Jumapili, 4 Agosti 2019

OLE NASHA: SERIKALI HAITAMVUMILIA MTENDAJI YEYOTE ATAKAYEHUJUMU FEDHA ZA UJENZI WA OFISI ZA UTHIBITI UBORA WA SHULE


 Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha ameagiza watendaji  wa idara ya uthibiti ubora wa shule kusimamia kwa makini miradi ya ujenzi wa ofisi za Uthibiti ubora wa shule pamoja na fedha zinazotumwa kwa ajili ya ujenzi huo katika Halmashauri za wilaya mbalimbali nchini.


Naibu Waziri Ole Nasha amesema hayo mkoani Geita wakati wa ziara ya kukagua miradi ya maendeleo ya sekta ya Elimu inayotekelezwa mkoani humo, ambapo amesema serikali haitamvumilia mtumishi yeyote atakayehujumu ama kutumia vibaya fedha hizo zilizotolewa na wizara kwa ajili ya kujenga ofisi hizo.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita (Hawapo Pichani) baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa ofisi hizo ambapo ameipongeza Halmashauri hiyo kwa usimamizi mzuri wa ujenzi wa ofisi hizo.
Amesema miradi ya ujenzi wa ofisi hizo ni muhimu sana kwa wizara kwani ili kuwa na maendeleo katika sekta ya elimu lazima kuwa na uthibiti ubora wa shule ulio mahiri, wenye uwezo wa kukagua shule na wenye vitendea kazi vya kuwezesha wathibiti ubora wa shule kufanya kazi katika mazingira wezeshi.

“Kama tunataka kuwa na maendeleo katika sekta ya Elimu lazima kuwe na usimamizi thabiti na ndio maana tumechukua hatua mbalimbali kuhakikisha tumeboresha idara ya uthibiti ubora kwa kuhuisha mfumo kutoka kuwa ukaguzi na kuwa uthibiti kwa maana kwamba unashirikisha kila mtu katika hatua zote,” amesema Ole Nasha.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akikangua maendeleo ya ujenzi wa ofisi za wathibiti ubora wa shule katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita ambapo yupo mkoani humo kukagua utekelezaji wa  miradi ya maendeleo ya sekta ya elimu.
Ole Nasha amesisitiza kuwa haiwezekani kufanya kazi ya uthibiti ubora wa shule kama hakuna ofisi, vitendea kazi ikiwemo magari na ndio maana kila Afisa Elimu wa Kata kwa nchini nzima alipewa pikipiki ya kumwezesha kufanya kazi. Serikali pia ilitoa magari 45 kwa wilaya mbalimbali na sasa halmashauri zipatazo 100 zinajengewa ofisi za uthibiti ubora.

Naibu Waziri Ole Nasha amesema baada ya kukamilika kwa ujenzi wa ofisi hizo, Wizara itapeleka vifaa vyote muhimu kwenye ofisi hizo ili kurahisisha kuchakata taarifa zote za elimu kutoka maeneo yote ya nchini kwa lengo la kurahisha huduma za kielimu.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akiangalia baadhi ya vitabu katika maktaba ya shule ya wasichana ya sekondari Nyankumbu alipofikia  shuleni hapo kukagua  chumba chs kompyuta, waziri Ole Nasha yupo Mkoani Geita kwa ziara ya Kikazi
Aidha, Waziri Ole Nasha amesema ameridhishwa na usimamizi na matumizi ya fedha za ujenzi wa ofisi za uthibiti ubora Kanda ya Ziwa ambayo inajumuisha Mikoa ya Geita, Mwanza na Mara ambayo kwa ujumla inajengewa ofisi 15 zenye thamani zaidi ya bilioni 2.28.

Katika ziara hiyo Waziri Ole Nasha amekagua majengo ya uthibiti ubora wa shule katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita na Halmashauri ya mji wa Geita. Ole Nasha pia amekagua ujenzi wa vyumba vya madarasa, mabweni mawili na vyoo katika shule ya sekondari Mwatulole ambayo inatarajiwa kuanzisha kidato cha tano hivi karibuni.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akisikiliza maelezo ya kuhusu kompyuta kutoka kwa wanafunzi wa shule ya sekondari ya Mwatulole s alipofikia  shuleni hapo kukagua  maendeleo ya ujenzi wa mabweni mawili pamoja na madarasa unaotekelezwa na wizara ya Elimu.
Shule nyingine aliyotembelea ni shule ya sekondari ya Wasichana Nyankumbu ambapo ametembelea chumba cha kompyuta na ameahidi kupeleka kompyuta 50 shuleni hapo ili kuongeza ari ya kujifunza.

Awali Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita, Ali Kidwaka alimweleza Naibu Waziri kuwa ameshirikiana na watendaji wengine kufanikisha ujenzi ambao uko kwenye hatua ya ukamilishaji na kuahidi kuwa ataendelea kusimamia ili jengo hilo likamilike kwa wakati.
Muonekana wa jengo la ofisi za uthibiti ubora wa shule ya Halmashauri ya Wilaya ya Geita huku ujenzi ukiendelea. Jengo hili ni moja ya majengo ya ofisi za wathibiti bora kati ya matano yanayoendelea kujengwa katika Mkoa wa Geita.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni