto, kutunga  sheria zinazolinda haki za watoto dhidi ya uonevu na ubaguzi wowote na pia imepitisha Sera zinazowalinda na kuwapatia fursa watoto.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akichangia mjadala wakati wa maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Jitihada nyingine ni pamoja na ujenzi wa shule karibu na makazi ya watu ili kupunguza watoto kutembea umbali mrefu, ujenzi wa mabweni na pia  mafunzo mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuweka mkazo juu ya stadi za maisha, elimu ya afya ya uzazi na ujinsia katika shule za msingi na sekondari na vyuo vya ualimu.

Katika hatua nyingine Naibu Waziri Ole Nasha ameutaka umma kutambua kuwa jukumu la kuwaendeleza watoto kielimu ni la kila mmoja wetu na kwamba ifahamike kuwa watoto wa kike na wa kiume wote ni sawa, hivyo hatuna budi kuwapunguzia watoto wa kike mzigo wa kazi za nyumbani ili wapate muda wa kujisomea sawa na ilivyo kwa watoto wa kiume.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akipokea risala kutoka kwa mmoja wa watoto walioshiriki Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika Jijini Dar es Salaam.
Siku ya Mtoto wa Afrika huadhimishwa Juni 16 ya kila mwaka ambapo kwa mwaka 2019 maadhimisho hayo Kitaifa yamefanyika Mkoani Geita na yalikuwa na Kauli Mbiu isemayo “Mtoto ni Msingi wa Taifa Endelevu: Tumtunze, Tumlinde na Kumuendeleza.”

NDALICHAKO AZINDUA MABARAZA YA UJUZI YA KISEKTA

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amesema serikali kupitia Wizara ya Elimu inaendelea kuimarisha stadi na ujuzi katika sekta sita za kipaumbele ili kufikia azma ya kuwa na uchumi wa kati unaotegemea viwanda ifikapo 2025.

Waziri Ndalichako ametoa kauli hiyo wakati wa halfa ya uzinduzi wa Mabaraza ya Ujuzi ya Kisekta jijini Dar es Salaam ambapo mabaraza hayo yaliyoundwa kupitia Mradi wa Kukuza Ujuzi na Stadi za Kazi (ESPJ) na sekta zilizopewa kipaumbele katika Mpango Mkakati wa Taifa wa Kukuza na Kuendeleza ujuzi ni pamoja na Kilimo, TEHAMA, Nishati, Ujenzi, Uchukuzi na Utalii.

“Katika azma ya Serikali ya kufikia uchumi wa kati unaotegemea viwanda ifikapo 2025, tunapaswa kuhakikisha nchi  yetu inakuwa na nguvukazi yenye ujuzi na stadi stahiki zinazohitajika kwenye soko la ajira,” amesisitiza Waziri Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako, akitoa hotuba yake wakati wa uzinduzi wa Mabaraza ya Ujuzi ya Kisekta uliofanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam.
Akizungumzia Mabaraza ya Ujuzi ya Kisekta Prof. Ndalichako amesema Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia iliingia makubaliano rasmi ya ushirikiano (MoU) na Tanzania Private Sector Foundation (TPSF) ili kusimamia uanzishaji na kuratibu mabaraza hayo ambayo yatakuwa kiunganishi muhimu kwa kuwaleta pamoja wadau mbalimbali wa masuala ya kuendeleza na kutumia ujuzi nchini.

“Tutaendelea kutoa ushirikiano kwa sekta binafsi na wadau wengine kwa kuweka mifumo wezeshi na rafiki, programu mbalimbali za kuendeleza ujuzi, na kuimarisha miundombinu ili kuhakikisha nchi inajenga ujuzi na stadi stahiki kwa ustawi wa maendeleo ya nchi,” amesema Prof. Ndalichako.
Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), Salum Shamte, akitoa hotuba ya utangulizi kabla ya kumkaribisha Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako kufungua rasmi Mabaraza ya Ujuzi ya Kisekta.
Waziri Ndalichako amesema kupitia ushirikiano kati ya Sekta Binafsi na Umma serikali inatarajia kupata ushirikiano katika programu za mafunzo ya wahitimu tarajali mahali pa kazi (internships) na kutambua ujuzi uliopatikana nje ya mfumo rasmi wa elimu (recognition to prior learning - RPL) ili kupunguza na kuondoa changamoto mbalimbali zilizopo katika jamii.

Aidha, Prof. Ndalichako ametoa ombi kwa sekta binafsi kuendelea kupokea vijana wanaokwenda kufanya mafunzo kwa vitendo ili kuwajengea utayari wa kuingia kwenye soko la ajira.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako akisalimiana na wadau waliohudhuria katika uzinduzi rasmi wa Mabaraza ya Ujuzi ya Kisekta.
Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF), Salum Shamte alisema mabaraza yatakuwa ni fursa pekee ya kuunganisha Taasisi Binafsi, Serikali na Wadau mbalimbali wa maendeleo kutoka nje ya nchi katika kuleta ufanisi katika maendeleo.

