Ijumaa, 14 Julai 2017

Naibu Waziri wa Elimu akagua ujenzi na Ukarabati katika shule ya Sekondari Mbweni Tete


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhandisi Stella Manyanya ameonyesha kutokuridhishwa na hatua ya Halmashauri ya Kinondoni kuhamisha fedha za ujenzi wa madarasa, mabweni na vyoo zilizokuwa zimetolewa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknlojia kupitia mradi wa lipa kwa matokeo kwa shule ya Sekondari ya Kambwangwa na kupelekwa katika Shule ya sekondari Mbweni tete bila kufuata utaratibu wa kuitaarifu wizara iliyotoa fedha hizo.

Mhandisi Manyanya ameyaeleza hayo leo Jijini Dar es Salaam wakati wa ziara yake ya kuzitembelea shule mbalimbali kwa lengo la kukagua utekelezaji wa ujenzi na ukarabati unaofanywa na Mradi wa Lipa kwa Matokeo (P4R). Amesema kuhamishwa kwa mradi si tatizo lakini kuhamisha bila kutoa taarifa ndo tatizo lilipo kwani wizara imetoa fedha nyingi kwa ajili ya ujenzi huo hivyo ni lazima kufanya ufatiliaji ili kuweza kujirizisha kama ujenzi unafanyika lakini wakati najiandaa kwenda Kambagwa ndipo alipotaarifa kuhusu kuhamishwa kwa  mradi huo.

“Leo wakati tunataka kuanza kwenda kuangalia ujenzi ulipofikia lakini tukapewa taarifa kuwa mradi huo haupo Kambangwa na ulihamishwa kupelekwa eneo jingine, hivyo ni muhimu kupeana taarifa maana kuhamishwa kwa mradi kunaleta hoja za ukaguzi” alisisitiza Mhandisi Manyanya.

Naibu Waziri amesema ujenzi wa miundombinu hiyo katika Halmashauri mbali mbali imekuja baada ya wizara ya Elimu kwa kushirikiana na TAMISEMI uwepo wa umuhimu wa kuongeza  miundombinu ya madarasa, mabweni na vyoo katika baadhi ya shule ili kuongeza idadi ya wanafunzi  wanaodahili kwa ajili ya kujiunga na masomo ya kidato cha tano. Amesma lengo la serikali ni kuona wanafunzi wote waliofaulu wanapata nafasi ya kuendelea na masomo yao ya kidato cha tano bila mmoja kuachwa.




Naibu Waziri wa Elimu agiza shule zilizotengwa kwa ajili ya elimu maalum kupatiwa mahitaji muhimu


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhandisi Stella Manyanya ameziagiza Halmashauri zote nchini kuhakikisha shule zilizotengwa kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maalum zinapewa haki zake ikiwa ni pamoja na kupatiwa vifaa vya kufundishia na kujifunzia  ili kuwezesha wanafunzi hao kupata elimu sawa na wanafunzi wengine.

Naibu Waziri Manyanya ametoa agizo hilo alipofanya ziara kwenye shule ya msingi  Sinza Maalum iliyopo jijini Dar es Salaam kwa lengo la kujionea mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji katika shule hiyo, mbapo  pia amezitaka halmashauri hizo kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa mabweni yatakayosaidia kupunguza ugumu wa wanafunzi hao kuhudhuri masomo  kutokana na sababu mbalimbali za kimaumbile za watoto hao na hivyo kuwafanya wengine kushindwa kutembea umbali  mrefu kufuata shule.

Pia Naibu waziri alitembelea shule ya sekondari ya Mbweni Teta kukagua ujenzi wa madarasa, mabweni na vyoo unaofanywa na Wizara ya Elimu, Sayasni na Teknolojia Kupitia Programu ya lipa kulingana na matokeo, P4R kwa ajili ya wanafunzi wa kidato cha Tano wanaotarajiwa kuanza shule Julai 17, mwaka huu.






Jumanne, 11 Julai 2017

Naibu Waziri wa Elimu akabidhi Bendera ya Taifa kwa wanafunzi wa Sayansi


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhandisi Stella Manyanya leo amekabidhi Bendera ya Taifa kwa wanafunzi saba wanaosoma masomo ya sayansi wanaokwenda kuiwakilisha nchi katika mashindano ya First Global Challenges nchini Marekani. Makabidhiano hayo yamefanyika katika shule ya Sekondari ya  wasichana Jangwani.

