Jumanne, 11 Februari 2020

WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA KUJENGA KUJENGA BWALO KATIKA SHULE YA MRISHO GAMBO ILIYOPO MKOANI ARUSHA



Akizungumza mara baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa shule hiyo, Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Leonard Akwilapo  amesema Wizara itajenga bwalo la chakula ili kuwezesha wanafunzi wa shule hiyo kuwa na sehemu nzuri na salama ya kupatia chakula watakapokuwa wakiishi katika mabweni yatakayojengwa na wizara.

"Nimeambiwa wanafunzi wa shule hii wanatoka maeneo ya mbali, Wizara ilishaahidi kujenga mabweni mawili sasa tutajenga na bwalo," amesema Dkt. Akwilapo.

 Aidha, Dkt. Akwilapo amesema  serikali ina wajibu wa kuhakikisha wanafunzi wanasoma  katika
 mazingira salama na yenye miundombinu salama.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo amesema shule hiyo imejengwa baada ya kupokea maombi kutoka kwa  wakazi wa Olasite baada shule yao kuzidiwa na wingi wa wanafunzi.

"Baada ya kupokea maombi kutoka kwa wakazi wa hapa  na kuona kweli kuna shida katika shule hii ya Olasite ndipo tukaanza kutafuta wadau mbalimbali ambao walijitokeza na kusaidia uanzishwaji wa ujenzi wa shule hiyo," amesema Gambo.

Mkuu wa shule hiyo, Fedelis Michael amesema mazingira ya wanafunzi kusoma mbali sana na shule ni changamoto kwao kwani njiani wanakutana na mambo mengi ambayo yanaweza kuwasababishia kushindwa kusoma vizuri.

Jumatatu, 10 Februari 2020

CANADA YATOA ZAIDI YA BILIONI 90 KWA AJILI YA KUBORESHA ELIMU YA UALIMU

Serikali ya Canada imetoa zaidi ya bilioni 90 kwa Tanzania zitakazotumika kuboresha elimu ya ualimu nchini.

Hayo yamesemwa Jijini Arusha na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo  wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kupitia na kutathmini utekelezaji wa Mradi wa Kuendeleza Elimu nchini (TESP) ambapo amesema mradi huo pia umewezesha kuinua kiwango cha ubora wa elimu katika shule za msingi na sekondari kwa kuzalisha rasilimali watu yenye ubora.
.
Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo akizungumza na wadau wa Elimu ya Ualimu (hawapo pichani) wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kupitia na kutathimini Mradi wa Kuendeleza Elimu ya Ualimu (TESP) Jijini Arusha
Dkt. Akwilapo amesema Canada kupitia TESP imetoa fedha hizo ambazo zimetumika katika kuvijenga upya baadhi ya vyuo vya ualimu, kuboresha miundombinu ya kufundishia na kujifunzia  pamoja na kutoa mafunzo kazini kwa  walimu.

Kansela Mkuu, Ushirikiano na Maendeleo kutoka Canada Gwen Walmsely akizungumza na wadau wa Elimu ya Ualimu jijini Arusha
Kiongozi huyo amesema kuwa Ushirikiano wa Tanzania na Canada unalenga kuongeza uwezo wa vyuo vya ualimu kufundisha walimu waliobobea watakaofundisha vizuri katika shule mbalimbali.

“Tunatoa shukrani nyingi sana kwa serikali ya Canada na Kitengo chao cha Global Affairs ambacho kinasimamia mradi huu, mafanikio makubwa yamepatikana kupitia mradi huu na matokeo yameshaanza kuonekana," amesisitiza Katibu Mkuu Akwilapo.

Dkt. Akwilapo amesema mafanikio  ya mradi huo yameanza kuonekana ambapo walimu wameongeza uwezo katika ufundishaji na matumizi ya TEHAMA katika kufundisha.

Kansela Mkuu, Ushirikiano na Maendeleo ​kutoka Canada Gwen Walmsley amesema kuwa Canada itaendelea kutoa fedha zaidi katika kuboresha sekta ya elimu nchini na mradi huo ni moja kati ya juhudi wanazozifanya katika kuunga mkono serikali ya Tanzania katika jitihada za  kuboresha elimu.

