Jumanne, 27 Machi 2018

Wizara ya Elimu yawasilisha Taarifa ya Utekelezaji, Makadirio ya Bajeti kwa mwaka 2018/19 kwa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii.


Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imewasilisha Taarifa ya Utekelezaji kwa mwaka wa fedha 2017/18 na Makadirio ya Bajeti kwa mwaka 2018/19 kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii.

Uwasilishaji wa taarifa hiyo umefanyika leo katika ofisi za Bunge zilizopo Mkoani Dodoma ambapo wajumbe wa Kamati hiyo wamepata fursa ya kupitia na kujadili Fungu 46. 

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Pro.Joyce Ndalichako  akifafanua jambo wakati wa uwasilishaji wa Taarifa ya Utekelezaji  2017/18 na Makadirio ya Bajeti kwa Mwaka 2018/19 kwenye Kamati  ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii.


Makamu Mwenyekiti wa kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Juma Nkamia akisitiza jambo wakati wa uwasilishaji wa Taarifa ya utekelezaji na Makadirio ya Bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa mwaka 2018/19 Mkoani Dodoma.

Wajumbe wa Kamati  ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii wakifuatilia kwa makini uwasilishaji wa Taarifa ya utekelezaji na Makadirio ya Bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa mwaka 2018/19.

Alhamisi, 15 Machi 2018

Maafisa Habari wa Serikali watoa msaada kwa Shule ya Laibon


Maafisa Habari, Mawasiliano na Uhusiano wa Serikali Leo wamekabidhi msaada wa Vitabu, Madaftari, kalamu na Matanki mawili ya kuhifadhia maji katika Shule ya Msingi Laibon iliyopo mkoani ARUSHA.

Akizungumza wakati akikabidhi msaada huo Mwenyekiti wa Chama Cha Maafisa hao- TAGCO, Pascal Shelutete amesema lengo ni kuunga mkono jitihada zinazofanywa na Serikali za kutoa Elimu bure.

Kwa upande wake Mwalimu Mkuu wa shule hiyo Rashid Njarita ameshukuru kupokea msaada huo ambapo amesema matanki ya maji yataondoa changamoto ya maji iliyokuwepo shuleni hapo.

Msaada uliotolewa unathamani ya shilingi milioni mbili na laki tano.

Mwenyekiti wa Chama Cha Maafisa Habari, Mawasiliano na Uhusiano wa Serikali - TAGCO, Pascal Shelutete akimkabidhi Mwalimu Mkuu wa shule ya Msingi Laibon Rashid Njarita Madaftari kwa ajili ya wanafunzi wa shule hiyo.
Maafisa hao wa Mawasiliano wanashiriki kikao kazi ambacho kinalenga kujengeana uwezo wa namna bora ya kutangaza shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na Serikali ya awamu ya tano.


Kikao hicho kimeanza Machi 12 na kitamaliza Machi 16, 2018 huku kauli mbiu ya mkutano huo inasema Je? Mawasiliano ya kimkakati yanachagiza Vipi Tanzania ya Viwanda.

Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Habari MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali Dk. Hassan Abass akimkabidhi daftari mmoja wa wanafunzi wa shule ya Msingi Laibon iliyopo mkoani Arusha.



Ijumaa, 9 Machi 2018

Naibu Waziri Ole Nasha asisitiza uadilifu na utunzaji wa siri za ofisi.


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. William Ole Nasha amewataka watumishi wapya wa Wizara hiyo kuwa waadilifu katika utendaji kazi pamoja na kutunza siri katika maeneo wanayofanyia kazi.

Naibu Waziri Ole Nasha ametoa rai hiyo mjini Dodoma wakati wa akifunga mafunzo kwa waajiriwa wapya wa Wizara hiyo, mafunzo ambayo yamelenga kuwakumbusha taratibu, sheria na miongozo ya kazi inayotakiwa katika utumishi wa umma.

