Ijumaa, 1 Novemba 2019

SERIKALI YATENGA BILION 201 KWA AJILI YA UBORESHAJI NA UJENZI WA MIUNDOM...

SERIKALI KUIMARISHA MICHEZO KATIKA VYUO VYA UALIMU


Serikali ya Awamu ya Tano imeweka kipaumbele katika kuimarisha michezo kama eneo muhimu la mtaala wa mafunzo ya ualimu kutokana na ukweli kwamba michezo inaimarisha stadi za kujifunza, nidhamu na ni ajira pia.

Hayo yamesemwa Mkoani Mtwara na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha wakati wa kufunga Mashindano ya Kitaifa ya Michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu Tanzania Bara (UMISAVUTA).
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akitoa kombe la ushindi wa mpira wa miguu kwa wachezaji wa Kanda ya Ziwa wakati wa ufungaji wa mashindano ya Kitaifa ya Michezo na Sanaa ya Vyuo vya Ualimu UMISAVUTA yaliyomalizika mkoani Mtwara.

Amesema pamoja na kuwepo kwa mchepuo wa michezo katika baadhi ya vyuo vya Ualimu ni vizuri vyuo hivyo kupitia Ofisi ya Kamishna wa Elimu wakaweka mikakati ya kuhakikisha kuwa ufundishaji na ujifunzaji wa michezo na Sanaa unalenga kuwawezesha vijana kufanya vizuri katika eneo hilo kwa maendeleo yao na Taifa.

Ametaja vyuo ambavyo kwa sasa vinatoa mchepuo wa michezo kuwa ni Chuo cha Ualimu Tarime, Butiama, Butiama Mtwara Kawaida na Ilonga na kwamba Wizara itahakikisha kuwa michezo inaimarishwa katika vyuo vyote vya ualimu nchini.

Naibu Waziri Ole Nasha amevitaka vyuo vya ualimu kuhakikisha vinaendeleza michezo chuoni kutoka na faida zitokanazo na michezo ikiwa ni pamoja na kuhakikisha  wahitimu wa mafunzo ya ualimu wanapata mafunzo ambayo wakihitimu wanakwenda kuwa walimu mahiri wa michezo katika shule za msingi na sekondari ambapo ndipo wanamichezo na wasanii wanaandaliwa.

“Nimefarijika kuona mashindano ya michezo na Sanaa kwa vyuo vya ualimu imerudi tena baada ya kutokuwepo kwa miaka 20 iliyopita hatuna budi kuwekeza katika michezo kwa sababu ni fursa za kuweza kusaidia kukua kiuchumi. Nchi nyingi duniani michezo imekuwa sehemu kubwa ya kusaidia kukua kiuchumi,” alisema Naibu Waziri Ole Nasha.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akisalimiana na wachezaji kabla ya kuanza mechi ya fainali wakati wa ufungaji wa Mashindano ya Kitaifa ya Michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu Tanzania Bara yaliyofanyika Mkoani Mtwara.

Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Mtwara ambae pia ni Afisa Elimu Mkoa Germina Mng’aho amesema kufanyika kwa michezo hiyo ni utekelezaji wa ilani ya Chama cha Mapinduzi ambayo inataka kuwepo kwa mashindano ya michezo kwa shule na vyuo ili kuwezesha kuinua vipaji ambavyo vitaleta mafanikio katika michezo ya kitaifa na kimataifa.

Nae Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Seksheni ya Mafunzo ya Ualimu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Agusta Lupokela amesema anaishukuru Serikali ya Awamu ya Tano kwa kutambua faida zinazopatikana katika michezo ikiwemo stadi za kujifunza na kuamua kurejesha mashindano ya michezo kwenye Vyuo vya Ualimu.
Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Seksheni ya Mafunzo ya Ualimu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na TeknolojiaAgusta Lupokela akikabidhi kikombe kwa mwakilishi wa Kanda ya Kaskazini ambao ni washindi wa mbio wakati wa kufunga mashindano ya Kitaifa ya Michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu, UMISAVUTA mkoani Mtwara

Akitoa taarifa ya mashindano hayo kwa  Naibu Waziri Mwenyekiti wa UMISAVUTA Taifa Agustine Sahili amesema kuwa michezo hiyo imeendeshwa kulingna na taratibu za michezo na matokeo yameamuliwa kwa weledi na haki katika kupata washindi.

