Jumatano, 16 Oktoba 2019

WAZIRI NDALICHAKO ATOA SIKU 15 KWA MSHAURI ELEKEZI BICO KUFANYA TATHMINI YA GHARAMA ZA UJENZI CHUO CHA UALIMU KABANGA


Wakati Mradi wa ujenzi wa Chuo cha Ualimu Kabanga kilichopo Wilayani Kasulu  mkoani Kigoma ukiendelea kwa kusuasua Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako ametoa siku 15 kwa Mshauri Elekezi BICO  kupitia upya gharama za ujenzi wa mradi huo ambazo ni  zaidi ya shilingi bilioni kumi  ili kujiridhisha kama fedha hiyo inaendana na ukubwa wa mradi.

Prof. Ndalichako ametoa agizo hilo mara baada ya kufanya ziara ya kukagua mradi huo ambapo pamoja na kutoridhishwa na kasi ya Mkandarasi ametilia shaka gharama ya  ujenzi ambayo ni zaidi ya shilingi bilioni kumi kutumika ndivyo sivyo kutokana na aina ya majengo yanayojengwa katika chuo hicho kuwa ya thamani ndogo.

"Hivi ni vighorofa mtoto na narudia ni vighorofa mtoto huwezi kuniambia kwamba majengo haya ambayo kwanza ni machache, pili siyo ghorofa zile kubwa kama tulizojenga katika miradi mingine tena kwa gharama ndogo ya shilingi bilioni sita zinazidiwa na vighorofa hivi hapa kuna kitu hakipo sawa nataka ndani ya siku kumi na tano gharama za mradi zipitiwe upya kwa kila jengo na nipewe taarifa vinginevyo mratibu wa miradi hii utafute kazi nyingine," alisema Prof. Ndalichako.
Injinia wa mradi wa ujenzi wa Chuo cha Ualimu Kabanga akimuonesha Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako namna chuo cha Ualimu Kabanga kitakavyoonekana baada ya ujenzi kukamilika

Kuhusu kusuasua kwa Mradi Waziri Ndalichako amemtaka Mkandarasi huyo ambaye ni Kampuni ya SUMA JKT kuongeza kasi ya kufanya kazi akisisitiza ziletwe mashine za kisasa ambazo zitarahisisha kazi pamoja na kuongeza vibarua kwenye eneo la kazi.

"Huwezi kutekeleza mradi wa zaidi ya shilingi bilioni kumi kama nyumba yako unayojenga, yaani una kamashine kamoja tena kakusukuma,vibarua wenyewe inaonekana umewaleta leo baada ya kusikia nakuja kukagua, hii haikubaliki tunataka kazi ifanyike usiku na mchana kwa sababu pesa zipo lazima mradi ukamilike haraka," alisema Waziri  Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako akikagua mradi wa ujenzi wa Chuo cha Ualimu, Kabanga unaojengwa na Wizara kupitia Mradi wa TESP wilayani Kasulu mkoani Kigoma

Mapema akitoa  taarifa  ya mradi huo, Kaimu Mkuu wa Kanda ya Ujenzi SUMA JKT, Luteni Kanali Onesmo Njau amesema mpaka sasa ujenzi umekamilika kwa asilimia thelathini na kudai kukabiliwa na changamoto kadhaa ikiwemo  usumbufu wa kupata vifaa vya ujenzi kama saruji na mchanga.

"Mheshimiwa Waziri tulikuwa tukitegemea kupata saruji kwa kampuni ya Dangote lakini kwa sasa inabidi tufuate wenyewe Dodoma na hivyo kutumia muda mwingi kusubiri vifaa vifike kwenye eneo la mradi," alisema Kanali Njau.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako akikagua ujenzi wa Chuo cha Ualimu Kabanga Kasulu Mkoani Kigoma

Naye mshauri elekezi wa mradi huo kutoka BICO, Fred Munishi amekiri kuwa kazi inasuasua na kusema kuwa tayari ametoa maelekezo kwa Mkandarasi kuongeza kasi ya ujenzi taarifa ambayo hata hivyo imeonekana kukinzana na taarifa ya Mkandarasi na hivyo kutakiwa kufanya kazi kwa karibu na Mkandarasi.

