Jumanne, 26 Septemba 2017

KKK NA UBORESHAJI MIUNDOMBINU GEITA

Mkuu wa mkoa wa Geita Meja Jenerali Ezekiel Kyunga amesema ujenzi na uboreshaji wa miundombinu unaotekelezwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia  programu ya Lipa kulingana na Matokeo ( P4R ) umepunguza changamoto ya uhaba wa madarasa uliokuwa unaukabili mkoa huo kutokana na kuwepo kwa mwitikio mkubwa wa wazazi wa kuandikisha watoto kujiunga na darasa la kwanza.

Kyunga amesema mkoa huo ulipatiwa kiasi cha shilingi milioni 194 kutoka Programu ya P4R ambazo zimejenga madarasa Nane, kuweka umeme shuleni hapo na uchimbaji wa  kisimana hivyo kutatua changamoto ya upatikanaji wa maji.


Shule za msingi zilizotembelewa ni pamoja na Nguzombili,   Kalangalala ambazo zina madarasa ya awali mpk darasa la tatu, (madarasa yanayoongea)pamoja na kituo cha wanafunzi wenye mahitaji maalumu  kilichopo kwenye shule ya Mbugani.

Mwanafunzi wa  darasa la kwanza wa Shule ya msingi kalangalala iliyopo mkoani Geita akisoma ubaoni mbele ya wanafunzi wenzako pale alipotakiwa kufanya hivyo na Mwalimu wake. Hii ni kufuatia ziara ya Maafisa wa kitengo cha mawasiliano Wizarani pamoja na wanahabari ambao wanafuatilia ujifunzaji na ufundishaji wa KKK.


Programu ya Lipa kulingana na matokeo imesaidia kupunguza changamoto ya uhaba wa vyumba vya madarasa katika shule ya msingi Nguzo mbili, iliyopo mkoani Geita pia shule hiyo umeweza kuweka umeme na kuchimba kusoma na hivyo kutatua changamoto ya maji shuleni hapo


Moja ya darasa linaloongea lililopo kalangalala, mkoani Geita ambalo hutumiwa na wanafunzi wa awali shuleni hapo. Kuanzishwa kw mtaala wa KKK kumewafanya wanafunzi kupenda shule, imesaidia kupunguza utoro kwa wanafunzi na pia imechangia ufaulu wa wanafunzi.

TATHMINI YA MWAKA 2016, P4R

Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na OR - TAMISEMI kwa kushirikiana na Washirika  wa maendeleo leo wamekutana mjini Dodoma kufanya Tathmini  ya utekelezaji wa Programu ya Lipa Kulingana na Matokeo ( EP4R)  kwa mwaka 2016/17 ili kuona mafanikio yaliyopatikana, changamoto na kuweka mikakati ya kutatua changamoto zilizopo katika suala la utoaji wa Elimu bora Nchini.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo Mratibu wa Programu ya Lipa Kulingana na Matokeo  Gerald Mweli kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia amesema programu hiyo inafanya tathmini ili kujua hali halisi ya utekelezaji wa majukumu, kwa kiasi gani mradi umefanikiwa lakini pia kuona changamoto na namna ambavyo serikali kwa kushirikiana na washirika wa watakavyozitatua.

Mweli ametaja  mafanikio yaliyopatikana kupitia mradi huo,kuwa ni pamoja na  kujenga na kukarabati  miundombinu chakavu ya shule za Msingi na Sekondari zipatazo 361 kutoka katika Halmashauri 129, vyumba vya mdarasa 1,435, mabweni 261, majengo ya utawala 11, mabwalo 4, vyoo 2,832, nyumba za walimu 12, maktaba 4, na uwekaji wa maji katika shule nne (4).

Kwa upande wa vyuo vya ualimu programu imefanikiwa kukarabati  vyuo 10 vya ualimu ikiwa ni pamoja na kununua  compyuta 260 zitakazowawezesha walimu  kutekeleza  majukumu yao kwa urahisi, magodoro 6,730 yatakayotumiwa na wanafunzi pamoja na viti 1976 kwa ajili ya wanachuo.


Aidha, programu imenunua vifaa vya maabara 1,696 kwa ajili ya shule za sekondari ambavyo zitasaidia katika ufundishaji wa masomo ya sayansi na kuongeza uelewa kwa wanafunzi.


Jumatano, 9 Agosti 2017

TANGAZO LA NAFASI ZA KAZI KWA WALIMU WA SHULE ZA MSINGI NA SEKONDARI.



