Ijumaa, 19 Oktoba 2018

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA
MINISTRY OF EDUCATION, SCIENCE AND TECHNOLOGY

COMMONWEALTH SCHOLARSHIPS TENABLE IN THE UNITED KINGDOM 2019

The Ministry of Education, Science and Technology as a Nominating Agent in the county for the Commonwealth Scholarships is inviting applications from qualified Tanzanians for Master’s and Doctoral degree tenable in the United Kingdom academic year for 2019.

The Scholarship includes:-
·        One year taught Master degrees.
·        Doctoral degree of up to three years duration.

Qualification

(i)               Applicants must be holders of Bachelor or Master’s degrees
(ii)             Applicants for Master’s degree must have a Bachelor degree with a GPA of not less than 3.5
(iii)          Applicants for PhD must have a Master’s degree with a GPA of not less than 4.0

Mode of Application

·        All applications should be made directly to the Commonwealth Secretariat and should be online using the following link http://cscuk.dfid.gov.uk/apply/applicants.

·        It is important that applicants should read and understand all instructions when filing the application forms, and all applicants must attach all the required attachments such as certified copies of academic certificates, transcript, birth certificates  and submit them online through the above link;

·        All applicants must ensure that, their referees submit reference letter on time;

·        Applicants who are employees must attach letters from their employers confirming that, if granted scholarships will be allowed to utilize these opportunities;
·        In order to be nominated all applicants must submit the filled application forms accompanied with the attached certified photocopies of academic certificates, transcript, birth certificates to the address below before 19th December, 2018

Permanent Secretary,
Ministry of Education, Science and Technology,
College of Business and Law,
University of Dodoma,
Block 10,
P.O. Box 10,
Dodoma.





Jumatano, 17 Oktoba 2018

BARAZA LA TAIFA LA ELIMU YA UFUNDI (NACTE) LATAKIWA KUHUISHA MITAALA ILI IENDANE NA SOKO LA AJIRA


Serikali imelitaka Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) kuhakikisha Vyuo inavyovisimamia vinahuisha mitaala yake kila baada ya miaka mitatu kwa mujibu wa sheria ili kile kinachofundishwa kiweze kuendana na mahitaji halisi ya soko kwa sasa ikiwa ni pamoja na mabadiliko ya sayansi na Teknolojia.

Kauli hiyo ya Serikali imetolewa  na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha jijini Dar Es Salaam alipofanya ziara katika Taasisi hiyo ikiwa ni utaratibu aliojiwekea wa kutembelea Taasisi zilizo chini ya Wizara na kuona namna wanavyotekeleza majukumu yao.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akizungumza na watumishi wa Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi NACTE (hawapo pichani) alipofanya ziara katika Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam kuona namna wanavyotekeleza majukumu yao.

Ole Nasha alisema ufundi ni taaluma ambayo inabadilika kila siku hivyo ni vyema mitaala ikahuishwa ili kozi zinazotolewa ziendana na ushindani wa soko la ajira. 

Pia Naibu Waziri Ole Nasha amelitaka Baraza hilo kuendelea kufanya ukaguzi wa vyuo vyake na kuvifutia usajili vyuo vyote ambavyo havifuati sheria, kanuni na taratibu ikiwa ni pamoja na kuvichukulia hatua vinavyoendelea kufanya makosa kwa mujibu wa sheria.

“Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) tangu mwaka 2016 imefungia vyuo 74 ambavyo havifuati taratibu wakati mwaka huu vyuo 3 vimefungiwa huku vingine 21 vikizuiliwa kutoa baadhi ya kozi hii ni kutokana na dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Tano iliyo nayo ya kuhakikisha Elimu itolewayo ni bora na sio bora Elimu” aliongeza Naibu Waziri Ole Nasha.
Watumishi wa Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) wakifuatilia hotuba ya Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha alipofanya ziara katika Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es salaam

Katika hatua nyingine ameipongeza NACTE kwa kusimamia vizuri udahili wa wanafunzi kwa mwaka huu ikiwa ni pamoja na kutengeneza mifumo 14 ya TEHAMA ambayo imesaidia zoezi la udahili kufanyika kwa ufanisi hatua iliyopelekea kuongeza idadi ya wanafunzi elfu kumi zaidi kutoka ile ya mwaka jana ambayo walidahili wanafunzi 110,000.

