Alhamisi, 8 Agosti 2019

WIZARA YA ELIMU YAKUTANISHA WADAU WA MAFUNZO YA ELIMU YA UALIMU ILI KUTOA MAONI YA KUBORESHA MTAALA WA ELIMU YA UALIMU


Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia Taasisi ya Elimu Tanzania inakusudia kufanya maboresho ya mtaala wa elimu ya ualimu ili iendane na mitaala mipya ya elimu ya Sekondari na msingi ambayo imeanza kutumika mwaka 2015.

Hayo yamesemwa Jijni Dar es Salaam na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. Leonard Akwilapo wakati wa ufunguzi wa mkutano wa wadau wa Elimu ya Ualimu ambao wamekutana kwa lengo la kutoa maoni yatakayosaidia kuboresha usimamizi na maendeleo hususan maboresho ya mtaala  wa elimu ya ualimu.

Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa wadau wa Elimu ya Ualimu kuhusu usimamizi na uendeshaji bora wa Elimu ya Ualimu uliofanyika Jijini Dar es Salaam.


Dkt.Akwilapo alisema mtaala wa mafunzo ya ualimu uliopo sasa ni wa zamani  akitolea mfano mtaala wa mafunzo ya  ualimu kwa walimu wa diploma ambao ni wa mwaka 2008 huku ngazi ya cheti ukiwa wa mwaka  2009 hivyo kutoendana na mtaala mpya wa elimu msingi ambao unazingatia ufundishaji wa KKK.

“Elimu ni suala la Kitaifa hivyo serikali haiwezi kujifanya haisikii jamii inasema nini ndio maana kikao cha wadau kimeitishwa na pia Waziri wa elimu yupo mbioni kuitisha mkutano wa wadau kwa lengo la kupata maoni ya namna bora ya  kuboresha Elimu,”aliongeza Dkt Akwilapo.

Aidha Katibu Mkuu huyo amewataka wadau hao kutumia mkutano huo kujadili na kutafakari kwa kina mfumo wa maandalizi ya walimu nchini kwa kuzingatia mada ya Usimamizi na Maendeleo ya Elimu ya Ualimu, Fursa na Changamoto   pamoja na upimaji na tathmini yake.

“Tumieni mkutano huu vizuri na mambo mtayakojadili yajikite katika kuona ni namna gani mnaboresha mahiri zinazohitajika kwa mwalimu, ama mkufunzi, mazingira na miundombinu wezeshi, uongozi na usimamizi wa mafunzo, upimaji na tathmini ya mafunzo pamoja na maendeleo endelevu ya mwalimu,” alisisitiza Dkt Akwilapo.

Wadau wa Elimu ya Ualimu wakifuatilia hotuba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo wakati wa ufunguzi wa mkutano wa wadau hao uliofanyika jijini Dar es Salaam.


Akizungumza katika Mkutano huo Kamishna wa Elimu Dkt. Lyabwene Mtahabwa  amesema  mkutano huo wa wadau wa  elimu utachochea mabadiliko katika sekta nzima ya elimu kwani ili kufanikiwa katika sekta hiyo ni lazima kuwe na ushirikishwaji wa wadau wa elimu.
 
“Tumekutana kwa ajili ya kuongelea moyo wa Taifa letu, Elimu ni moyo wa taifa unaposema elimu unapozungumzia elimu ya ualimu katika kuleta mabadiliko ya sekta nzima ya elimu,” aliongeza Dkt Mtahabwa.

Dkt Mtahabwa anasema unaweza kujenga shule nyingi, ukawa na vifaa vya kutosha lakini kama hauna walimu bora ni kazi bure hivyo tunataka walimu wawe na waledi, wawe kioo cha jamii kuanzia uvaaji wake, kutembea, kuongea na namna anaivyoishi shuleni na hata kijijini awe mfano wa kuigwa katika jamii.

Kaimu Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo ya Ualimu Augusta Lupokela akizungumza wakati wa Mkutano wa Wadau wa Elimu ya Ualimu ambapo amesema matokeo ya Mkutano huo yatasaidia katika maandalizi ya mpango mkakati wa maboresho ya usimamizi wa mafunzo ya ualimu.


Awali Kaimu Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo ya Ualimu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Augusta Lupokela alimweleza Katibu Mkuu kuwa mkutano huo, pamoja na mambo mengine umelenga kujadili masula yanayohusu usimamizi wa mafunzo ya ualimu na kwamba mada zitakazowasilishwa zitahusu usimamizi na maendeleo ya Elimu ya ualimu, fursa zilizopo pamoja na changamoto.

Aliongeza kuwa matokeo ya mkutano huo ni maandalizi ya mpango mkakati wa maboresho ya usimamizi wa mafunzo ya ualimu ili kufikia malengo ya serikali ya kutoa elimu bora ya ualimu.

Wadau wa Elimu ya Ualimu wakiwa wameshikana mkono huku wakiimba wimbo wa “solidarity” kuashiria umoja katika utekelezaji wa majukumu ili kufikia malengo mapana ya kutoa elimu iliyo bora.


Nae Mratibu wa mradi wa Elimu kwa Walimu (TESP) Ignasi Chonya amesema kupitia mradi anaousimamia wamekuwa wakitoa mafunzo kwa walimu kazini na walimu tarajali kuhusu matumzi ya TEHAMA, ualimu kwa vitendo kwa vyuo vyote vya Serikali na binafsi ili kuwajengea uwezo wa namna ya kufundisha kwa vitendo.

Mkutano wa wadau wa Elimu ya Ualimu unafanyika kwa siku tatu kuanzia Agosti 08, 2019 na  umehusisha wadau kutoka Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa pamoja na Taasisi zake, Viongozi na Mameneja wa shule, vyuo vya ualimu kutoka sekta binafsi, Washirika wa Maendeleo na Wizara ya Elimu.

Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo akiwa katika picha ya pamoja na wadau wa mkutano wa wadau wa elimu ya ualimu baada ya kufungua mkutano huo jijini Dar es Salaam.


Maoni 1 :

  1. Nivyema mkutano ulivyo itishwa kwani ni kweli kuna umuhimu wa kubadili mtaala wa elimu ili elimu yanayotolewa iendane na mabadiliko ya jamii tuliyo nayo na kumuwezesha muhitimu wa mafunzo ya ualimu kuwa na elimu ya kutosha kwa kutumi fursa pia kutoa elimu kwa vijana wengine kuwa wabunifu ili kuendana na mfumo wa maisha wa sasa na badae. Hivyo elimu ya ujasiriamali pia ni ya muhimu.

    JibuFuta