"Inaonekana hapa hakuna maelewano mazuri baina ya Mkandarasi na mshauri elekezi, sitaki mivutano kazini kaeni pamoja fanyeni kazi ya serikali na mkiendelea hivi tutawaondoa," alisema Waziri Ndalichako.

Akiwa katika Halmashauri ya wilaya ya Kasulu, Waziri Ndalichako pia amekagua miradi mingine minne ya elimu katika shule za sekondari na msingi za Kigodya, Ruhita, Nyantare  na Kasyenene na kueleza kuridhishwa na kazi huku akisisitiza kuwa serikali inatoa fedha ili kuona matokeo.

Katika ziara hiyo Waziri Ndalichako aliambatana pia na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Dkt. AveMaria Semakafu pamoja na Mratibu wa Mradi wa Lipa Kulingana na Matokeo pamoja na ule wa TESP.
Muonekano wa sasa wa hatua ya ujenzi wa baadhi ya majengo katika eneo la mradi wa Chuo cha Ualimu Kabanga wilani Kasulu Mkoani Kigoma

UKARABATI CHUO CHA MZUMBE NA MIAKA 20 BILA MWALIMU NYERERE

USIMAMIZI MBOVU WA MIRADI YA ELIMU BUHIGWE WAMKERA WAZIRI NDALICHAKO


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako ameonesha kukerwa na usimamizi mbovu wa miradi ya Elimu katika Halmashauri ya Wilaya Buhigwe mkoani Kigoma na kumuagiza Katibu Mkuu wa Wizara anayoisimamia, Dkt. Leonard Akwilapo kuleta wataalamu watakaofanya ukaguzi maalum wa utekelezaji wa miradi ya elimu katika wilaya hiyo.

Waziri Ndalichako ametoa kauli hiyo  Wilayani Buhigwe mkoani Kigoma mara baada ya kukagua baadhi ya  miradi ya Elimu inayotekelezwa na Wizara kupitia Mpango wa Lipa Kulingana na Matokeo (EP4R)na kubaini uwepo wa kasoro kadhaa ikiwemo matumizi ya vifaa vya ujenzi vilivyo chini ya Kiwango na  majengo ya shule ya Msingi ya mfano Bwega  kutofautiana na ramani iliyopendekezwa na wizara.

"Kwa ujumla usimamizi wa Miradi katika wilaya ya Buhigwe  siyo mzuri, maafisa elimu hawawajibiki katika kuangalia kazi zao, unakuta kazi zimefanyika hovyo, watu hawafuatilii," alisema Waziri Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia akikagua moja ya nyumba za walimu katika Shule ya Msingi Kasumo iliyoko wilayani Buhigwe mkoani Kigoma

Waziri Ndalichako amesema Mhandisi wa Halmashauri ya Wilaya ya Buhigwe hatimizi wajibu wake ipasavyo kwa kuwa ameshindwa kusimamia miradi hiyo kwa viwango vinavyotakiwa na kuruhusu matumizi ya vifaa vya ujenzi visivyo na ubora lakini pia ameshindwa kufuata ramani  katika ujenzi wa majengo ya shule ya msingi ya mfano inayojengwa wilayani humo.

Kiongozi huyo amesema tayari  amewasiliana na Katibu Mkuu wa Wizara, Dkt. Leonard Akwilapo ili ufanyike ukaguzi wa kina katika miradi ya elimu  Wilaya ya Buhigwe lengo likiwa ni kubaini mapungufu na iwapo kuna mtu kafanya uzembe kwa manufaa yake awajibike.