Sahili ameiomba  Wizara  kuimarisha kozi ya michezo na fani mbalimbali za ndani katika vyuo vya ualimu ili wataalamu waweze kupatikana shuleni ambako ndiko chimbuko halisi la vipaji linapatikana lakini pia kuwajengea uwezo wasimamizi na waamuzi wa michezo kwa kuendesha kozi fupi na ndefu kwa kushirikiana na Wizara ya Habari Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Pia ameiomba Wizara kuongeza wakufunzi wa michezo na Sanaa vyuoni kwani kwa sasa vyuo vingi havina wakufunzi wa aina hiyo hali inayodunisha uendeshaji wa michezo na ukuzaji wa vipaji kwa vijana chuoni ambapo pia inasababisha shule za msingi na sekondari kukosa walimu mahiri katika michezo na Sanaa.
Wanamichezo wakipita mbele ya mgeni rasmi (hayupo pichani) wakati wa kufunga mashindano ya Kitaifa ya Michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ulimu yaliyofanyika Mkoani Mtwara.

Nae Mshiriki wa Mashindano ya Michezo na Sanaa Albert Thomas kutoka Kanda ya Ziwa ameishukuru Serikali kwa kurejesha mashindano ya UMISAVUTA kwani inasaidia kujenga afya na  akili lakini pia inasaidia kuwa na uelewa wa masula ya michezo na kutoa elimu ya michezo kwa wanafunzi ambao watakwenda kuwafundisha  baada ya kumaliza masomo. Ameiomba Serikali kuendeleza vipaji vya wanamichezo wanaoshindana katika mashindano ya ngazi ya shule na vyuo na kuonekana washindi ili vipaji hivyo visiishie kwenye ngazi ya kitaifa bali katika ngazi ya kimataifa.

Ufungaji wa mashindano ya Kitaifa ya Michezo na Sanaa kwa vyuo vya ualimu yaliyoanza Oktoba 25, 2019 na kuhitimishwa Oktoba 31, 2019 yamepambwa na mechi kati ya Kanda ya ziwa na kanda ya kusini ambapo kanda ya ziwa wameibuka kidedea baada ya kuwafunga kanda ya kusini goli moja kwa sifuri.
Kanda ya Ziwa wakifurahia kupata vikombe vya ushindi katika michezo mbalimbali ambayo wameshindania katika mashindano ya kitaifa ya michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu Tanzania Bara yaliyofanyika Mkoani Mtwara.

Jumapili, 27 Oktoba 2019

WIZARA YA ELIMU YAPONGEZWA KWA KUREJESHA MASHINDANO YA UMISAVUTA


Serikali imeipongeza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kutekeleza agizo la kurudisha mashindano ya Michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu (UMISAVUTA) huku ikiitaka kuhakikisha kuwa michezo na Sanaa vinapewa kipaumbele katika mipango endelevu ya Wizara.

Pongezi hizo zimetolewa Mkoani Mtwara. na Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe kwa niaba ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Mjaliwa wakati wa ufunguzi wa mashindano ya UMISAVUTA.
Mgeni rasmi Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe akipiga mpira kuashiria uzinduzi rasmi wa mashindano ya michezo na sanaa kwa vyuo vya ualimu nchini katika viwanja vya Nangwada Sijaona mkoani Mtwara.

Dkt. Mwakyembe amesema eneo la michezo na Sanaa ni sehemu muhimu katika makuuzi ya watoto kwani yanajenga na kuimarisha afya ya mwanadamu lakini pia yanaimarisha mahusiano baina ya raia.