Katika makabidhiano hayo Mhandisi Manyanya amewataka wanafunzi wote nchini kusoma kwa bidii masomo ya sayansi, teknolojia na ubunifu ili kuhakikisha ndoto ya Tanzania ya kuwa na uchumi wa kati kupitia viwanda na biashara inafanikiwa na kwamba wizara tutaendelea na jukumu lake la kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia ili wanafunzi wote waendelee kufanya vizuri katika masomo ya sayansi.

Shule zilizotoa wanafunzi watakaoshiriki katika mashindano hayo ni pamoja na Jangwani, Azania, Jamhuri, Benjamini Mkapa, Feza na Kisutu.

Naye mratibu wa mashindano hayo kwa upande wa Tanzania ndugu Mkufu Shabani Tindi alisema mashindano haya yameanzishwa na kufadhiliwa na shirika lisilokuwa la kiserikali la Marekani liitwalo FIRST yenye maana ya for inspiration and recognition of science and technology lenye lengo la kuhamasisha ulimwenguni kote vijana wanaosoma masomo ya sayansi, uhandisi, teknolojia na hesabu kuweza kutatua changamoto mbalimbali ulimwenguni

Wanafunzi watakaoshiriki wanatarajia kuondoka kesho Juni 12, 2017 na watakuwa nchini Marekani kwa ajilia ya mashindano hayo makubwa  kiulimwengu ambapo  zaidi ya nchi 170 zitashiriki.

Naye mmoja wa washiriki Raymond Benedict kutoka Shule ya Sekondari Jamhuri amesema yeye wenzake wamejiandaa vizuri katika kuhakikisha wanaiwakilisha nchi katika mashindano hayo vizuri na kwa ufahari.







Jumamosi, 17 Juni 2017

MAADHIMISHO YA KILELE CHA SIKU YA MTOTO WA AFRIKA.

Mkurugenzi wa Elimu ya Juu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Sylivia Temu amewataka Wazazi, walezi na walimu  kuwalea watoto  katika misingi ambayo itawafanya wawe na maadili mema ili waje kuwa viongozi, na  wazazi bora katika maisha yao ya baadae.

Profesa Temu amesema hayo hii leo katika maadhimisho ya kilele cha siku ya mtotot wa Afrika ambayo yamefanyika kwenye kijiji cha Humekwa, Wilayani Chamwino mkoani Dodoma.

Profesa Temu amesewasihi Watoto kupenda kusoma na kuacha kujiingiza kwenye makundi ya matumizi ya  dawa za kulevya, na badala yake watoto wajikite zaidi katika kusoma kwa bidii ili wawe  viongozi bora na wenye maadili sahihi katika taifa letu.

Kauli mbiu ya maadhimisho ya  siku ya mtoto wa Afrika ni: Maendeleo Endelevu 2030 " Imarisha Ulinzi na Fursa Sawa kwa Watoto."

Maadhimisho hayo ambayo kufanyika kila mwaka juni 16 yameadhimishwa kwenye mikoa mbalimbali nchini kote.










Jumatano, 24 Mei 2017

Wasichana na Wanawake kuwezeshwa kupitia elimu


Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknoloji Dkt Leonard Akwilapo leo amefungua warsha ya kuanzishwa kwa mradi wa pamoja wa uwezeshaji wa wasichana na wanawake  kupitia elimu kwa lengo la kuwatafakarisha wilaya lengwa (Ngorongoro, Kasulu, Sengerema,micheweni na mkoani pemba) juu ya vikwazo vya elimu kwa wasichana katika maeneo yao na kubuni mikakati mbalimbali ya kukabiliana navyo ili wasichana wapate fursa ya kujiendeleza kielimu na kukuza fursa ya kuwa raia bora Zaidi.

Mradi huu wenye thamani ya dola za kimarekani milioni tano unafadhiliwa na shirika la Kimataifa la Maendeleo la Korea (KOICA) kupitia Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) ambapo unatarajiwa kuwanufaisha wasichana na wasichana 8,000 walioko shuleni na wasichana 600 walio nje ya shule, kwa kuwapatia fursa ya kuimarisha ujuzi wao wa msingi, ufundi na ujuzi wa kawaida ambao utawawezesha kuwa raia bora katika nchi yao na ulimwengu kwa ujumla ikiwa ni pamoja na kuchangia kikamilifu katiak maendeleo ya Tanzania.