Amesema Serikali ya Awamu ya Tano ni Serikali ambayo imejipambanua katika kufikia uchumi wa kati na wa Viwanda ambao ili uweze kufanikiwa uanahitaji mafundi waliosoma vizuri, hivyo elimu ya ufundi ni moja ya vipaumbele vya Serikali na kuzitaka Mamlaka hizo kusimamia elimu itolewayo ili tolewe kama inavyostahili.

Naibu Waziri amehitimisha ziara yake ya siku moja jijini Dar es Salaam kwa kutembelea Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi stadi VETA ambapo amewataka kuandaa vijana ambao ni mahiri na wabobezi katika fani mbalimbali watakaofanya kazi katika viwanda ili kujenga uchumi wa viwanda.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akiwa katika picha ya pamoja na viongozi pamoja na watumishi wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi VETA Makao makuu jijini Dar es Salaam.

Jumapili, 14 Oktoba 2018

NAIBU WAZIRI OLE NASHA AWATAKA WAHITIMU FEZA KUEPUKA VITENDO VIOVU


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha amewataka wahitimu wa darasa la saba katika shule ya Msingi Feza kuepuka vitendo viovu ambavyo vinaweza kukatisha ndoto zao katika maisha.

Ole Nasha ametoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam katika mahafali ya 15 ya darasa la saba ya shule hiyo na kuwataka vijana hao kutambua kuwa kuhitimu katika hatua hiyo ndio mwanzo wa safari ndefu waliyonayo katika Elimu na kuwa nidhamu pekee ndio msingi wa mafanikio.

“Jamii yetu kwa sasa inakabiliwa na mmomonyoko wa maadili vitendo viovu kama vile vijana kujishirikisha katika masuala ya ngono, ulevi, matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii jihadharini navyo sana katika maisha yenu, mkijiingiza tu mtaharibu ndoto zenu mlizojiwekea na matokeo yake mtashindwa kushiriki katika jitihada za kuijenga nchi yenu,” alisisitiza Naibu Waziri Ole Nasha


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akihutubia wakati wa mahafali ya kumaliza Elimu ya Msingi Feza yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam. Amewataka wahitimu kuwa na nidhamu, bidii na kutanguliza uzalendo katika yale watakayokuwa wakifanya ili kuweza kufikia malengo yao.

Alisema Serikali inatambua na kuthamini mchango mkubwa wa Sekta binasfi katika maendeleo ya Elimu nchini kwa kuwaandaa vijana kimaadili na kitaaluma ili kufikia dira ya Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 inayolenga kuwa na mtanzania aliyeelimika na mwenye maarifa, stadi, umahiri, uwezo na mitizamo chanya ili kuweza kuchangia katika kuleta maendeleo ya Taifa.

“Mtaona Serikali sasa imefuta tozo na kodi ambazo zilikuwa ni kero kwa wamiliki wa Shule binafsi kama vile Tozo ya Uendelezaji Ujuzi (Skills Development Levy-SDL), Tozo ya Zimamoto, Kodi ya Mabango na Tozo ya Usalama Mahali pa Kazi (Occupational Safety and Health Administration-OSHA) hii yote ni kuthamini mchango mkubwa ambao mmekuwa mkiutoa katika kuelimisha vijana wa Taifa hili,” aliongeza Naibu Waziri Ole Nasha.


Wahitimu wa darasa la saba katika shule ya msingi Feza wakifuatilia hotuba ya Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha wakati wa mahafali yao yaliyofanyika oktoba 13, 2018 jijini Dar es salaam.

Hata hivyo amewataka wamiliki wote wa shule nchini kutambua kuwa pamoja na shule kuwa zao wanatakiwa kufuata taratibu, sheria na kanuni katika uendeshaji wa shule hizo kwa ni bado elimu itolewayo ni mali ya umma na watoto ni wa kitanzania.