1.0     Serikali inatarajia kuajiri Walimu 92 wa Shahada na 174 wa Stashahada wa masomo ya Fizikia, Hisabati, Kilimo na Biashara kwa Shule za Sekondari na Walimu 2,767 wa Cheti kwa Shule za Msingi.

2.0     Waombaji kwa shule za Sekondari wawe waliohitimu mafunzo ya Ualimu mwaka 2016 au kabla, na wale wa Shule za Msingi wawe waliohitimu mafunzo yao mwaka 2014 au kabla. 

3.0     Sifa za Waombaji:

3.1     Walimu wa Sekondari:
(i)          Shahada ya Elimu (Bachelor with Education) au Shahada ya Ualimu (Bachelor of Education) yenye somo moja la kufundishia au zaidi au Shahada isiyo ya Ualimu/Elimu yenye somo moja la kufundishia au zaidi pamoja na Stashahada ya Uzamili ya Elimu (Postgraduate Diploma in Education) kutoka Vyuo vya Elimu ya Juu vinavyotambulika na Serikali. Masomo ya kufundishia ni kati ya Fizikia, Hisabati, Kilimo au Biashara.
(ii)        Stashahada ya Ualimu katika masomo yaliyoainishwa kwenye kipengele Na. 2.1 (i) hapo juu.
(iii)      Cheti cha Kidato cha Sita
(iv)       Cheti cha Kidato cha Nne

3.2     Walimu wa Shule za Msingi:
(i)          Astashahada ya Ualimu iliyotolewa na Chuo kinachotambuliwa na Serikali.
(ii)        Cheti cha Kidato cha Nne (wenye cheti Kidato cha Sita watapewa kipaumbele).

4.0     Utaratibu wa Kutuma Maombi:
(a)        Maombi yatumwe kupitia Posta kwa njia ya Rejesta (EMS).  Juu ya bahasha iandikwe kwa mkono "Maombi ya Kazi ya Ualimu - Sekondari au Maombi ya Kazi ya Ualimu - Msingi".

(b)        Mwombaji aambatishe nakala za Vyeti vilivyothibitishwa (Certified) na Mwanasheria pamoja na "Transcript".

NB:  Barua za maombi zisiwasilishwe kwa mkono.  Barua zitakazowasilishwa kwa mkono hazitapokelewa.


5.0     Masuala Mengine ya Kuzingatia:
(a)        Mwombaji aandike majina yake yote matatu.  Kama Vyeti vina majina mawili, utaratibu wa kisheria wa kuongeza jina uzingatiwe.
(b)        Mwombaji aambatishe nakala ya Cheti cha Kuzaliwa.

Mwisho wa kupokelewa maombi ni tarehe 31/08/2017.

Maombi yatumwe kwa:
Katibu Mkuu,
Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia,
             S. L. P. 10,
           40479 DODOMA.           

Imetolewa na:

KATIBU MKUU

WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA

Alhamisi, 27 Julai 2017

Waziri Mkuu afungua Maonyesho ya 12 ya Vyuo vya Elimu ya Juu


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassimu Majaliwa Majaliwa ameitaka Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania TCU kuhakikisha programu za masomo zinazoanzishwa na Vyuo vya elimu ya juu nchini zinazingatia mahitaji ya Taifa na soko la ajira.

Waziri Mkuu ametoa agizo hilo leo katika ufunguzi wa maonyesho ya kumi na mbili (12) ya vyuo vya elimu ya juu yaliyofanyika katika Viwanja vya Mnazi mmoja jijini Dar es Salaam ambapo amesema serikali inayathamini maonesho hayo kwa kuwa yanatoa fursa ya vijana kujifunza na kupata taarifa za vyuo na programu wanazoendesha  moja kwa moja

Naye Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Saimon Msanjila ameitaka TCU kuhakikisha utaratibu uliotumika kufanya uhakiki wa vyuo na programu na kupelekea baadhi ya vyuo na programu kufungiwa utumike huohuo kuhakiki pindi vitakaporekebisha  mapungufu yaliyojitokeza awali. Aidha, amevitaka vyuo vyote vilivyofungiwa kupeleka TCU majibu ya maeneo  walioambiwa yana mapungufu  kama utaratibu unavyotaka badala ya kuyapeleka Wizarani.