"Inabidi kabla ya kuleta fedha nyingine za miradi ya elimu wilayani Buhigwe ije timu ya watalaamu mainjinia wachunguze walinganishe BoQ na kilichofanyika, haiwezekani turuhusu uzembe kama huu kuendelea kwenye miradi inayotumia fedha ya wananchi wanyonge," aliongeza Waziri Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako akionesha dosari kwenye jengo la maabara la shule ya sekondari Janda wakati akikagua miradi ya elimu inayotekelezwa katika shule hiyo na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia Programu ya Lipa Kulingana na Matokeo (EP4R)

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Buhigwe, Kanali Michael Ngayanalina amemshukuru Waziri Ndalichako kwa ziara yake wilayani humo na kusema kuwa  mapungufu yote yaliyobainika tayari  Kamati yake imeyatolea maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo na kwamba zoezi linaloendelea ni kuwachukulia hatua wahusika.

"Kamati ya Usalama ya wilaya ilibaini mapungufu katika miradi mbalimbali na tulitoa maelekezo kupitia kwa  Mkurugenzi na vyombo vyetu vilishaagizwa kufanya uchunguzi na kuchukua hatua stahiki," amesema Mkuu wa Wilaya hiyo, Ngayalina.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akikagua ujenzi wa maabara unaoendelea katika shule ya sekondari Janda iliyoko Buhigwe Mkoani Kigoma

Naye Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Anosta Nyamoga amesema ofisi yake tayari imemfukuza kazi fundi aliyekuwa na mkataba wa kufanya ukarabati na ujenzi wa vyumba vya madarasa katika Shule ya Sekondari Janda kutokana na kufanya kazi hiyo chini ya viwango na kuahidi kuzifanyia kazi kasoro zote ambazo zimebainishwa na Waziri Ndalichako.

Akiwa wilayani Buhigwe Waziri Ndalichako amekagua miradi ya elimu katika shule ya msingi Bwega, shule ya sekondari Janda,  shule ya sekondari Muyama na shule ya msingi Kasumo ambayo kwa pamoja inatarajia kugharimu zaidi ya shilingi bilioni moja.

Waziri Ndalichako yuko Mkoani Kigoma kwa ziara ya kikazi kukagua miradi ya Elimu katika Halmashauri ya Wilaya ya Buhigwe na Halmashauri ya Mji Kasulu.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akikagua moja ya dawati lililoko katika Shule ya Sekondari Muyama mara baada ya kukagua ujenzi wa darasa hilo

Ijumaa, 4 Oktoba 2019

WAZIRI NDALICHAKO AWAASA WANAFUNZI WANAOMALIZA KIDATO CHA NNE KUWA NA MAADILI


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako  amesema elimu bila nidhamu na maadili haiwezi kusaidia kufanikiwa katika maisha.

Waziri Ndalichako ameyasema hayo wakati wa mahafali ya 32 ya shule ya sekondari Suji iliyoko  wilayani Same mkoani Kilimanjaro.

Amesema katika maisha ili mtu afanikiwe ni lazima awe na nidhamu ya kufanya kazi aliyonayo kwa wakati ikiwa ni pamoja na kuheshimu mamlaka na hata watu walio chini yako na kuwataka wanafunzi  kuyaishi hayo mara baada ya kumaliza elimu ya kidato cha nne
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako akimtunuku cheti cha kuhitimu kidato cha Nne Mwanafunzi Tajiel Omary wa Shule ya Sekondari Suji iliyoko wilayani Same Mkoani Kilomanjaro

Kiongozi huyo ameupongeza uongozi wa shule ya sekondari Suji kwa kuwalea wanafunzi katika maadili mema ya kumjua Mungu na kuwapongeza kwa  kuendelea kufanya vizuri katika mitihani ya Taifa ya Kidato cha nne na cha sita.
Ndalichako amewataka wanafunzi kuongeza juhudi katika masomo yao ili wengi zaidi waweze kufaulu kwa kupata daraja la kwanza.

"Pamoja na ufaulu wenu mzuri lakini nataka  daraja la kwanza ziongezeke, kwa sababu ukiangalia matokeo ya shule hii kwa miaka mitatu  mfululizo kuanzia 2016 hadi 2018 hata kama hakuna daraja la nne lakini wanaopata daraja la kwanza ni wachache hivyo ongezeni juhudi ili ili huku kwenye daraja la kwanza muongezeke,"alisema Waziri Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako akizungumza wakati wa mahafali ya 32 ya Shule ya Sekondari Suji iliyoko Wilayani Same mkoani kilimanjaro

Amewataka wanafunzi kuwa na uzalendo na nchi yao ikiwa ni pamoja na kuzilinda tunu Taifa zilizoachwa na waasisi waxtaifa letu  ambazo ni pamoja na amani, umoja na  mshikamano.