Akizungumza wakati wa ufunguzi Katibu Mkuu amesema Awamu ya kwanza ya mradi huu unalenga nchi tatu ambazo ni Tanzania, Mali na Nepal na utaratibiwa na Wizara ya elimu Sayansi na Teknolojia, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto na Wizara ya katiba na Sheria na kutekelezwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni pamoja na UNFPA na UN Women.

Mradi huu ni sehemu ya mpango wa ulimwengu kupitia mashirika ya UNESCO, UNFPA na UN Women kwa ajili ya kuwawezesha wasichana kupitia elimu uliozinduliwa katika nchi sita duniani kote.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt Leonard Akwilapo akifungua warsha ya kuanzishwa kwa mradi wa pamoja wa uwezeshaji wa  Wanawake na Wasichana kupitia Elimu, mkutano ambao umefanyika jijini Dar es salaam hii leo.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt Leonard Akwilapo akifuatilia Makala zilizoandaliwa kuonyesha namna Wasichana  na Wanawake wanavyofurahia kupata Elimu ya namna ya kujikinga na matatizo katika jamii yanayoambatana na mila potofu kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni. (UNESCO.)

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt Leonard Akwilapo akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa warsha mara baada ya ufunguzi wa warsha ya kuanzishwa kwa mradi wa pamoja wa uwezeshaji wa wasichana na Wanawake kupitia Elimu.



Jumanne, 23 Mei 2017

Ushiriki wa Waziri wa Elimu Sayansi, na Teknolojia katika Mkutano Mkuu wa 18 wa kawaida wa Wakuu wa Nchi zinazounda Jumuiya ya Afrika Mashariki

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli wakati wa Mkutano Mkuu wa 18 wa Wakuu wa Nchi zinazounda Jumuiya ya Afrika Mashariki, uliifanyika hivi karibuni Ikulu jijini Dar Es Salam, Tanzania.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako pamoja na Waziri wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dkt. Augustine Mahiga wakibadilishana uzoefu na baadhi ya wajumbe wa Mkutano Mkuu wa 18 wa Kawaida  wa Wakuu wa Nchi zinazounda Jumuiya ya Afrika Mashariki, uliofanyika mwishoni mwa wiki Ikulu, jijini Dar es Salaam, nchini Tanzania.



 Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Afrika Mashariki likiwa katika picha ya pamoja na viongozi Wakuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wakati wa Mkutano Mkuu wa Kawaida wa 18 uliofanyika hivi karibuni Ikulu jijini Dar es Salaam, nchini Tanzania.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akiwa na baadhi ya Mawaziri wa Tanzania wanaounda Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Afrika Mashariki wakifuatilia Mkutano Mkuu wa 18 wa Wakuu wa Nchi wa Jumuiya hiyo uliofanyika hivi karibuni, Ikulu jijini Dar es Salaam, Tanzania

Ijumaa, 12 Mei 2017

MKUTANO WA BARAZA LA WAFANYAKAZI WA WIZARA YA ELIMU SAYANSI NA TEKNOLOJIA-MOROGORO


Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Saimon Msanjila amezindua mkutano wa 24 wa baraza la wafanyakazi wa Wizara ulioanza leo katika ukumbi wa Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine mjini Morogoro ambapo amewaasa watumishi kufanya kazi kwa weledi na maarifa zaidi ili kuleta ufanisi utakaokuwa na tija.

 Profesa Msanjila amesema ili kuleta mabadiliko katika sekta ya elimu ni lazima watumishi kubadilika na kufanya kazi kwa kujituma na kuachana na tabia ya kufanya kazi kwa mazoea.

Profesa Msanjila  amesisitiza kuwa wizara ina wajibu wa kuhakikisha nchi inakuwa na elimu bora ili kupata wahitimu na wataalam watakaowezesha nchi kufikia lengo la kuwa na  uchumi wa viwanja.

Aidha, amewataka wajumbe wa mkutano kujielekeza zaidi katika mbinu na mikakati ya utekelezaji kwa kushirikiana na uongozi wa Wizara ili kukamilisha malengo ya mwaka 2016/17 na malengo mapya ya mwaka 2017/18.