Shamte amesema TPSF imekuwa ikitoa ushauri na mapendekezo mbalimbali kwa serikali kupitia Baraza la Taifa la Biashara (TNBC) katika ngazi ya wilaya, Mkoa , Wizara na hata Taifa ili yaweze kufanyiwa kazi.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako, akipongezwa na Mwenyekiti wa Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), Salum Shamte mara baada kuzinduzia Mabaraza ya Ujuzi ya Kisekta uliofanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam.
Mwakilishi wa Sekta ya Kilimo akitoa neno la shukrani.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akiwa katika picha ya pamoja na Wawakilishi wa Sekta ya Kilimo.

Wadau wa Sekta ya Nishati wakiwa katika picha ya pamoja na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako.
Wawakilishi kutoka Sekta ya Tehama wakiwa katika picha ya pamoja na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako.

Wawakilishi kutoka TEA na Bodi ya Mikopo wakiwa katika picha ya pamoja na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia akiwa katika picha ya pamoja na Wawakilishi wa wanafunzi wa Vyuo Vikuu.

Washirika wa Maendeleo wakiwa katika picha ya pamoja na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako akiwa katika picha ya pamoja na Wawakilishi wa Sekta ya Utalii.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako akiwa katika picha ya pamoja na Wawakilishi wa Sekta ya Usafirishaji.

Jumatatu, 17 Juni 2019

NAIBU KATIBU MKUU MDOE ASEMA MAADILI YA UTUMISHI WA UMMA NI MSINGI WA UFANISI KATIKA UTENDAJI KAZI

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa James Mdoe amesema maadili ya utumishi wa umma ni msingi na nguzo ya utendaji wa ufanisi katika utumishi wa umma.

Profesa Mdoe ameyasema hayo jijini Dodoma wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya maadili kwa watumishi wa kada saidizi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ambapo amesema lengo la kufanya mafunzo hayo ni kukumbushana kuhusu maadili katika utumishi wa umma, utoaji wa huduma bora kwa mteja na utunzaji wa siri na nyaraka za serikali.
Naibu Katibu Mkuu wa wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. James Mdoe akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya maadili kwa watumishi wa kada saidizi yaliyofanyika jijini Dodoma Juni 17, 2019. Amesisitiza kuwa na
maadili mahali pa kazi ili kuleta ufanisi wa kazi.
"Suala la maadili katika utumishi wa umma si suala la hiari kwa yeyote aliyeajiriwa na kwamba inapotokea mtumishi akatenda kinyume atachukuliwa hatua kulingana na sheria, kanuni na taratibu za kiutumishi zilizopo," alisisitiza Profesa Mdoe.

Naibu Katibu Mkuu Mdoe amesema utumishi unaozingatia maadili hujidhihirisha pale mtumishi anapotoa huduma kwa wananchi bila upendeleo, rushwa, ubaguzi, staha, uadilifu, uwazi na kufanya kazi kwa bidii.

Aliongeza kuwa suala la uadilifu linakwenda sambamba na utunzaji wa siri na nyaraka za serikali na zile za wateja wanaotumia huduma za wizara na linapaswa kuzingatiwa na kila mtumishi wa umma katika nafasi yake huku akisisitiza matumizi sahihi ya teknolojia katika utendaji.
Baadhi ya watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia wanaoshiriki mafunzo ya maadili wakifuatilia Hotuba ya ufunguzi ya Naibu Katibu Mkuu, Prof. James Mdoe.
"Watumishi tujihadhari na matumizi mabaya ya teknolojia sio kila kitu unachokiona ofisini unakipiga picha na kukisambaza, teknolojia itumike na maadili ikunufaishe na sio ikuangamize,"aliongeza Profesa Mdoe.

Prof. Mdoe amemtaka kila mtumishi kuona fahari ya kuhudumu katika utumishi wa umma na lengo kubwa katika utendaji liwe kutoa huduma inayokidhi mahitaji ya watumiaji wa huduma inayotolewa.

Awali akizungumza katika mafunzo hayo Mkurugenzi Msaidizi wa Rasilimaliwatu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Sebastian Inoshi alimweleza Naibu Katibu Mkuu kuwa utoaji wa mafunzo hayo ni muendelezo wa utekelezaji wa Mpango wa wizara kwa mwaka 2018/19 wa kutoa mafunzo ya muda mfupi kwa watumishi kwa ajili ya kuwajengea uwezo ili kuwasaidia kuongeza tija na ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya kiofisi.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. James Mdoe akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya watumishi walioshiriki mafunzo ya maadili yaliyofanyika jijini Dodoma Juni 17, 2019.

