Ijumaa, 14 Februari 2020

UKWELI KUHUSU VYUO VYA MAENDELEO YA WANANCHI (FDCs)

WAZIRI NDALICHAKO ATAKA USIMAMIZI THABITI WA MIRADI YA ELIMU

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako ametoa rai kwa watendaji wa Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kusimamia vizuri fedha za  miradi ya Elimu inayotelekezwa katika maeneo yao ili  ikamilike kwa wakati na ubora.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza wakati wa uzinduzi wa Jengo la  Utawala la Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam, Jijini Dar es Salaam
Waziri Ndalichako ametoa rai hiyo Jijini Dar es Salaam wakati akizinduzia Jengo la Utawala la Chuo Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam (DUCE) lililokarabatiwa na kuongeza ukubwa ambapo amesema Serikali imekuwa ikitoa fedha nyingi za Miradi lakini haikamiliki kutokana na usimamizi mbovu hivyo kutaka watendaji hao kusimamia miradi ipasavyo.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizindua Jengo la Utawala la Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam, Jijini Dar es Salaam
Amesema Serikali ya Awamu ya Tano imefanya kazi kubwa sana katika kuboresha mazingira ya utoaji elimu  na kwamba kukamilika kwa mradi wa upanuzi wa Jengo la Utawala la Chuo Kishiriki cha DUCE ni sehemu tu ya mambo mengi ambayo Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli na serikali yake imefanya.
Baadhi ya Wanajumuiya ya Chuo Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako wakati wa uzinduzi wa Jengo la Utawala la Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam, Jijini Dar es Salaam
Profesa Ndalichako aliongeza kuwa wakati Serikali ikiendelea na maboresho hayo, taasisi za elimu ya juu zinatakiwa kuendelea  kutekeleza wajibu wao ipasavyo ambao  ni kutoa taaluma, kufanya tafiti pamoja na kutoa huduma na ushauri kwa jamii.

“Vyuo Vikuu vimekuwa vikijikita katika utoaji wa taaluma wakati mwingine vinakuwa vikisahau jukumu la kufanya tafiti na ndio maana tunaona idadi ya machapisho imekuwa ikipungua mwaka hadi mwaka. Niwaambie tunapokuwa tunafanyiwa tathmini ya upangaji wa madaraja ya vyuo, sehemu ambayo mara nyingi imekuwa ikituangusha ni sehemu ya tafiti, kwa hiyo nitumie nafasi hii kuzikumbusha Taasisi za elimu ya juu kuendelea kufanya tafiti na tafiti zenyewe ziwe ni zile zinazotoa mchango moja kwa moja katika maendeleo ya nchi,” amesema Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wanajumuiya wa Chuo Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam mara baada ya  kuzindua Jengo la utawala la chuo hicho,  jijini Dar es Salaam
Katika hatua nyingine Profesa Ndalichako ametoa wito kwa Vyuo vya Elimu ya Juu nchini kutumia vema mapato yao ya ndani yanayotokana na huduma wanazotoa  kama za ushauri na tafiti kwa maendeleo ya Vyuo ikiwa ni pamoja na  kutenga sehemu ya Mapato hayo ndani kugharamia masomo ya watumishi.

“Nakipongeza Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa kuweza kutumia fedha kutoka kwenye mapato  ya ndani kutoa ufadhili wa masomo kwa watanzania wenye ufaulu wa kiwango cha Juu. Huu ni mchango mkubwa kwa Taifa letu kwani unatoa fursa kwa watanzania ambao wamefaulu vizuri lakini kutokana na sababu mbalimbali wasingeweza kunufaika na mikopo itolewayo na Bodi ya Mikopo,” alisema Waziri Ndalichako.
 
Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Chuo Kishiriki cha Dar es Salaam ambae pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Usimamizi ya DUCE Profesa William Anangisye amemuahidi Waziri Ndalichako kuendelea kusimamia vizuri matumizi ya fedha za Miradi ikiwa ni pamoja na kuhakikisha jengo lililozinduliwa leo linatumika kwa malengo yaliyokusudiwa na kuwa chachu ya maendeleo ya Chuo hicho.

“Mhe. Waziri nakuahidi kuwa majengo haya yatatunzwa vizuri na kutoa mchango mkubwa katika utekelezaji wa majukumu ya chuo,” amesema Prof. Anangisye.

Naye Kaimu Rasi wa Chuo Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam (DUCE), Prof. Stephen Maluka ameishukuru Serikali kwa namna inavyoendelea kuboresha mazingira ya utoaji elimu kwa Taasisi za elimu ya Juu ambapo amesema katika Chuo hicho upanuzi wa Jengo la utawala umeondoa changamoto iliyokuwepo ya ukosefu wa ofisi za watumishi huku akiiomba Serikali kuwapatia fedha kwa ajili ya kusomesha wataalamu wao.

