Jumanne, 11 Februari 2020

Kongamano la Kimataifa la kuunganisha wanataaluma na wadau wa sekta ya Utalii na Ukarimu

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akiongea wakati wa kufunga Kongamano la Kimataifa la kuunganisha wanataaluma na wadau wa sekta ya utaliina ukarimu liliofanyika Jijini Dar es Salaam.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha amesema taasisi za mafunzo na wadau wa sekta ya utalii wanahitajika kufanya kazi kwa pamoja ili kutatua changamto zilizopo ikiwemo nguvu kazi yenye weledi na ufanisi wa kutosha  katika tasnia hiyo.

Naibu Waziri Ole Nasha ameyasema hayo Jijini Dar es Salaam wakati wa kufunga Kongamano la Kimataifa la kuunganisha wanataaluma na wadau wa sekta ya Utalii na Ukarimu ambapo amesema ushindani katika soko ni mkubwa hivyo kunahitajika maandalizi mazuri ya rasilimali watu ili kuweza kushindana katika soko la dunia.



Mmoja wa washiriki wa   Kongamano la Kimataifa la kuunganisha wanataaluma na wadau wa sekta ya utalii akipokea cheti cha ushiriki kutoka kwa Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha wakati wa kufunga kongamano hilo Jijini Dar es Salaam.

Amesema Utalii ni moja ya Sekta inayolipatia  Taifa  fedha za kigeni akitolea mfano mwaka jana 2019 nchi ilipata fedha za kigeni dola  milioni 2.4 kutokana na utalii hivyo kukiwa na nguvu kazi yenye weledi na ufanisi wa kutosha nchi itaneemeka kupitia utalii.

“Hakika tunahitaji kuandaa vizuri rasilimali watu, nchi jirani zimepiga hatua kwenye kuvutia watalii sio kwamba wana vivutio vingi kuliko sisi ni kutokana na  pamoja na mambo mengine kuwa na nguvu kazi yenye weledi ndio maana kama Taifa tunawekeza katika kutayarisha vijana ili kuwa na nguvu kazi yenye weledi katika sekta ya utalii," amesema Naibu Waziri Ole Nasha.
Mmoja wa washiriki wa kongamano  la Kimataifa la kuunganisha wanataaluma na wadau wa sekta ya utalii  na Ukarimu Zera Mwanga kutoka Chuo cha Taifa cha Utalii cha Jijini Dar es Salaam akionesha cheti cha ushiriki mara baada ya kukabidhiwa.
Kiongozi huyo aliongeza kuwa kwa sasa Taifa letu linatoa kipaumbele katika kuimarisha viwanda ili kuleta mabadiliko ya kiuchumi ikiwa ni pamoja na kuandaa nguvu kazi, hivyo ni vizuri kukawa na mfumo wa mafunzo pacha kati ya Taasisi za mafunzo na wamiliki wa viwanda.

“Ninawiwa kusema kuwa kongamano hili limekuja kwa wakati muafaka sana na Wizara yangu itayachukua kwa uzito mapendekezo yote yaliyotolewa ukizingatia kuwa kuimarisha muunganiko kati ya wanatasnia na wanataaluma ni moja ya vipaumbele katika wizara yangu ili kuhakikisha tunazalisha wahitimu bora wanaokidhi mahitaji ya soko,” aliongeza Naibu Waziri Ole Nasha. 

Naibu Waziri Ole Nasha amekipongeza chuo cha Taifa cha Utalii na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa kuandaa mkutano wa kuwaunganisha wakufunzi na watoe huduma hiyo walio katika biashara ya Utalii kwani kwa pamoja wanaweza kutatua changamoto zilizopo.

Naye Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Utalii, Dkt. Shogo Mlozi amesema kwa kushirikiana na vyuo vingine vinavyotoa mafunzo ya utalii wataendelea kuimarisha mpango wa utoaji mafunzo  kwa kufanya kazi karibu na watoa huduma ili kupata nguvu kazi yenye weledi na ujuzi. 
Baadhi washiriki wa kongamano  la Kimataifa la kuunganisha wanataalumana wadau wa sekta ya Utalii na Ukarimu wakifuatlia hotuba ya Naibu Waziri wa Elimi, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha wakati wa kufunga kongamano hilo jijini Dar es Salaam
Kwa upande wake mshiriki wa kongamano hilo kutoka VETA makao makuu,  Happiness Salema amesema ni vizuri kukawa na makongamano ya aina hii kwa kuwa yanawaleta pamoja watoa mafunzo na wamiliki wa viwanda, jambo ambalo linasaidia kuona changamoto zilizopo na kuweka mkakati kwani nchi zilizoendelea zinatumia mfumo huu katika kutoa mafunzo.