"Mnaona kazi kubwa ambayo Rais wetu wa Awamu ya Tano  anaifanya anahakikisha rasilimali za nchi haziibiwi zinawanufaisha watu wote hivyo mnapomaliza mkamuunge mkono kwa kufanya kazi kwa bidii ili dhamira yake ni kuona nchi yetu inapata maendeleo inafanikiwa ," alisema Waziri Ndalichako.

Waziri Ndalichako ametumia fursa hiyo kuwatakia heri na mafanikio wanafunzi wote wa kidato cha nne wanaotarajia kuanza mitihani yao Mwezi Novemba mwaka huu.
Baadhi ya wahitimu wa Kidato cha Nne katika Shule ya Sekondari Suji ya Wilayani Same Mkoani Kilimanjaro wakiingia kwenye mahafali yaliyofanyika katika viawanja vya shule hiyo

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Same Rozimary Staki amesema Wilaya ya same ina shule za sekondari 53 ambapo 17 zinamilikiwa na watu binafsi pamoja na taasisi za dini.

Staki amesema kama Wilaya wamekuwa wakishirikia na na Viongozi wa Dini katika kuelimisha mabinti umuhimu wa kujitambua wanapokuwa shuleni.

Nae Mkuu wa Shule ya Sekondari Suji Silnani Dismas amesema shule hiyo pamoja  na kusisitiza masoma inawalea  wanafunzi katika maadili na nidhamu ya hali ya juu  kwa kuwa ni ya kanisa.

Dismas amesema shule hiyo ina wanafunzi takribani 568 na mafanikio wanayojivunia ni kuendelea kufanya vizuri katika mitihani ya Taifa.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako akisalimiana na Walimu wa shule ya Sekondari Suji mara baada ya kuwasili katika shule hiyo kwa ajili ya mahahafali ya 32 ya shule hiyo.

Mwanafunzi bora katika masomo Tajiel Omary ambae anatarajia kuhitimu masomo ya kidato cha nne mwaka huu amasema ufauli katika masomo unatokana na juhudi ambazo amekuwa akizifanya katika masomo ikiwa ni pamoja na kumuomba Mungu ili malengo yake yatimie. 

Waziri Ndalichako pia alitembelea shule ya sekondari Makanya na kuongea na wanafunzi ambapo amewatakia pia heri katika mitihani yao ya kumaliza kidato cha nne Mwezi Novemba mwaka huu.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akifurahi pamoja na Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Makanya iliyopo Wilayani Same Mkoani Kilimanjaro

Jumatano, 2 Oktoba 2019

WAZIRI NDALICHAKO AZINDUA KIWANDA CHA KUTENGENEZA SAMANI –VETA DODOMA


       •   Ataka VETA kutumia mafundi wao kujenga Vyuo vya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi 
           vya Wilaya

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako ameitaka Mamlaka ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kuhakikisha wanatumia mafundi wao kujenga Vyuo 25 vya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi vya Wilaya nchi nzima.

Waziri Ndalichako ametoa agizo hilo Jijini Dodoma wakati wa ufunguzi wa kiwanda cha kutengeneza samani cha Ufundi Stadi na Huduma Dodoma ambapo amesema haiwezekani VETA wakawa wanafundisha kujenga lakini wao wakiwa na kazi za ujenzi wanatafuta mafundi kutoka nje.