“Kwa sasa nchi imeonesha mafanikio makubwa katika michezo hivyo ili Taifa lipate wataalamu na vipaji sahihi katika michezo na Sanaa hatuna budi kuanza ngazi za awali za elimu, “alisema Dkt. Mwakyembe.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. leonard Akwilapo amesema Wizara imejipanga vyema katika kuendeleza michezo ili kuongeza furaha kwa wananchi wa Tanzania kwa kuziona timu zinashiriki na kushinda mashindano makubwa ya kimataifa.

“Kama Wizara tunasema muda wa kushiriki sasa umetosha tunataka kuwa washindani na mashindano haya ni sehemu ya maandalizi ya kutekeleza azma hiyo,” alisema Katibu mkuu Akwilapo.
Mgeni rasmi Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe akisalimiana  na washiriki wa mashindano ya michezo na sanaa kwa vyuo vya ualimu nchini wakati wa ufunguzi wa mashindano hayo mkoani Mtwara.

Katibu Mkuu Akwilapo alisema kupitia mashindano haya washiriki wataongeza ujuzi  katika michezo na kuwa walimu ambao wataimarisha michezo wakati watakapokuwa kazini huku wengine wakiendeleza vipaji vyao na kuwa hazina ya Taifa kwa siku za usoni.

Michezo inayoshindaniwa ni pamoja na mpira wa Pete, mpira wa miguu, wavu kikapu, riadha, mashindano ya uchoraji, Sanaa za maonesho, ngoma pamoja na kwaya. Mingine ni pamoja na ile ya kutengeneza zana za kufundishia na kujifunzia kwa lengo la kumjengea mwalimu umahiri wa kuandaa na kutumia zana nzuri za kufundishia.
Baadhi ya Walimu Tarajali wakiingia  katika uwanja wa Nangwanda mkoani Mtwara wakati wa ufunguzi wa mashindano ya michezo na sanaa kwa vyuo vya ualimu nchini mapema hii leo mkoani Mtwara.

Nae Kaimu Mkurugenzi Msaidizi kutoka Seksheni ya Mafunzo ya Ualimu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Agusta Lupokela amesema mashindano hayo yaliyoanza Oktoba 25, 2019 yanatarajiwa kuhitimishwa Oktoba 31, 2019 na yameshirikisha Kanda saba ambazo ni Kanda ya Kati, Kusini, Mashariki, Magharibi, Kanda ya Ziwa, Kaskazini na Kusini ambazo zimeundwa kulingana na vyuo vya ualimu.

Juni 10, 2019 katika Viwanja vya Nagwanda Sijaona mkoani Mtwara wakati Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anafungua mashindano ya UMISSETA na UMITASHUMTA alitoa agizo kwa Wizara ya Elimu kuhakikisha kuwa mashindano ya michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu yanarejeshwa.
Baadhi ya Walimu Tarajali wakiandamana kuelekea katika uwanja wa Nangwanda mkoani Mtwara wakati wa ufunguzi wa mashindano ya michezo na sanaa kwa vyuo vya ualimu nchini mapema hii leo mkoani Mtwara.

Alhamisi, 17 Oktoba 2019

WAZIRI NDALICHAKO ATAKA MKUU WA SHULE KASANGEZI KUHAMISHWA


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako ametilia shaka matumizi ya fedha za serikali zaidi ya shilingi milioni mia tano zilizotolewa kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa shule ya sekondari Kasangezi iliyopo wilayani Kasulu mkoani Kigoma.

Akizungumza mara baada ya kukagua utekelezaji wa mradi huo waziri Ndalichako amesema shule hiyo imepatiwa zaidi ya shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa 4, mabweni 4 yenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 80 katika kila moja, matundu ya vyoo 10, bwalo pamoja na ukarabati wa maabara.

Ndalichako amesema  kazi iliyofanyika haiendani na fedha iliyotolewa kutokana na miundombinu hiyo kujengwa chini ya Kiwango.