Ijumaa, 14 Juni 2019

WAZIRI NDALICHAKO ATAKA VIONGOZI WA ELIMU KUTAMBUA JUHUDI ZINAZOFANYWA NA WALIMU NA WANAFUNZI KATIKA MASOMO


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amezitaka shule na wanafunzi kuendeleza juhudi katika masoma ili kujenga Taifa la watu waliosheheni ujuzi na maarifa ambao unahitajika kwa ajili ya maendeleo endelevu nchini.

Waziri Ndalichako ametoa wito huo jijini Dodoma wakati wa maadhimisho ya siku ya elimu ambayo yamekwenda sambamba na hafla ya utoaji tuzo kwa shule na wanafunzi wa darasa la saba, kidato cha nne na cha sita waliofanya vizuri zaidi katika mitihani ya kitaifa ya mwaka 2018.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akisisitiza jambo wakati wa maadhimisho ya siku ya elimu yaliyofanyika Jijini Dodoma. Maadhimisho hayo yamekwenda sambamba na hafla ya utoaji tuzo kwa Shule na wanafunzi wa shule za Msingi na Sekondari waliofanya vizuri katika mitihani ya kitaifa kwa mwaka 2018. 
Kiongozi huyo amewataka wanafunzi waliopata tuzo hizo kuendeleza juhudi katika masomo yao wanayoendelea nayo huku akiwataka viongozi wa elimu katika ngazi zote kujenga utamaduni wa kuwapongeza walimu na wanafunzi wanaofanya vizuri katika masomo kwani inatoa chachu ya kuendele kufanya vizuri zaidi.

“Haya matokeo ya wanafunzi sio matokeo ya kupika yanatokana na juhudi zao wenyewe, walimu na wazazi wao katika kusimamia ikiwa ni pamoja na juhudi za Serikali katika kuhakikisha wanakuwa na mazingira mazuri ya kufundishia na kujifunzia,” alisema Waziri Ndalichako

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akitoa zawadi kwa baadhi ya shule zilizofanya vizuri katika mitihani ya kitaifa kwa mwaka 2018.
Aidha Waziri Ndalichako amesema Wizara yake inatambua umuhimu wa kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia ili kupata matokeo mazuri ambapo katika mwaka wa fedha 2018/19 Serikali imejenga madarasa 1208, mabweni 222 matundu ya vyoo 2,141 na nyumba za walimu takribani 198, huku ikiimarisha huduma za maji kwenye shule ambazo zilikuwa na changamoto ya upatikanaji wa maji na kupelekea wanafunzi kulazimika kutembea umbali mrefu kutafuta maji.

Pia Waziri Ndalichako amesema Wizara inatambua umuhimu wa kuwaandaa walimu katika mazingira yaliyo mazuri hivyo imeendelea kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia katika vyuo hivyo.

“Kama ambavyo mmeshuhudia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli alipokuwa katika ziara yake ya mikoa ya kusini mwa nchi yetu aliweza kufika katika vyuo vya ualimu Kitangali, Mpuguso ambapo hii ni sehemu ya miradi mikubwa ambyo inafanywa na Wizara na miradi aliyoizindua ni sehemu ya miradi mikubwa minne inayotekelezwa katika vyuo vya ualimu Shinyanga, Mpuguso, Kitangali pamoja na Ndala, tunafanya kweli hatubeep,” alisisitiza Waziri Ndalichako.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akitoa zawadi ya cheti na fedha kwa mmoja wa wanafunzi waliofanya vizuri katika mitihani ya Kitaifa kwa mwaka 2018. 
Awali akizungumza katika hafla hiyo Kamishna wa Elimu Dkt. Lyabwene Mtahabwa alisema utoaji wa tuzo kwa shule na Wanafunzi wanaofanya vizuri katika mitihani ya Taifa ni miongoni mwa shughuli zinazotekelezwa na Mradi wa Lipa Kulinga na Matokeo katika Elimu (EP4R) ambapo kwa mwaka 2019 zawadi zimetolewa kwa jumla ya shule 3,916 (Msingi 3,135 na Sekondari 781) zilizofanya vizuri na zilizoongeza ufaulu kwa asilimia 10 pamoja na wanafunzi 29 wa shule za Sekondari kidato cha nne na cha sita.

1.      KAMISHNA WA ELIMU LYABWENE MTAHABWA AKIZUNGUMZA WAKATI WA HAFLA YA UTOAJI TUZO KWA SHULE NA WANAFUNZI WALIOFANYA VIZURI KATIKA MITIHANI YA KITAIFA YA MWAKA 2018.