Jumatano, 12 Februari 2020

UFUNGUZI WA MAFUNZO YA MAAFISA BAJETI WA WIZARA NA WA OFISI ZA UTHIBITI UBORA WA SHULE KANDA

Serikali imeweka kipaumbele katika kuwajengea uwezo watendaji wake ili kutimiza majukumu yao kwa ufanisi ikiwa ni pamoja na kuongeza nidhamu katika matumizi ya fedha na usimamizi fanisi wa mali za serikali.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya Maafisa Bajeti wa Wizara nawa Ofisi za Uthibiti Ubora wa Shule Kanda mkoani Morogoro
Hayo yamesemwa Mkoani Morogoro na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha wakati wa Ufunguzi wa Mafunzo ya Maafisa Bajeti wa Wizara na wa Ofisi za Uthibiti Ubora wa Shule Kanda yenye lengo la kuboresha utendaji kazi hususani katika maandalizi ya Bajeti.

Kiongozi huyo amesema utoaji wa mafunzo haya utasaidia kutoa maarifa mapya na stadi zaidi katika utekelezaji wa majukumu ikiwa ni Pamoja na  kuongeza uwazi na uwajibikaji katika utendaji kazi.

Mkurugenzi wa Idara ya Uthibiti Ubora wa Shule kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Mwl Euphrasia Buchuma akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya Maafisa Bajetu wa Wizara na wa Ofisi za Uthibiti Ubora wa Shule Kanda Mkoani Morogoro

“Mkurugenzi wa Uthibiti Ubora wa shule amenieleza kuwa kulikuwa na changamoto katika uaandaji wa bajeti kwa kuwa haikuwa na uhalisia, natambua mwenye kujua hali halisi kwenye ofisi ya uthibiti ubora ni yule ambaye yuko katika ofisi husika za kanda na wilaya na kwa kuwa  wataalamu wa bajeti wameona kuna mapungufu ndiyo maana tumeitisha mafunzo haya ili katika kupanga bajeti iwe na uhalisia,”alisema Naibu Waziri Ole Nasha
Mwezeshaji kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Pendo Sianga akiwapitisha wajumbe kwenye utaratibu wa kuandaa bajeti wakati wa mafunzo ya bajeti mkoani Morogoro

Katika hatua nyingine Naibu Waziri Ole Nasha amesema Serikali katika kipindi cha miaka minne ya Uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano imeweka mkazo katika kuimarisha Uthibiti Ubora wa Shule kwa kuwajengea uwezo wa kiutendaji Wathibiti Ubora na kuweka mazingira sahihi ya ufanyaji kazi.

Ametaja maboresho yaliyofanyika katika eneo hilo kuwa ni pamoja na  ununuzi wa magari 45 ya wathibiti ubora wa Shule kwa wilaya ambazo hazikuwa na magari Pamoja na Kujenga Ofisi 100 za Wathibiti na kuziwekea samani na vitendea kazi. Aidha Serikali pia imenunua pikipiki 2,894 za Maafisa elimu Kata ili kuimarisha usimamizi wa  shule, pamoja na kuwapatia mafunzo ya kiutendaji wathibiti Ubora wa shule 1,276.
Baadhi ya Washiriki wa mafunzo ya Bajeti Mkoani Morogoro wakifuatilia hotuba ya Ufunguzi ya Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha
Maboresho mengine ni Kuongeza idadi ya Maafisa Uthibiti Ubora wa shule 400 ngazi ya Wilaya na Kanda pamoja na kuanzisha ofisi mpya 5 za Uthibiti Ubora wa shule katika wilaya mpya za Songwe, Kigamboni, Ubungo, Chalinze na Ushetu ili kurahisisha utoaji huduma za uthibiti Ubora huku serikali ikijipanga kununua magari mengine mapya 65 kwa ajili ya idara hiyo.

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Uthibiti Ubora wa Shule Mwl. Euphrasia Buchuma amesema mafunzo haya yanafanyika kutokana na changamoto ambazo zimekuwa zikibainika katika bajeti zinazoandaliwa ikiwa ni pamoja na kueleweshana taratibu za matumizi ya fedha kulingana na vifungu vilivyowekwa.
 
Mafunzo ya kuwajengea uwezo maafisa bajeti wa Wizara na wa Ofisi za Uthibiti Ubora wa shule za Kanda yameanza leo Februari 12, 2020 na yana jumla ya washiriki 70 kutoka Ofisi hizo na Wizara ya Elimu Makao makuu.

KONGAMANO LA KIMATAIFA LA KUUNGANISHA WANATAALUMA NA WADAU WA SEKTA YA U...