“Milango ya madarasa na hata ya mabweni mmetengeneza kwa mbao laini tofauti na BOQ pamoja na kuwa laini ina uwazi hii nataka itolewe, tazama sakafu imeshaharibika hapa hata mwaka haujaisha mabweni mliambiwa ya watu themanini mmejenga ya watu sitini"
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako akiangalia mlango wa darasa ambao umetengenezwa kwa mbao laini kinyume cha taratibu katika shule ya sekondari Kasangezi

Kufuatia hali hiyo ndalichako ameagiza kuwa ujenzi wa mabweni urudiwe kwa kuzingatia BoQ na ameaguza ujenzi huo uwe umekamilika ifikapo desemba.

"Nitakuja mwenyewe mwezi wa kwanza kukagua kama hayo yatakuwa hayajatekelezwa mengine yatafuata,” amesema waziri Ndalichako.

Aidha waziri Ndalichako amemuagiza  Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kasulu Mhandisi  Godfrey Kasekenya  kumuondoa  mara moja shuleni hapo mkuu wa shule hiyo kwa kushindwa kusimamia  vizuri kazi hiyo na hivyo kuisababishia hasara serikali.

“Kwanza ujenzi wa mara ya kwanza hata matofali hukununua ulichukua kwenye benki ya wananchi na tayari nilikuwa nimeleta fedha sasa kwanini hukujiongeza hata ukarekebisha ofisi ya Mkuu wa Shule ambayo iko katika hali isiyoridhisha vitu vingine ni kudhalilisha Serikali, Mkurugenzi muahamishe huyu katika shule hii,” alisema waziri Ndalichako.


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako akikagua maendeleo ya  ujenzi wa moja ya bweni katika shule ya sekondari Kasangezi iliyoko Halmashauri ya wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma.

Waziri Ndalichako pia ameitaka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na  Rushwa (TAKUKURU) wilayani Kasulu   kufuatilia muenendo wa upatikanaji wa madawati miamoja themanini yaliyonunuliwa katika mradi huo kama yametimia na yamenunuliwa kwa kufuata utaratibu.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kasulu Kanali Saimon Anange amekiri kuwepo uzembe katika kusimamia miradi hiyo na kumuhakikishia waziri Ndalichako kuwa ofisi yake itafanyia kazi maelekezo yote aliyoyatoa katika ziara hiyo.

Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolijia Prof. Joyce Ndalichako yupo mkoani Kigoma Kwa ziara ya Kikazi akikagua miradi ya elimu inatekelezwa kupitia fedha za Programu ya lipa kwa matokeo EP4R.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako akikagua mlago wa darasa ambao umetumia mbao laini tofauti na maelekezo katika shule ya sekondari Kasangezi.

Jumatano, 16 Oktoba 2019

WAZIRI NDALICHAKO ATOA SIKU 15 KWA MSHAURI ELEKEZI BICO KUFANYA TATHMINI YA GHARAMA ZA UJENZI CHUO CHA UALIMU KABANGA


Wakati Mradi wa ujenzi wa Chuo cha Ualimu Kabanga kilichopo Wilayani Kasulu  mkoani Kigoma ukiendelea kwa kusuasua Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako ametoa siku 15 kwa Mshauri Elekezi BICO  kupitia upya gharama za ujenzi wa mradi huo ambazo ni  zaidi ya shilingi bilioni kumi  ili kujiridhisha kama fedha hiyo inaendana na ukubwa wa mradi.

Prof. Ndalichako ametoa agizo hilo mara baada ya kufanya ziara ya kukagua mradi huo ambapo pamoja na kutoridhishwa na kasi ya Mkandarasi ametilia shaka gharama ya  ujenzi ambayo ni zaidi ya shilingi bilioni kumi kutumika ndivyo sivyo kutokana na aina ya majengo yanayojengwa katika chuo hicho kuwa ya thamani ndogo.