"Soko la hotelia na utalii liwe tayari kupokea mfumo wa mafunzo pacha hali kadhalika kuwa tayari kutoa nafasi kwa ajili ya walimu kupata ujuzi kwani kwa kufanya hivyo nchi itakuwa ya kwanza kuongoza kwenye sekta ya utalii na ukarimu," amesema Salema.

Kongamano la kimataifa la kuunganisha sekta ya Utalii na Ukarimu katika nchi zinazoendelea limefanyika kwa siku mbili Jijini Dar es Salaam na limewakutanisha  wadau  na wanataaluma katika sekta ya Utalii na Ukarimu kutoka nchi zinazoendelea.

WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA KUJENGA KUJENGA BWALO KATIKA SHULE YA MRISHO GAMBO ILIYOPO MKOANI ARUSHA



Akizungumza mara baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa shule hiyo, Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Leonard Akwilapo  amesema Wizara itajenga bwalo la chakula ili kuwezesha wanafunzi wa shule hiyo kuwa na sehemu nzuri na salama ya kupatia chakula watakapokuwa wakiishi katika mabweni yatakayojengwa na wizara.

"Nimeambiwa wanafunzi wa shule hii wanatoka maeneo ya mbali, Wizara ilishaahidi kujenga mabweni mawili sasa tutajenga na bwalo," amesema Dkt. Akwilapo.

 Aidha, Dkt. Akwilapo amesema  serikali ina wajibu wa kuhakikisha wanafunzi wanasoma  katika
 mazingira salama na yenye miundombinu salama.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo amesema shule hiyo imejengwa baada ya kupokea maombi kutoka kwa  wakazi wa Olasite baada shule yao kuzidiwa na wingi wa wanafunzi.

"Baada ya kupokea maombi kutoka kwa wakazi wa hapa  na kuona kweli kuna shida katika shule hii ya Olasite ndipo tukaanza kutafuta wadau mbalimbali ambao walijitokeza na kusaidia uanzishwaji wa ujenzi wa shule hiyo," amesema Gambo.

Mkuu wa shule hiyo, Fedelis Michael amesema mazingira ya wanafunzi kusoma mbali sana na shule ni changamoto kwao kwani njiani wanakutana na mambo mengi ambayo yanaweza kuwasababishia kushindwa kusoma vizuri.

Jumatatu, 10 Februari 2020

CANADA YATOA ZAIDI YA BILIONI 90 KWA AJILI YA KUBORESHA ELIMU YA UALIMU

Serikali ya Canada imetoa zaidi ya bilioni 90 kwa Tanzania zitakazotumika kuboresha elimu ya ualimu nchini.

Hayo yamesemwa Jijini Arusha na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo  wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kupitia na kutathmini utekelezaji wa Mradi wa Kuendeleza Elimu nchini (TESP) ambapo amesema mradi huo pia umewezesha kuinua kiwango cha ubora wa elimu katika shule za msingi na sekondari kwa kuzalisha rasilimali watu yenye ubora.
.
Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo akizungumza na wadau wa Elimu ya Ualimu (hawapo pichani) wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kupitia na kutathimini Mradi wa Kuendeleza Elimu ya Ualimu (TESP) Jijini Arusha
Dkt. Akwilapo amesema Canada kupitia TESP imetoa fedha hizo ambazo zimetumika katika kuvijenga upya baadhi ya vyuo vya ualimu, kuboresha miundombinu ya kufundishia na kujifunzia  pamoja na kutoa mafunzo kazini kwa  walimu.

Kansela Mkuu, Ushirikiano na Maendeleo kutoka Canada Gwen Walmsely akizungumza na wadau wa Elimu ya Ualimu jijini Arusha
Kiongozi huyo amesema kuwa Ushirikiano wa Tanzania na Canada unalenga kuongeza uwezo wa vyuo vya ualimu kufundisha walimu waliobobea watakaofundisha vizuri katika shule mbalimbali.

“Tunatoa shukrani nyingi sana kwa serikali ya Canada na Kitengo chao cha Global Affairs ambacho kinasimamia mradi huu, mafanikio makubwa yamepatikana kupitia mradi huu na matokeo yameshaanza kuonekana," amesisitiza Katibu Mkuu Akwilapo.

Dkt. Akwilapo amesema mafanikio  ya mradi huo yameanza kuonekana ambapo walimu wameongeza uwezo katika ufundishaji na matumizi ya TEHAMA katika kufundisha.