Ijumaa, 21 Julai 2017

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia ampongeza Mkuu wa Wilaya ya Korogwe kwa kusimamia vizuuri ujenzi wa miundombinu ya shule


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhandisi Stella Manyanya amempongeza Mkuu wa Wilaya ya Korongwe Mhandisi Robert Gabriel kwa kuhamasisha wananchi kuchangia katika sekta ya elimu ambapo mchango huo wa wananchi umewezesha mradi wa ujenzi madarasa uliofadhiliwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia mradi wa Mradi wa lipa kulingana na matokeo kufanikiwa kwa kiwango kikubwa pamoja na ujenzi wa miundombinu mengine ya elimu inayofanywa na Halmashauri.

Mhandisi Manyanya ametoa pongezi hizo leo wilayani Korongwe Mkoani Tanga katika wakati wa ziara yake wilayani humo yenye lengo la kukagua utekelezaji wa ujenzi na ukarabati unaofanywa na Mradi wa Lipa kwa Matokeo (P4R). Amesema Mkuu wa wilaya huyo pamoja na kamati yake wameweza kuhamasisha wananchi kuchangia katika mradi huo na kuwezesha kujengwa madarasa zaidi ya yaliyokuwa yamelengwa hapo awali kwani wananchi walichangia nguvu kazi zao, mifuko ya saruji na vifaa vinine vya ujenzi.

Naibu Waziri ametolea mfano wa ujenzi wa miundombinu ya vyoo katika shule ya Msingi Kilimani ambapo wameweza kuijenga matundu ya vyoo 12 kwa gharama ya shilingi milioni 11 wakati sehemu nyingine ambazo ameshazitembelea wameshindwa kumaliza ujenzi wa vyoo kama hvyo kwa gharama hiyo.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Korongwe Mhandisi Robert Gabriel amemueleza Naibu Waziri kuwa Halmashauri yake imejipanga kuhakikisha wanaondoa tatizo la miundombinu ya madarasa katika wilaya yake kwa kujenga madarasa 360 pamoja na ofisi za walimu 70 ndani ya kipindi cha miezi 12 kwa kutumia nguvu za wananchi.

Katika ziara hiyo Mhe Naibu Waziri alitembelea shule za Msingi Kilimani, Bagamoyo, Matondoro, Kilole, Kwasemangube, Shule ya Sekondari Semkiwa pamoja na Chuo cha Ualimu Korogwe.











Ijumaa, 14 Julai 2017

Naibu Waziri wa Elimu akagua ujenzi na Ukarabati katika shule ya Sekondari Mbweni Tete


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhandisi Stella Manyanya ameonyesha kutokuridhishwa na hatua ya Halmashauri ya Kinondoni kuhamisha fedha za ujenzi wa madarasa, mabweni na vyoo zilizokuwa zimetolewa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknlojia kupitia mradi wa lipa kwa matokeo kwa shule ya Sekondari ya Kambwangwa na kupelekwa katika Shule ya sekondari Mbweni tete bila kufuata utaratibu wa kuitaarifu wizara iliyotoa fedha hizo.

Mhandisi Manyanya ameyaeleza hayo leo Jijini Dar es Salaam wakati wa ziara yake ya kuzitembelea shule mbalimbali kwa lengo la kukagua utekelezaji wa ujenzi na ukarabati unaofanywa na Mradi wa Lipa kwa Matokeo (P4R). Amesema kuhamishwa kwa mradi si tatizo lakini kuhamisha bila kutoa taarifa ndo tatizo lilipo kwani wizara imetoa fedha nyingi kwa ajili ya ujenzi huo hivyo ni lazima kufanya ufatiliaji ili kuweza kujirizisha kama ujenzi unafanyika lakini wakati najiandaa kwenda Kambagwa ndipo alipotaarifa kuhusu kuhamishwa kwa  mradi huo.

“Leo wakati tunataka kuanza kwenda kuangalia ujenzi ulipofikia lakini tukapewa taarifa kuwa mradi huo haupo Kambangwa na ulihamishwa kupelekwa eneo jingine, hivyo ni muhimu kupeana taarifa maana kuhamishwa kwa mradi kunaleta hoja za ukaguzi” alisisitiza Mhandisi Manyanya.

Naibu Waziri amesema ujenzi wa miundombinu hiyo katika Halmashauri mbali mbali imekuja baada ya wizara ya Elimu kwa kushirikiana na TAMISEMI uwepo wa umuhimu wa kuongeza  miundombinu ya madarasa, mabweni na vyoo katika baadhi ya shule ili kuongeza idadi ya wanafunzi  wanaodahili kwa ajili ya kujiunga na masomo ya kidato cha tano. Amesma lengo la serikali ni kuona wanafunzi wote waliofaulu wanapata nafasi ya kuendelea na masomo yao ya kidato cha tano bila mmoja kuachwa.