Jumatatu, 20 Januari 2020

MKUTANO WA KIMATAIFA WA ELIMU JIJINI LONDON UINGEREZA

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako na baadhi ya wataalamu wa elimu kutoka Tanzania  wakiwemo kutoka  Washirika wa Maendeleo kutoka "DFID" Tanzania na British Council Tanzania wanashiriki Mkutano wa Kimataifa wa Elimu jijini London, Uingereza ambapo ajenda kuu ya mkutano huo ni nini kifanyike kuboresha Elimu ndani ya kizazi kimoja "One Generation."


Mkutano huo unawaleta pamoja Mawaziri wenye dhamana ya Elimu na wataalamu katika Sekta ya Elimu kutoka nchi 120 ambapo pia watajadili kuhusu mfumo sahihi wa upimaji uelewa wa wanafunzi na iwapo matokeo ya mwanafunzi yanatokana na mwanafunzi mwenyewe, Mfumo, Walimu au Mitaala.


Mengine yatakayojadiliwa katika Mkutano huo ni pamoja na uboreshaji Mazingira  ya utoaji elimu kwa ajili ujifunzaji, uboreshaji Elimu jumuishi, uimarishaji Elimu ya Ufundi katika kuongeza Vijana wenye ujuzi, umuhimu wa vipaumbele vya elimu katika ngazi zote za elimu  kuwiana, maendeleo ya Teknolojia  yanavyochagiza na kutumika katika ujifunzaji na ufundishaji, umuhimu wa  kuwa na takwimu sahihi za Kitaifa za Sekta na pia umuhimu wa uwekezaji katika elimu ya awali katika ujifunzaji.

Jumapili, 19 Januari 2020

NDALICHAKO AKABIDHIWA MAGHOROFA YA NSSF KWA AJILI YA HOSTELI

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako Jumamosi Januari 18, 2020  amekabidhiwa rasmi maghorofa 32 ya NSSF yatakayotumika kwa ajili ya kutoa huduma ya Hosteli kwa Wanafunzi wa Elimu ya Juu nchini.

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Ajira, Vijana, Kazi na Watu wenye Ulemavu Mheshimiwa Jenista Mhagama amesema mpango huo wa NSSF umetokana na maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt John Pombe Magufuli ambapo Wizara yake ilisimamia utekelezaji wake huku akieleza kuwa awamu ya pili NSSF watakamilisha majengo ambayo yatawezesha wanafunzi wengine zaidi ya 4000 kuishi.

Nae Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa  Joyce Ndalichako amemshukuru na kuwapongeza  Rais kwa uamuzi huo na kuongeza kuwa hiyo ni moja tu ya hatua kubwa anazoendelea kuchukua katika kuboresha Sekta ya Elimu.
Profesa Ndalichako amesema hatua hiyo itapunguza changamoto ya uhaba wa Hosteli za wanafunzi wa Elimu ya juu hapa Dar es Salaam na ameishukuru na kupongeza Bodi na Uongozi wa NSSF kwa utekelezaji wa haraka wa agizo hilo na kukamilisha mahitaji muhimu ya miundo mbinu katika Majengo hayo kwa wakati.

Majengo hayo yako eneo la Mtoni Kijichi, Wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam na yatahudumia wanachuo  4,317 kutoka Chuo cha Kumbukumbu  ya Mwalimu Nyerere, Chuo cha Usimamizi wa fedha IFM, Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu (DUCE), Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA)Chuo cha Diplomasia  na Taasisi ya Teknolojia  Dar es Salaam.

Jumamosi, 18 Januari 2020

MAHAFALI YA 11 YA CHUO CHA UFUNDI ARUSHA

Naibu Waziri wa Elimu ,Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha amewataka vijana wanaohitimu katika vyuo vya ufundi kujikita katika kuanzisha ajira mpya kwa kujiajiri badala ya kusubiria nafasi chache za ajira zilizopo ikiwa ni pamoja na kutumia ujuzi wao na taalamu katika kuihudumia jamii na kupata manufaa ya kiuchumi.


Akizungumza katika Mahafali ya 11 ya Chuo​ cha Ufundi Arusha yaliyofanyika Jijini Arusha Naibu Waziri Ole Nasha amewataka wahitimu hao kuwa na uthubutu wa kuanzisha ajira zao wenyewe hata katika kiwango cha chini kwani zitaweza​ kukua na kuwafanikisha malengo yao.

Nasha amewataka wahitimu hao wasikae majumbani wakisubiri ajira bali waanzishe miradi midogo midogo itayowasaidia na kusaidia jamii zao hivyo kusukuma gurudumu la maendeleo.

“Hakika Mafanikio katika maisha yenu hayatategemea tu elimu ya ufundi bali yatatokana na nidhamu na uthubutu .Ninafahamu zipo changamoto katika kujiajiri lakini muhimu kuliko yote ni kuwa na nia na uthubutu .Eneo​ la ufundi lina fursa nyingi sana,” anaeleza Naibu Waziri wa Elimu.