Naye Mkurugenzi wa Shule za Feza Ibrahimu Yunus anasema kwa sasa shule hiyo ya Msingi ina jumla ya wanafunzi 770 ambapo wanaohitimu darasa la saba mwaka huu ni jumla ya wanafunzi 75 huku shule hiyo ikijivunia kufanya vizuri kwenye masuala ya Elimu katika ngazi zote zinazotolewa shuleni hapo.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akigawa cheti kwa mmoja wa wanafunzi aliyehitimu darasa la saba mwaka huu katika shule ya Msingi Feza wakati wa mahafali yao yaliyofanyika jijini Dar es Salaam Oktoba 13, 2018


MILIONI 40 ZIMECHANGWA ILI KUJENGA MABWENI YA WASICHANA


WAZIRI NDALICHAKO AENDELEA KUSISITIZA KUWA ELIMU MSINGI NI MIAKA 7
Zaidi ya kiasi cha shilingi Milioni 40 zimechangwa na wadau wa Elimu na wananchi mbalimbali wa Wilaya ya Pangani kwa ajili ya kuchangia ujenzi wa mabweni ya wasichana wa kidato cha tano na sita katika shule Sekondari Mwera mkoani Tanga.

Fedha hizo zimekusanywa mara baada ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako kuongoza harambee hiyo wakati wa kongamano la wadau wa Elimu lililoandaliwa na mbunge wa jimbo hilo, ambaye pia ni Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji Juma Aweso.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akimkabidhi Mbunge wa Pangani na Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji Juma Aweso kiasi cha Tsh. Milioni 3 kwa ajili ya kuchangia ujenzi wa mabweni ya wasichana  katika Shule ya Sekondari Mwera iiyopo Wilayni Pangani mkoani Tanga

Kupitia kongamano hilo la Elimu Waziri Ndalichako ameendelea kuwasisitiza wananchi kuwa muda wa elimu ya Msingi ni miaka 7 na kuwa sheria hiyo haijafanyiwa marekebisho, hivyo hata kama wanafunzi wanaosoma mtaala mpya hivi sasa watasoma kwa miaka saba na kuwa suala hilo ni la kisheria.

“Pamoja na kuwepo mtaala mpya bado elimu msingi ni miaka 7 na kuwa suala hilo lipo kisheria hivyo kama kutakuwa  na mabadiliko yoyote Serikali itashirikisha  wadau katika kutoa maoni na mwisho wa siku wadau watapata taarifa kamili, hata hivyo  serikali mkakati wake hivi  sasa ni wa kuhakikisha ina boresha miundombinu ya kujifunzia na kufundishia,”alisisitiza Waziri Ndalichako.

Waziri Ndalichako pia amezitaka kamati za shule kuhakikisha zinasimamia taaluma pamoja na kuhoji kuhusu matokeo ya elimu ambayo hayaridhishi lakini pia ushirikiano wa pamoja lazima uwepo ili kuhakikisha wanafunzi wanafanya vizuri kwenye taaluma Wilayani humo.

“ Mtumieni Mheshimiwa mbunge Juma Aweso awe ni mfano wenu wa kuiga, amekuwa akijitolea mfano kuwa mama yake alikuwa mama ntilie, lakini amezingatia sana elimu na hiyo ndiyo imemkomboa ndiyo maana leo hii ameweza  kuwa mbunge wa jimbo la Pangani na pia ni Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji, yote hii ni kwa sababu amesoma, amesisitiza Ndalichako.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza wakati wa Harambee ya kuchangia fedha kwa ajili ya ujenzi wa mabweni ya wasichana kwenye shule y sekondari Mwera, ambapo zaidi ya Milioni 40 zilikusanywa katika harambee hiyo Wilayani Pangani mkoani Tanga.

Akizungumza na wananchi katika kongamano hilo la Elimu Mkuu wa Wilaya ya Pangani Zainab Abdallah alisema kuwa familia  nyingi Wilayani humo zina maisha magumu hivyo ni vyema Wilaya hiyo ikawa na  michepuo ya kidato cha tano na sita ili wanafunzi wanaoofaulu wabaki hapo hapo kuendelea na masomo badala ya wazazi kuanza kuingia gharama za kuwapeleka kwenye shule za mbali.

“Mheshimiwa Waziri Wilaya yetu ina shule moja tu yenye kidato cha tano na sita, sasa tumejiwekea malengo angalau tuwe na shule 3 tofauti ili wanafunzi waendelee kusoma hapa hapa pia tunahitaji Chuo cha Ufundi kwa lengo la kuwajengea uwezo wanafunzi wetu waweze kujiajiri,” alisisitiza Mkuu huyo wa Wilaya.