Kansela Mkuu, Ushirikiano na Maendeleo ​kutoka Canada Gwen Walmsley amesema kuwa Canada itaendelea kutoa fedha zaidi katika kuboresha sekta ya elimu nchini na mradi huo ni moja kati ya juhudi wanazozifanya katika kuunga mkono serikali ya Tanzania katika jitihada za  kuboresha elimu.

Gwen ameipongeza Tanzania kwa kufanya Sekta ya Elimu kipaumbele ili  kuhakikisha watoto wote wanapata elimu, suala ambalo limewezesha zaidi ya watoto milioni 10.6 kujiunga na elimu ya msingi na sekondari

Mratibu wa Mradi wa kuendeleza Elimu​ ya Ualimu TESP kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Ignas Chonya amesema kuwa mradi huo umewawezesha walimu kuboresha mbinu za ufundishaji kupitia Tehama ambapo vyuo 35 vya ualimu vimeanganishwa na mfumo huo na wanatarajia kuunganishwa na mkongo wa Taifa.

Jumamosi, 8 Februari 2020

MKUTANO WA WATUMISHI WA WIZARA WALIOKO MAKAO MAKUU


Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Leonard Akwilapo amesema utumishi wa umma una sheria, kanuni, taratibu, maadili na miiko ya kiutendaji ambayo kila mtumishi anapaswa kuielewa na kuzingatia katika utendaji kazi.
 
Katibu Mkuu Akwilapo amesema hayo wakati wa Mkutano  wa Wafanyakazi wa kutathmini utendaji wa Wizara katika kipindi cha miezi sita kuanzia Julai hadi Desemba 2019 ambapo amesema ni vizuri kila mtumishi akazingatia taratibu hizo ili kutekeleza majukumu yake ipasavyo.

Amesema pamoja na kuzingatia sheria hizo ni vizuri tukafanya kazi kwa kushirikiana na kuelekezana ili kupata matokeo chanya katika utekelezaji wa majukumu.

Kiongozi huyo amepongeza watumishi wa Wizara hiyo kwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo ili kufikia malengo makubwa ya Wizara ambayo ni kutoa Elimu bora nchini.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. AveMaria Semakafu amesema ni vizuri watumishi wakaendeleza kasi liyopo sasa ya utendaji huku wakizingatia utendaji wenye viwango ili sekta ya Elimu iendelee kufanya vizuri.

Akizungumza kwa niaba ya Watumishi wa Wizara Bwana Nicholaus Moshi ameupongeza Uongozi wa Wizara kwa namna unavyoweka mazingira wezeshi ya utoaji Elimu kwa  kujenga na kukarabati miundombinu ya elimu, kununua vifaa vya kufundishia na kujifunzia, kuhakikisha uwepo wa vitendea kazi pamoja na ujenzi wa ofisi zikiwemo za Wathibiti Ubora wa shule na ukarabati na upanuzi wa  Vyuo  ya Ualimu.

Alhamisi, 6 Februari 2020

SERIKALI KUJENGA SHULE ZA WANAFUNZI WENYE MAHITAJI MAALUM KILA MKOA

Serikali imesema itaendelea na mpango mkakati wa kutekeleza elimu bila malipo pamoja na kutoa vipaumbele kwa watu wenye ulemavu kupata elimu iliyo bora.

Hayo yameelezwa jijini Dar es Salaam na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Ave Maria Semakafu wakati wa ufungaji wa mafunzo ya TEHAMA na Teknolojia Saidizi kwa wakufunzi na walimu wa Sekondari wenye mahitaji maalum.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu akiongea wakati wa ufungaji wa mafunzo ya Tehama na Teknolojia Saidizi kwa Wakufunzi na Walimu wa Sekondari wenye mahitaji maalumu jijini Dar es Salaam.
Dk. Semakafu amesema  serikali imejipanga kuhakikisha walimu  na wanafunzi wanapata elimu ya Tehama, elimu jumuishi sambamba na kujenga shule zao maalum katika kila mkoa ambapo kwa sasa wameanza na mkoa wa Katavi.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu akitoa maelekezo kwa mmoja wa washiriki wa mafunzo ya Tehama na Teknolojia Saidizi OUT, jijini Dar es Salaam.
Hata hivyo awali ilielezwa kuwa tayari serikali imetumia kiasi cha shilingi bilioni 5.9 kwa ajili ya kununua na kusambaza vifaa maalum vya kielimu saidizi katika shule za msingi na sekondari zinazopokea wanafunzi wenye mahitaji maalum nchini.