Naye Balozi wa Norway nchini Tanzania, Elisabeth Jacobsen ​ amesema kuwa Norway itaendelea kushirikiana na Tanzania katika kuboresha elimu ya Ufundi ambayo ni kichocheo kikubwa cha maendeleo katika kufikia uchumi wa kati na Tanzania ya Viwanda kama iliyo azma ya serikali.

Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Chuo cha Ufundi Arusha (ATC), Dr. Masudi Senzia amesema kuwa chuo hicho kimeongeza udahili wa wanafunzi wa kike katika masomo ya kike kutokana na idadi ndogo ya​ vijana wa kike wanaojiunga na elimu ya Ufundi .

Masudi ameiomba serikali iwapatie fedha za kujenga shule za bweni kwa ajili ya wanafunzi wa kike ambao asilimia kubwa wanaishi nje ya chuo.

Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo cha Ufundi ​ Arusha (ATC, Chacha Makamba Wambura ​ amepongeza juhudi kubwa zinazofanywa na serikali ya awamu ya tano katika kuboresha elimu ya ufundi na kujenga miundombinu rafiki na vifaa vya kisasa vya kujifunzia suala linalopelekea kupata wahitimu waliobobea katika fani zao.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akipata maelezo kuhusu mitambo ya kisasa inayotumika kufundishia katika Chuo cha Ufundi Arusha kabla ya kuanza mahafali ya kumi na moja ya Chuo hicho.

Jumla ya wahitimu 436 wamemaliza katika Chuo cha Ufundi Arusha na kutunukiwa vyeti katika ngazi ya Astashahada, Stashahada, Shahada ya juu na Shahada.

UZINDUZI WA KITUO CHA MAFUNZO YA KUFUA UMEME

zaidi ya shilingi bilioni 8.5 zimetumika katika kukarabati na kujenga  majengo mpya katika kituo cha mafunzo ya kufua umeme wa nguvu ya maji cha Kikuletwa kinachomilikiwa na Chuo cha Ufundi Arusha


Akizungumza kabla ya kuzindua kituo hicho  Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha amesema kituo hicho ni sehemu ya mpango mkakati mkubwa wa Serikali wa kuleta mapinduzi katika utoaji wa Elimu ya Ufundi nchini na Afrika Mashariki kutokana na kutoa mafunzo kwa vitendo yatakayosaidia kupata mafundi mahiri waliobobea katika fani yaa kufua umeme.

“Elimu itakayopatikana hapa itawasaidia vijana kuitumia elimu hiyo kujiajira kwani kuna fursa nyingi kwenye kujiajiri kuliko kusubiri fursa chache zilizopo za kuajiriwa, nani uhakika vijana wanaotoka hapa watakuwa mahiri katika kufua umeme na wataweza kujiajiri na kuajiri wenzao” amesema Ole Nasha

Naibu Waziri huyo amesisitiza kuwa uanzishaji wa Kituo cha mafunzo cha kufua umeme kwa kutumia nguvu ya maji hapa Kikuletwa umelenga kuhakikisha kuwa watalaamu; hasa mafundi stadi (artisans) na mafundi sanifu (technicians) wanapatikana ili kuongeza ufuaji wa umeme kutoka nyanzo vidogo vidogo vya maji na vikubwa pamoja kufanya tafiti juu ya nishati jadidifu (Research in renewable energy) ikiwemo uzalishaji umeme kutokana na nguvu ya maji.


Ole Nasha amesema serikali inatambua umuhimu wa Elimu ya ufundi kuelekea Tanzania ya viwanda ambapo inaendelea kufanya uwekezaji mkuwa katika vyuo vya ufundi, uwekezaji ambao umeongeza udahili na ubora katika Elimu ya ufundi. Kutokana na uwekezaji unaoendelea idadi ya wanafunzi wanaojiunga na mafunzo ya ufundi imeongezeka kutoka 30,000 mwaka 2015 hadi 151,969 mwaka 2019 pia inaendelea na ujenzi wa vyuo vipya vya ufundi stadi 43 kwa gharama ya shilingi bilioni 92 katika maeneo mbalimbali nchini pamoja na ujenzi wa chuo kipya Jijini Dodoma chenye hadhi sawa na ATC au DIT kwa gharama ya shilingi bilioni 18.

Aidha, Naibu Waziri ameongeza kuwa serikali imeanza utekelezaji wa mradi mkubwa wa Elimu ya Ufundi Afrika Mashariki (EASTRIP) unaofadhiliwa na Benki ya Dunia kwa gharama ya dola za kimarekani milioni 75 unaolenga kuleta mapinduzi katika Elimu ya ufundi nchini kwa kuvijengea vyuo uwezo ili viweze kuzalisha wanafunzi wenye ujuzi stahiki wa kuwawezesha kujiajiri ama kuajiriwa utawezesha ujenzi wa miundombinu bora na kuweka vifaa pamoja na kuwajengea uwezo wakufunzi.