Naye Mbunge wa Jimbo hilo ambaye pia ni Naibu Waziri wa Majina Umwagiliaji Juma Aweso amesema Wilaya hiyo ilichelewa sana kuwekeza kwenye Elimu na hivyo amewataka wanapangani kubadilika na kuwa elimu pekee ndiyo Mkombozi wao.

“Kupitia Elimu, mtoto wa mama ntilie anaweza kuwa Mkemia, Profesa, Mhandisi, Daktari bingwa, kiongozi, hivyo elimu pekee ndiyo silaha ya kuifanya Jamii yoyote iweze kuwa na Maendeleo,”alisema Aweso.
Viongozi wa Wilaya ya Pangani akiwemo Mkuu wa Wilaya hiyo Zainab Abdallah, Mbunge wa jimbo hilo ambaye pia ni Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji Juma Aweso wakiwa na Waziri Ndalichako wakati wa kukagu Miundombinu ya vyumba vya madarsa katika shule ya sekondari Mwera iliyopo Wilayani humo.


Ijumaa, 12 Oktoba 2018

PROF. MDOE: MAAFISA MIKOPO MSIWE CHANZO CHA MIGOGORO KWA WANAFUNZI ELIMU YA JUU


Maafisa wanaosimamia madawati ya mikopo vyuoni wametakiwa kutokuwa chanzo cha migogoro ili kuhakikisha wanafunzi wanapata huduma bora isiyokuwa na urasimu, kuacha umangimeza, rushwa na badala yake wahakikishe wanaimarisha madawati yao ili kuhakikisha wanafunzi wenye sifa na uhitaji   wananufaika na mikopo kama ilivyokusudiwa na Serikali.

Agizo hilo limetolewa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa James Mdoe wakati akizungumza katika kikao kazi cha siku mbili cha maafisa hao kilichoanza leo mjini Bagamoyo mkoani Pwani na kusisitiza kuwa dhamira ya Serikali ya awamu ya Tano ni kuhakikisha watanzania wengi wanapata Elimu ya juu.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. James Mdoe aliyekaa katikati akizungumza na maafisa wanaosimamia madawati ya mikopo kwenye Taasisi za Elimu nchini, (hawapo pichani),wakati wa kikao Kazi kinachofanyika Wilayani Bagamoyo mkoani Pwani

Profesa Mdoe amesema kwa mwaka wa fedha 2018/19 serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 427. 5 ambapo jumla ya wanafunzi 124 watanufaika na mkopo huo, na kuwa ugawaji wa mikopo hiyo uzingatie haki, vigezo, kanuni na sheria.

“Nataka twende vizuri tukahakikishe huduma bora inatolewa katika mwaka huu mpya wa masomo ikiwa ni pamoja na kutoa huduma bora, kusimamia kumbukumbuku na kuhakikisha mawasiliano ya mara kwa mara yanakuwepo kati ya maafisa mikopo na bodi ya mikopo na kwamba haipendezi maafisa mikopo kuwa chanzo cha migogoro,” amesisitiza Profesa Mdoe.

Profesa Mdoe pia ameitaka bodi hiyo kuimarisha mifumo ya TEHAMA ili kuboresha utendaji kazi, ikiwa ni pamoja na kuongeza kasi ya kuwasaka waajiri  warejeshe fedha ambazo wafanyakazi wao walisoma kwa mkopo, ili fedha hizo zitumike kwa wanafunzi wengine.
Maafisa mikopo wanaosimamia madawati ya mikopo katika Taasisi za Elimu ya juu hapa nchi wakiwa katika kikao kazi mjini Bagamoyo mkoani Pwani kwa lengo la kujitathmini na  kujengeana uwezo wa namna  bora ya kuboresha utendaji Kazi zao.

Akizungumza katika kikao kazi hicho Mkurugenzi Mtendaji wa bodi ya mikopo Abdul- Razq badru amesema kuwa maagizo yote yaliyolewa na Naibu Katibu Mkuu watayasimamia katika utekelezaji wa ugawaji wa mikopo kwa wnanafunzi huku akikiri kuongezeka kwa idadi ya wanufaika wa mikopo hiyo inayotolewa na serikali.