“Hii kazi pia si ndogo, napenda kwa namna ya kipekee kabisa kutumia nafasi hii kuushukuru Uongozi wa Chuo Kikuu Huria kwa kukubali kuendesha mafunzo haya hapa chuoni na kutoa wawezeshaji, vifaa pamoja na miundombinu mingine kwa ajili ya kufanikisha mafunzo haya muhimu,’’ amesema Dk. Semakafu.
Mmoja wa washiriki wa mafunzo ya Tehama na Teknolojia Saidizi akiwa katika mafunzo yaliyofanyika Chuo Kikuu Huria jijini Dar es Salaam.  Kulia ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu.
Aliongeza kuwa mafunzo waliyoyapata ni muhimu kwani yatawasaidia katika matumizi ya TEHAMA kwenye  ufundishaji na ujifunzaji, kutafuta rejea mbalimbali za kielektroniki kwenye mitandao na kutumia teknolojia saidizi zinazowezesha matumizi ya TEHAMA katika ufundishaji na ujifunzaji.

Akizungumza kwa niaba ya washiriki wa mafunzo hayo, Mwalimu wa shule ya sekondari ya Binti Mussa iliyopo Kiwalani jijini Dar es Salaam, Anna Mbogo alisema wanaishukuru kwa  dhati  Wizara ya Elimu kwa kuona umuhimu wa kutoa  mafunzo kwa walimu wenye mahitaji maalum.
Baadhi ya washiriki wa mafunzo ya Tehama na Teknolojia Saidizi kwa Wakufunzi na Walimu wa sekondari wenye mahitaji maalumu wakifuatilia hotuba ya Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu (hayupo pichani)  wakati wa kufunga mafunzo hayo jijini Dar es Salaam.
“Mafunzo haya  yalilenga kutujengea uwezo sisi walimu kuendana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia ya sasa, pia tunaushukuru uongozi wa OUT chini ya serikali ya awamu ya tano kuonesha bayana nia ya kuwasaidia walimu wenye mahitaji maalum na kuwathamini watu wenye ulemavu kwa kuajiri watu wenye ulemavu,’’ amesema Mwalimu Anna.

MAKISATU 2020 KUENDELEA KUIBUA WABUNIFU

Serikali imesema inatambua umuhimu na mchango wa ubunifu na teknolojia katika kurahisisha na kuongeza ufanisi  katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kiuchumi.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma kuhusu kuanza kwa Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (MAKISATU) 2020, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha amesema  mashindano hayo ni moja ya mikakati ya Serikali ya kuibua, kutambua na kuendeleza ubunifu na ugunduzi unaofanywa na watanzania.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Mkutano mara baada ya kuzungumza na Waandishi wa habari jijini Dodoma.  Kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. Leonard Akwilapo na kulia ni Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano, Sylvia Lupembe.

"Lengo kubwa la MAKISATU pamoja na kukuza na kusaidia kubiasharisha, yanatoa fursa kwa wabunifu na wagunduzi wa teknolojia mbalimbali kujitangaza na kutangaza kwa wadau ubunifu unaozalishwa," amesisitiza Ole Nasha.
Mwakilishi wa Benki ya CRDB, Prosper Nambaya akizungumza wakati wa Mkutano wa Waandishi wa habari kuzungumzia kuanza kwa mashindano ya MAKISATU, 2020 jijini Dodoma.
Ole Nasha amesema MAKISATU inawalenga wabunifu kutoka makundi ya shule za msingi, sekondari, vyuo vya ufundi stadi, vyuo vya kati, vyuo vikuu, Taasisi za utafiti na Mfumo usio rasmi.

Baadhi ya washiriki waliohudhuria Mkutano wa kuzungumzia kuanza kwa Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknonojia na Ubunifu (MAKISATU) 2020 jijini Dodoma, wakimsikiza Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha (hayupo pichani) wakati akizungumza na Waandishi wa habari.

Aliongeza kuwa kupitia MAKISATU 2019 Serikali imewaibua na kuwatambua wabunifu wachanga zaidi ya 415 huku wabunifu 60 mahiri wakiendelezwa ili ubunifu wao ufikie hatua ya kubiasharishwa.


Kiongozi huyo ametoa wito kwa watanzania wenye ubunifu mbalimbali kushiriki katika mashindani hayo na amewashukuru Benki ya CRDB kwa kukubali kufadhili mashindano hayo.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Wateja Wakubwa kutoka CRDB, Prosper Nambaya amesema Benki hiyo imeamua kuwa na ushirikiano endelevu na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ili kusaidia kukuza ubunifu unaozalishwa nchini kutokana na kuwepo kwa watu wengi wenye mawazo ya kibunifu yanayopaswa kuendelezwa.