Gwen ameipongeza Tanzania kwa kufanya Sekta ya Elimu kipaumbele ili  kuhakikisha watoto wote wanapata elimu, suala ambalo limewezesha zaidi ya watoto milioni 10.6 kujiunga na elimu ya msingi na sekondari

Mratibu wa Mradi wa kuendeleza Elimu​ ya Ualimu TESP kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Ignas Chonya amesema kuwa mradi huo umewawezesha walimu kuboresha mbinu za ufundishaji kupitia Tehama ambapo vyuo 35 vya ualimu vimeanganishwa na mfumo huo na wanatarajia kuunganishwa na mkongo wa Taifa.

Jumamosi, 8 Februari 2020

MKUTANO WA WATUMISHI WA WIZARA WALIOKO MAKAO MAKUU


Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Leonard Akwilapo amesema utumishi wa umma una sheria, kanuni, taratibu, maadili na miiko ya kiutendaji ambayo kila mtumishi anapaswa kuielewa na kuzingatia katika utendaji kazi.
 
Katibu Mkuu Akwilapo amesema hayo wakati wa Mkutano  wa Wafanyakazi wa kutathmini utendaji wa Wizara katika kipindi cha miezi sita kuanzia Julai hadi Desemba 2019 ambapo amesema ni vizuri kila mtumishi akazingatia taratibu hizo ili kutekeleza majukumu yake ipasavyo.

Amesema pamoja na kuzingatia sheria hizo ni vizuri tukafanya kazi kwa kushirikiana na kuelekezana ili kupata matokeo chanya katika utekelezaji wa majukumu.

Kiongozi huyo amepongeza watumishi wa Wizara hiyo kwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo ili kufikia malengo makubwa ya Wizara ambayo ni kutoa Elimu bora nchini.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. AveMaria Semakafu amesema ni vizuri watumishi wakaendeleza kasi liyopo sasa ya utendaji huku wakizingatia utendaji wenye viwango ili sekta ya Elimu iendelee kufanya vizuri.

Akizungumza kwa niaba ya Watumishi wa Wizara Bwana Nicholaus Moshi ameupongeza Uongozi wa Wizara kwa namna unavyoweka mazingira wezeshi ya utoaji Elimu kwa  kujenga na kukarabati miundombinu ya elimu, kununua vifaa vya kufundishia na kujifunzia, kuhakikisha uwepo wa vitendea kazi pamoja na ujenzi wa ofisi zikiwemo za Wathibiti Ubora wa shule na ukarabati na upanuzi wa  Vyuo  ya Ualimu.

Alhamisi, 6 Februari 2020

SERIKALI KUJENGA SHULE ZA WANAFUNZI WENYE MAHITAJI MAALUM KILA MKOA

Serikali imesema itaendelea na mpango mkakati wa kutekeleza elimu bila malipo pamoja na kutoa vipaumbele kwa watu wenye ulemavu kupata elimu iliyo bora.

Hayo yameelezwa jijini Dar es Salaam na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Ave Maria Semakafu wakati wa ufungaji wa mafunzo ya TEHAMA na Teknolojia Saidizi kwa wakufunzi na walimu wa Sekondari wenye mahitaji maalum.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu akiongea wakati wa ufungaji wa mafunzo ya Tehama na Teknolojia Saidizi kwa Wakufunzi na Walimu wa Sekondari wenye mahitaji maalumu jijini Dar es Salaam.
Dk. Semakafu amesema  serikali imejipanga kuhakikisha walimu  na wanafunzi wanapata elimu ya Tehama, elimu jumuishi sambamba na kujenga shule zao maalum katika kila mkoa ambapo kwa sasa wameanza na mkoa wa Katavi.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu akitoa maelekezo kwa mmoja wa washiriki wa mafunzo ya Tehama na Teknolojia Saidizi OUT, jijini Dar es Salaam.
Hata hivyo awali ilielezwa kuwa tayari serikali imetumia kiasi cha shilingi bilioni 5.9 kwa ajili ya kununua na kusambaza vifaa maalum vya kielimu saidizi katika shule za msingi na sekondari zinazopokea wanafunzi wenye mahitaji maalum nchini.

“Hii kazi pia si ndogo, napenda kwa namna ya kipekee kabisa kutumia nafasi hii kuushukuru Uongozi wa Chuo Kikuu Huria kwa kukubali kuendesha mafunzo haya hapa chuoni na kutoa wawezeshaji, vifaa pamoja na miundombinu mingine kwa ajili ya kufanikisha mafunzo haya muhimu,’’ amesema Dk. Semakafu.
Mmoja wa washiriki wa mafunzo ya Tehama na Teknolojia Saidizi akiwa katika mafunzo yaliyofanyika Chuo Kikuu Huria jijini Dar es Salaam.  Kulia ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu.
Aliongeza kuwa mafunzo waliyoyapata ni muhimu kwani yatawasaidia katika matumizi ya TEHAMA kwenye  ufundishaji na ujifunzaji, kutafuta rejea mbalimbali za kielektroniki kwenye mitandao na kutumia teknolojia saidizi zinazowezesha matumizi ya TEHAMA katika ufundishaji na ujifunzaji.