“Kama VETA mnafundisha kujenga lazima tuone mnafanya kazi kwa vitendo sio mnataka kupaka rangi mnatafuta mafundi wa mtaani nimesema marufuku nataka kuona hizi VETA 25 zinajengwa na ninyi kwa kutumia mafundi wenu vinginevyo nifute mafunzo ya ufundi, “alisema Waziri Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akifungua jiwe la msingi la Kiwanda cha VETA Dodoma. Pembeni ni Mbunge wa Dodoma Mjini na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira,  Vijana na Walemavu Mhe. Anthony Mavunde.
Amesema Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt John pombe Magufuli imeendelea kuviimarisha vyuo vya mafunzo ya ufundi stadi ili kuhakikisha  vinatoa mafunzo bora na mafunzo ya kisasa ambayo yanaendana na teknolojia ya kisasa na ndio maana inatumia fedha nyingi tena za walipa kodi kuhakikisha inajenga kiwanda cha samani na kutoa wito kwa vijana kujiunga na mafunzo ya useremala katika chuo hicho.

“Nimeambiwa hapa na Mwenyekiti wa Bodi kwamba takwimu za wanafunzi wanaosoma mafunzo ya ufundi seremala bado ziko chini lakini nipende kuwaambia ufundi seremala ni mzuri, kila mtu anahitaji vifaa vya ndani hivyo ni kozi ambayo inalipa natoa wito kwenu vijana kujiunga  na mafunzo haya na niwakaribishe  katika Chuo chetu cha VETA Dodoma ambacho kitakuwa na mafunzo ya kisasa kabisa,”aliongeza Waziri Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Kiwanda cha Samani VETA Dodoma.
Waziri Ndalichako ameupongeza uongozi wa VETA kwa kuweza kubuni na kutekeleza mradi wa kiwanda cha kisasa na kuwataka pamoja na kutoa mafunzo kuhakikisha wanakuwa na mpango mzuri wa uzalishaji mali utakaotumia mashine za kisasa zilizofungwa katika kiwanda hicho.

“Baada ya kuzindua kiwanda hiki nimekitembelea na kujionea namna kinavyoweza kufanya kazi kwa ufanisi, kutengeneza bidhaa kwa muda mfupi ni ukweli usiopingika kwamba  kimejengwa vizuri, naamini kitazalisha samani za hali ya juu na kwa bei nafuu na kuondoa dhana kuwa samani nzuri mpaka zitoke nje ya nchi,’aliongeza Waziri Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalicho akijaribu moja ya mashine katika kiwanda kipya cha samani cha VETA Dodoma.
Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Juma Nkamia amesema katika nchi nyingi duniani vyuo vingi vinavyozalisha nguvu kazi ni vyuo vya VETA na kuwataka vijana wanaosoma katika chuo hicho na wale walio nje ya chuo hicho kutoa hamasa kwa watanzania kusoma kwenye vyuo vya VETA ili kupata ujuzi utakaowawezesha kujiajiri.

Nae Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi VETA Peter Maduki amesema kiwanda hicho kitaendelea kuzalisha samani kwa ubora na kulingana na soko na kwamba uwepo wa Kiwanda hicho utasaidia kuongeza mapato yatakayotokana na uzalishaji wa samani zenye ubora na gharama nafuu.

Maduki alimweleza Waziri kuwa katika kufanikisha hilo watahakikisha wanaweka Menejimenti itakayoweza kuendesha kiwanda hicho na kuona malengo yaliyowekwa yanafikiwa huku akimweleza Waziri kuwa changamoto kubwa wanayoipata katika vyuo vya Veta ni kushindwa kupata na wanafunzi wa kutosha wa fani ya useremala.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalicho akitoa maelekezo wakati alipotembelea kiwanda cha samani cha VETA mara baada ya kukizindua rasmi.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA)..Pancras Bujulu alimweleza Waziri Ndalichako kuwa ujenzi wa kiwanda cha utengenezaji samani Dodoma umetekelezwa kwa awamu mbili moja ikiwa ya ujenzi wa jengo na miundombinu yake na awamu ya pili ikiwa ununuzi na ufungaji wa mashine na mitambo kazi zote zikigharimu  zaidi ya shilingi bilioni 3 ambazo ni fedha za ndani.

Hafla ya ufunguzi wa Kiwanda cha kutengeneza samani VETA Dodoma imekwenda sambamba na mahafali ya 36 ya Chuo cha Ufundi Stadi na Huduma Dodoma.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalicho akielekea kwenye tukio la uzinduzi wa kiwanda cha Samani VETA Dodoma.