“Bodi ya mikopo inaahidi kusimamia haki, vigezo, kanuni na sheria katika utoaji wa mikopo hiyo kwa wanafunzi kama ambavyo sheria zinavyoelekeza, niwasihi sana maafisa mikopo kufanya kazi kwa weledi na kuacha mazoea ili kuondoa migogoro inayoweza kujitokeza,” alisisitiza Badru
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya mikopo ya wanafunzi wa Elimu ya juu Abdul-razaq Badru akizungumza na maafisa mikopo wakati wa kikao kazi cha siku mbili kinachofanyika wilayani Bagamoyo mkoani Pwani.


NAIBU WAZIRI OLE NASHA ATOA MIEZI MITATU KWA HALMASHAURI YA MBULU KUKAMILISHA MIRADI YA ELIMU


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha ameiagiza Halmashauri ya Mji wa Mbulu, mkoani Manyara kuhakikisha inatafuta fedha za kukamilisha miradi ya elimu inayosimamiwa na Wilaya hiyo katika kipindi cha miezi mitatu.

Ole Nasha ametoa agizo hilo baada ya kutembelea na kukagua miradi hiyo na kukuta haijakamilika kutokana na halamashauri hiyo kukosa fedha za kukamilisha hali iliyosababishwa na kutofuata maelekezo ya mradi huku wakipanga kuchangisha wazazi wa wanafunzi wanaosoma katika shule hiyo ili kukamilisha miradi hiyo.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akikagua moja ya bweni linalojengwa na Wizara kupitia fedha za EP4R katika Shule ya Sekondari ya Chief Sarwatt iliyoko katika Halmashauri ya Mji wa Mbulu mkoani Manyara

Naibu Waziri ametaja miradi hiyo kuwa ni pamoja na ule wa ujenzi wa mabweni, madarasa na matundu ya vyoo ndio ambayo inatekelezwa katika shule ya Sekondari Chief Sarwatt iliyopo katika kata ya Endagikot Mkoani humo na kutaka ikamilike bila kuhusisha wanafunzi ama wazazi wao.

 “Suala kuchangisha wanafunzi liko wazi kwa kila mtu, Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli amekataza suala la kuchangisha mwanafunzi au mzazi wa mwanafunzi yeyote eti kwa kuwa mwanafunzi anasoma katika shule fulani, suala la michango linatakiwa kuhusisha jamii nzima bila kujali huyu ni mzazi wa mwanafunzi ama la na linafanyika kupitia ofisi ya Mkurugenzi na si walimu na katika hili mlipaswa kuishirikisha jamii kabla ya kuanza ujenzi,” alisisitiza Naibu Waziri Ole Nasha.

Naibu Waziri Ole Nasha alisema Wizara ya Elimu ilitoa fedha kiasi cha Shilingi milioni 215,500,000 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni 2 ya Wanafunzi, vyumba vitatu vya madarasa na matundu matano ya vyoo na kupaswa kutekelezwa kulingana na maelekezo, lakini halmshauri ilikuja na mpango mwingine wenye makisio tofauti na yale ya Wizara.

“kama mliona kuna chanagamoto mlipaswa kushirikisha Wizara kabla ya kufanya maamuzi mliyofanya ingesaidia kuondokana na kasoro ambazo zinaonekana sasa, na hiki si kitu kipya zipo Halmashauri zinapekelewa fedha kwa ajili ya Hosteli lakini wanaiomba Wizara kubadilishiwa kulingana na uhitaji walionao kwa wakati ule mngefanya hivyo kabla ya kuanza ujenzi ili kupata maelekezo,” aliongeza Naibu Waziri Ole Nasha.
Muonekano wa hatua iliyofikiwa ya ujenzi wa bweni katika shule ya sekondari ya Chief Sarwatt iliyoko katika halmashauri ya mji wa Mbulu mkoani Manyara

Nae Mwenyekiti wa Bodi ya shule ya Chief Sarwatt Emmanuel Tangao alisema walifikia hatua ya kuanza ujenzi bila kuwashirikisha wananchi kwa kuwa walikuwa wakikimbizana na tamko la Serikali kwamba mwaka huu walipaswa kupokea wanafunzi wa kidato cha tano, lakini pia watakapoishia wangejua ni kiasi gani cha fedha kilichohitajika kukamilisha ujenzi ndipo wachangishe.