Akizungumza kwa niaba ya washiriki wa mafunzo hayo, Mwalimu wa shule ya sekondari ya Binti Mussa iliyopo Kiwalani jijini Dar es Salaam, Anna Mbogo alisema wanaishukuru kwa  dhati  Wizara ya Elimu kwa kuona umuhimu wa kutoa  mafunzo kwa walimu wenye mahitaji maalum.
Baadhi ya washiriki wa mafunzo ya Tehama na Teknolojia Saidizi kwa Wakufunzi na Walimu wa sekondari wenye mahitaji maalumu wakifuatilia hotuba ya Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu (hayupo pichani)  wakati wa kufunga mafunzo hayo jijini Dar es Salaam.
“Mafunzo haya  yalilenga kutujengea uwezo sisi walimu kuendana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia ya sasa, pia tunaushukuru uongozi wa OUT chini ya serikali ya awamu ya tano kuonesha bayana nia ya kuwasaidia walimu wenye mahitaji maalum na kuwathamini watu wenye ulemavu kwa kuajiri watu wenye ulemavu,’’ amesema Mwalimu Anna.

MAKISATU 2020 KUENDELEA KUIBUA WABUNIFU

Serikali imesema inatambua umuhimu na mchango wa ubunifu na teknolojia katika kurahisisha na kuongeza ufanisi  katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kiuchumi.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma kuhusu kuanza kwa Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (MAKISATU) 2020, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha amesema  mashindano hayo ni moja ya mikakati ya Serikali ya kuibua, kutambua na kuendeleza ubunifu na ugunduzi unaofanywa na watanzania.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Mkutano mara baada ya kuzungumza na Waandishi wa habari jijini Dodoma.  Kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. Leonard Akwilapo na kulia ni Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano, Sylvia Lupembe.

"Lengo kubwa la MAKISATU pamoja na kukuza na kusaidia kubiasharisha, yanatoa fursa kwa wabunifu na wagunduzi wa teknolojia mbalimbali kujitangaza na kutangaza kwa wadau ubunifu unaozalishwa," amesisitiza Ole Nasha.
Mwakilishi wa Benki ya CRDB, Prosper Nambaya akizungumza wakati wa Mkutano wa Waandishi wa habari kuzungumzia kuanza kwa mashindano ya MAKISATU, 2020 jijini Dodoma.
Ole Nasha amesema MAKISATU inawalenga wabunifu kutoka makundi ya shule za msingi, sekondari, vyuo vya ufundi stadi, vyuo vya kati, vyuo vikuu, Taasisi za utafiti na Mfumo usio rasmi.

Baadhi ya washiriki waliohudhuria Mkutano wa kuzungumzia kuanza kwa Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknonojia na Ubunifu (MAKISATU) 2020 jijini Dodoma, wakimsikiza Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha (hayupo pichani) wakati akizungumza na Waandishi wa habari.

Aliongeza kuwa kupitia MAKISATU 2019 Serikali imewaibua na kuwatambua wabunifu wachanga zaidi ya 415 huku wabunifu 60 mahiri wakiendelezwa ili ubunifu wao ufikie hatua ya kubiasharishwa.


Kiongozi huyo ametoa wito kwa watanzania wenye ubunifu mbalimbali kushiriki katika mashindani hayo na amewashukuru Benki ya CRDB kwa kukubali kufadhili mashindano hayo.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Wateja Wakubwa kutoka CRDB, Prosper Nambaya amesema Benki hiyo imeamua kuwa na ushirikiano endelevu na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ili kusaidia kukuza ubunifu unaozalishwa nchini kutokana na kuwepo kwa watu wengi wenye mawazo ya kibunifu yanayopaswa kuendelezwa.

Jumatatu, 27 Januari 2020

WALIMU NA WAKUFUNZI 140 WENYE MAHITAJI MAALUM WANAPATA MAFUNZO YA TEHAMA

Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia katika kipindi cha miaka minne ya uongozi wa Awamu ya tano imetumiza Sh.bilioni 5.9 kununua na kusambaza vifaa maalum vya kielimu na saidizi katika shule za msingi na sekondari, zinazopokea  wanafunzi wenye mahitaji maalum nchini.