"Hivi ni vighorofa mtoto na narudia ni vighorofa mtoto huwezi kuniambia kwamba majengo haya ambayo kwanza ni machache, pili siyo ghorofa zile kubwa kama tulizojenga katika miradi mingine tena kwa gharama ndogo ya shilingi bilioni sita zinazidiwa na vighorofa hivi hapa kuna kitu hakipo sawa nataka ndani ya siku kumi na tano gharama za mradi zipitiwe upya kwa kila jengo na nipewe taarifa vinginevyo mratibu wa miradi hii utafute kazi nyingine," alisema Prof. Ndalichako.
Injinia wa mradi wa ujenzi wa Chuo cha Ualimu Kabanga akimuonesha Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako namna chuo cha Ualimu Kabanga kitakavyoonekana baada ya ujenzi kukamilika

Kuhusu kusuasua kwa Mradi Waziri Ndalichako amemtaka Mkandarasi huyo ambaye ni Kampuni ya SUMA JKT kuongeza kasi ya kufanya kazi akisisitiza ziletwe mashine za kisasa ambazo zitarahisisha kazi pamoja na kuongeza vibarua kwenye eneo la kazi.

"Huwezi kutekeleza mradi wa zaidi ya shilingi bilioni kumi kama nyumba yako unayojenga, yaani una kamashine kamoja tena kakusukuma,vibarua wenyewe inaonekana umewaleta leo baada ya kusikia nakuja kukagua, hii haikubaliki tunataka kazi ifanyike usiku na mchana kwa sababu pesa zipo lazima mradi ukamilike haraka," alisema Waziri  Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako akikagua mradi wa ujenzi wa Chuo cha Ualimu, Kabanga unaojengwa na Wizara kupitia Mradi wa TESP wilayani Kasulu mkoani Kigoma

Mapema akitoa  taarifa  ya mradi huo, Kaimu Mkuu wa Kanda ya Ujenzi SUMA JKT, Luteni Kanali Onesmo Njau amesema mpaka sasa ujenzi umekamilika kwa asilimia thelathini na kudai kukabiliwa na changamoto kadhaa ikiwemo  usumbufu wa kupata vifaa vya ujenzi kama saruji na mchanga.

"Mheshimiwa Waziri tulikuwa tukitegemea kupata saruji kwa kampuni ya Dangote lakini kwa sasa inabidi tufuate wenyewe Dodoma na hivyo kutumia muda mwingi kusubiri vifaa vifike kwenye eneo la mradi," alisema Kanali Njau.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako akikagua ujenzi wa Chuo cha Ualimu Kabanga Kasulu Mkoani Kigoma

Naye mshauri elekezi wa mradi huo kutoka BICO, Fred Munishi amekiri kuwa kazi inasuasua na kusema kuwa tayari ametoa maelekezo kwa Mkandarasi kuongeza kasi ya ujenzi taarifa ambayo hata hivyo imeonekana kukinzana na taarifa ya Mkandarasi na hivyo kutakiwa kufanya kazi kwa karibu na Mkandarasi.

"Inaonekana hapa hakuna maelewano mazuri baina ya Mkandarasi na mshauri elekezi, sitaki mivutano kazini kaeni pamoja fanyeni kazi ya serikali na mkiendelea hivi tutawaondoa," alisema Waziri Ndalichako.

Akiwa katika Halmashauri ya wilaya ya Kasulu, Waziri Ndalichako pia amekagua miradi mingine minne ya elimu katika shule za sekondari na msingi za Kigodya, Ruhita, Nyantare  na Kasyenene na kueleza kuridhishwa na kazi huku akisisitiza kuwa serikali inatoa fedha ili kuona matokeo.

Katika ziara hiyo Waziri Ndalichako aliambatana pia na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Dkt. AveMaria Semakafu pamoja na Mratibu wa Mradi wa Lipa Kulingana na Matokeo pamoja na ule wa TESP.
Muonekano wa sasa wa hatua ya ujenzi wa baadhi ya majengo katika eneo la mradi wa Chuo cha Ualimu Kabanga wilani Kasulu Mkoani Kigoma

UKARABATI CHUO CHA MZUMBE NA MIAKA 20 BILA MWALIMU NYERERE