Naibu Waziri Ole Nasha amekamilisha ziara yake ya kikazi mkoani Manyara ya kukagua uboreshaji wa miundombinu ya kujifunzia na kufundishia inayotekelezwa katika Halmashauri za Babati, Hanang, Mbulu na Mbulu, pia alitembelea na kukagua Shule ya Sekondari Gehandu, Chuo cha Maendeleo ya Wananchi.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akipata maelezo wa kile wanachojifunza kutoka kwa mwanafunzi anayechukua kozi ya huduma za mifugo katika Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Tango kilichopo Halmashauri ya mji wa Mbulu Mkoani Manyara.

Jumatano, 10 Oktoba 2018

WATUMISHI WANNE NA MWENYEKITI WA BODI YA SHULE WASWEKWA NDANI KWA MATUMIZI MABAYA YA FEDHA ZA MIRADI


Naibu waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Willam Ole Nasha amemuagiza mkuu wa Wilaya ya Mbulu Chelestine Mofuga kuwachukulia hatua za kisheria wale wote waliohusika kubadilisha matumizi ya fedha za miradi ya Shule ya Sekondari Tumatu iliyoko Wilayani Mbulu Mkoni Manyara.

Mheshimiwa Ole Nasha ametoa agizo hilo wakati akikagua ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya Elimu mkoani humo na kukuta fedha zilizotolewa na Wizara ya Elimu kiasi cha sh milioni 141, 600,000 kwa ajili ya ujenzi wa majengo mapya ya madarasa, bweni na vyoo zimetumika kukamilisha jengo la bweni na maktaba ambavyo vilijengwa kwa nguvu za wananchi.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akikagua ujenzi wa bweni katika Shule ya Sekondari Tumatu wilayani Mbulu Mkoani Manyara

Naibu Waziri Ole Nasha amesema shule hiyo ilipatiwa kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya Ujenzi wa bweni moja la wanafunzi, madarasa 3 na matundu ya vyoo 6 lakini fedha hizo hazikuelekezwa kwenye kile kilichokusudiwa badala yake zimetumika kukamilisha majengo ambayo tayari wananchi walianza kujenga kwa gharama ambazo hazina uhalisia.

 "Hapa kuna harufu ya ubadhirifu wa fedha za umma haiwezekani gharama za kumalizia majengo ambayo tayari wananchi wameanza kujenga na kukaribia kukamilika kutumia fedha za kujenga majengo mapya, kujua hili haiitaji mtu kuwa mhandisi ni mahesabu ya kawaida tu, hatua zichukuliwe dhidi ya waliohusika.” Aliongeza Naibu Waziri Ole Nasha
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akitoa maelekezo kwa Viongozi na watendaji wa Halmashauri ya Mbulu kuhusu ujenzi wa bweni la Wasichana uliofanyika  katika Shule ya Sekondari Tumatu iliyoko katika Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara. 

Naibu Waziri Ole Nasha amesema   Serikali ya Awamu ya Tano ya Mhe. Dk. John Pombe Magufuli inatoa kipaumbaele kwenye Sekta ya Elimu na ndio maana kila mahali kuna miradi ya Elimu hivyo fedha za miradi zitumike vizuri na kwamba haitasita kuchukua hatua dhidi ya mtu yeyote atakaebanika anafanya ubadhirifu wa fedha za miradi hiyo.

Kufuatia agizo hilo Mkuu wa Wilaya hiyo amewaweka chini ya ulinzi kwa saa 48 wafanyakazi hao ambao ni Afisa Elimu Sekondari wa Wilaya ya Mbulu Ludovic Longino, Fundi Sanifu (Civil tehnician) wa Halmashauri Moses Nguvava, Mwenyekiti wa Bodi ya Shule Bryson Panga, Mkuu wa shule hiyo Killian John na Afisa Ugavi Faustine Safari kutokana na tuhuma hizo na kuagiza TAKUKURU kuanza uchunguzi mara moja.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akiongea na wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Yaeda Ampa pamoja na wanakijiji wa eneo hilo ambapo kwa pamoja amewataka kuunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Tano anazozifanya katika kuboresha Sekta ya Elimu.