Kaimu Mkuu wa Chuo hicho Dkt.Masudi Senzia amesema kuwa tayari kituo hicho kimeanza kupokea wanafunzi ambao wanapata mafunzo katika fani mbalimbali za kufua umeme ambapo vijana wanaouzunguka eneo la Kikuletwa wamejitokeza kwa wingi​ kwa ajili ya kupata elimu itayowaezesha kujikwamua kimaisha.

Masudi amesema kuwa benki ya dunia ina mpango wa kutoa fedha kwa ajili ya kukiboresha kituo hicho cha mafunzo ili nchi za Afrika Mashariki ziweze kutumia chuo hicho kama kituo cha umahiri .

Kwa upande wake Balozi wa Norway nchini Tanzania Elizabeth Jacobsen amesema kuwa Norway itaendelea kuimarisha ushirikiano mwema uliopo baina ya nchi hizo ikiwa ni pamoja na kuijengea Tanzania uwezo katika masuala ya nishati jadidifu itakayosaidia kufikia uchumi wa kati na Tanzania ya Viwanda.

Balozi Elizabeth amesema kuwa kituo hicho kitasaidia katika mafunzo ya jinsi ya kuongeza uzalishaji wa umeme unaotokana na maji katika maeneo mbalimbali nchini huku ukilenga kujenga wataalamu waliobobea katika kufua umeme.

Mkuu wa Wilaya ya Hai,Lengai ​ Ole Sabaya amewataka wananchi kushirikiana na kituo hicho katika kulinda miundombinu iliyoko ili iweze kuwanufaisha vyema watu wa Hai,Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla.

Jumatano, 15 Januari 2020

MAKABIDHIANO YA MAGARI YA VYUO VYA UALIMU

 Serikali imetoa magari mapya 35 kwa Vyuo vya Ualimu vya Tanzania Bara yenye thamani ya bilioni 5.2 kwa ajili ya kurahisisha mchakato wa ufundishaji na ujifunzaji

#Profesa Joyce Ndalichako

# Halfa ya makabidhiano ya magari ya vyuo vya ualimu














Jumapili, 12 Januari 2020

HAFLA YA UWEKAJI JIWE LA MSINGI SKULI YA MWANAKWEREKWE ZANZIBAR

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli Januari 11, 2020 ameweka jiwe la Msingi katika Skuli Mwanakwerekwe, Zanzibar.
 
Hafla hiyo ya uwekaji wa jiwe la msingi imehudhuriwa na Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako pamoja na Viongozi mbalimbali wa Serikali.
Akihutubia wananchi waliohudhuria katika hafla hiyo Rais  John Pombe Magufuli ameipongeza Serikali ya Awamu ya Saba kwa miaka tisa kwa kuiletea Maendeleo Zanzibar ikiwemo Sekta ya Elimu, huku akiwataka Viongozi katika Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kusimamia katika kuongeza ufaulu wa Shule za visiwani katika mitihani ya kitaifa.
Amesema katika kipindi cha miaka tisa idadi ya wanafunzi imeongezeka katika skuli za Maandalizi kutoka 238 mwaka 2010  na kufikia wanafunzi 382 kwa mwaka 2018. Kwa upande wa Sekondari idadi imefikia wanafunzi 381 kutoka 299 mwaka 2010 na Vyuo Vikuu  kutoka 767 mwaka 2010 na kufikia Wanafunzi 3,624 mwaka 2018.
 
Skuli ya Mwanakwerekwe inajengwa kwa  gharama ya shilingi Bilioni 2.628 ambazo ni  mkopo wa Dola milioni 35 ambazo ni zaidi Bilioni 80 kutoka Benki ya Dunia na  zimejenga skuli mbalimbali ikiwemo Mwanakwerekwe.

Alhamisi, 9 Januari 2020

WAZIRI NDALICHAKO AFURAHISHWA NA MATOKEO KIDATO CHA NNE


Matokeo haya ni ya kwanza tangu kutekeleza Mpango wa Elimu bila Malipo, baadhi ya watanzania waliona ni jambo ambalo halitawezekana sasa tunashuhudia kiwango cha ufaulu kupanda kutoka 67.91% mwaka 2015 hadi kufikia 80.65% mwaka 2019.

Natoa pongezi za dhati kwa wanafunzi waliofanya vizuri katika mitihani yao na kwa walimu ambao wamekuwa nao bega kwa bega na kuwawezesha kupata matokeo mazuri

#Profesa Ndalichako
#TunaboreshaElimuYetu