Hayo yamesemwa Jijiji Dar es Salaam na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo wakati wa ufunguzi wa  mafunzo ya ya siku 10 ya Tehama na Teknolojia saidizi kwa wakufunzi na walimu wenye mahitaji maalumu wanaofundisha shule za sekondari  ili kuwajengea uwezo wa matumizi ya Teknolojia hiyo katika utekelezaji wa majukumu yao.

Kiongozi huyo ametaja vifaa vilivyonunuliwa na kusambazwa kuwa ni Shime sikio (Hearing Aids) kwa ajili ya wanafunzi wenye baki ya usikivu, mashine za kuandikia maandishi ya breli na Vivunge vyenye fimbo nyeupe (Braille kit)kwa ajili ya wasioona.

Alisema  kuwa katika kipindi cha miaka minne ya Rais John Magufuli,  pia Serikali imefanya upanuzi na ukarabati wa Chuo cha Ualimu Patandi ili kuongeza udahili wa walimu kutoka walimu 300 na kufikia walimu 450 kwa mwaka wa masomo 2019/2020.

Pia imejenga  shule ya sekondari ya mfano katika chuo hicho yenye uwezo wa kudahili wanafunzi 640 wenye mahitaji maalum.

Aidha, shule hiyo  itasaidia wanachuo kufanya mazoezi ya kufundisha wanafunzi wenye mahitaji maalumu kwa vitendo na kuwa mahiri katika fani wanazosomea.

“Mnaweza kuona jitihada ambazo serikali imekuwa ikizifanya nitoe wito kwa familia, na wadau wa maendeleo kuendelea kuona umuhimu wa kuchangia juhudi za serikali katika kuwapatia huduma stahihiki wanafunzi wenye mahitaji maalum ili kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika ujifunzaji, " alisema Katibu Mkuu Akwilapo

Dkt. Akwilapo amesema ushiriki wa jamii ni muhimu sana  kwani masuala ya watu wenye ulemavu ni mtambuka hivyo jitihada za pamoja zinahitajika ili kufikia malengo yaliyoanishwa katika miongozo ya kitaifa na kimataifa.

Akizungumzia mafunzo ya TEHAMA na Teknolojia saidizi yanayotolewa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Katibu Mkuu huyo amesema  yanalenga kuwajengea uwezo wakufunzi na walimu wa Sekondari wasioona, viziwi na wenye ualbino  katika matumizi ya TEHAMA na teknolojia saidizi ili  kuboresha ufundishaji katika vyuo vya ualimu na shule za sekondari nchini.

Aliongeza kuwa mafunzo hayo yatawapatia maarifa na stadi kuhusu mfumo, vipengele na utendaji kazi wa kompyuta, utumiaji wa program saidizi za sauti na kukuza maandishi katika kompyuta, kupata stadi za matumizi ya mitandao katika kutafuta na kutuma taarifa mbalimbali katika tovuti na barua pepe pamoja  na kutumia kikamilifu maudhui ya kielektroniki katika ufundishaji na ujifunzaji.

Kwa upande wake Kaimu Kamishna wa Elimu Paulina Mkonongo  alisema, kufanyika kwa mafunzo hayo ni mkakati endelevu wa Serikali kuhakikisha elimu bora inatolewa kwa makundi yote ikiwemo kuimarisha mafunzo kazini kwa kundi hili maalum.

Awali Kaimu Mkurugenzi Msaidizi wa Elimu Maalumu Greyson Mlanga ameeleza kuwa mafunzo hayo yana jumla ya washiriki  140 wenye mahitaji maalumu, wakiwemo viziwi 37, wasioona na wenye uoni hafifu 103  kutoka vyuo vya ualimu vya serikali na walimu wa shule za sekondari nchini.

Akizungumza kwa niaba ya washiriki wa mafunzo, Mkufunzi kutoka Chuo cha Ualimu Morogoro Godfrey Omary amesema anaishukuru Serikali kwa kutoa mafunzo hayo kwa kuwa yanakwenda vikwazo katika vya kiutendaji lakini pia itapunguza utegemezi na hivyo kuongeza ufanisi.

Mafunzo kuhusu matumizi ya TEHAMA na Teknolojia saidizi kwa walimu na wakufunzi na wenye mahitaji maalumu yameanza leo na yanatarajiwa kuhitimishwa  Februari 05, 2020.