Naibu Waziri huyo amesema anaamini mafunzo yaliyotolewa yatawawezesha kuwa watumishi bora wa umma ambao wanafahamu vema mipaka ya kazi, taratibu za kiutumishi lakini pia haki na wajibu katika utendaji kazi.

Naibu Waziri wa Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia, Mhe.William Ole Nasha akifunga mafunzo ya watumishi wapya wa Wizara hiyo ambapo amewataka kuzingatia maadili ya Utumishi wa Umma,ikiwa ni pamoja na kutunza Siri za ofisi.

Pamoja na mambo mengine Naibu Waziri Ole Nasha amemuagiza Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu wa Wizara hiyo Moshi Kabengwe kuandaa utaratibu wa mafunzo kwa watumishi wengine wa Wizara hiyo ili kuwakumbusha taratibu, kanuni na miongozo kwa lengo la kuepuka ukiukaji wa maadili na pia kuleta chachu ya mabadiliko katika utendaji kazi miongoni mwa watumishi.


Nae mmoja wa watumishi aliyeshiriki mafunzo hayo Lazaro Julius kutoka Ofisi ya Kamishna wa Elimu wa Wizara hiyo amesema mafunzo hayo ni muongozo thabiti katika kutekeleza majukumu ya kazi za kila siku katika utumishi wa umma ambapo ameahidi kuzingatia na kutekeleza yote yaliyoelekezwa.

Mafunzo  kwa waajiriwa wapya wa Wizara hiyo yamefanyika kwa siku Nne kuanzia Machi 6, na yameshirikisha waajiriwa wapya kutoka wizara ya Elimu Makao Makuu na Taasisi zilizo chini ya Wizara hiyo.

Watumishi wapya wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia wakifuatilia mafunzo Maalumu ya namna wanavyotakiwa kutekeleza majukumu yao katika Utumishi wa Umma ambayo yamefanyika mkoani Dodoma.


Ole Nasha apiga  marufuku Wanafunzi wa Shule kunyimwa vyeti kwa kutokamilisha michango
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha amepiga Marufuku Wanafunzi kunyimwa vyeti pindi wanapomaliza shule kwa madai ya kutokamilisha michango pindi walipokuwa wanasoma.

 Naibu Waziri Ole Nasha ametoa agizo hilo mkoani Tabora alipokutana na Wakuu wa Shule za Msingi na Sekondari kuzungumzia namna ambavyo wanapaswa kutekeleza agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania John PombeMagufuli la kukataza michango shuleni kwa kuwa Serikali inagharamia ElimuMsingi.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mheshimiwa William Ole Nasha akikagua Vifaa vyama Maabara katika Chuo cha UalimuTabora kilichopo Manispaa ya Tabora Mkoani humo.

Naibu Waziri huyo amesema Magufuli hajakataza uchangiaji wahiari isipokuwa amekataza michango holela ambayo ilikuwa ikichangishwa bila utaratibu na kumzuia Mwanafunzi kuendelea na masomo kwa madai kuwa hajachanga mchango wa aina fulani.

 ‘Waraka wa Elimu Namba 6 wa mwaka 2016 unaeleza wazi namna Elimu bila malipo itakavyotekelezwa na nijukumu la mzazi kwa mtoto wake hivyo ni marufuku Mwanafunzi kubakizwa nyumbani au kutopewa cheti chake anapomaliza Shule kwa madai kuwa hajakamilisha mchango fulani’.amesema Ole Nasha

Pia ametoa rai kwa walimu wote nchini kujielekeza kwenye jukumu lao la msingi la kufundisha badala ya kujihusisha na uchangishaji wa mchango wa aina yoyote na kwamba michango yote ya hiari itaratibiwa na Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri husika kupitia watendaji wake.

Ndalichako awataka Wanawake kufanya kazi kwa bidii


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amewataka Wanawake nchini kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili kuonyesha Thamani ya Mwanamke katika jamii na Taifa kwa ujumla.

 Waziri Ndalichako amesema bidii pekee katika shughuli mbalimbali za kujiletea Maendeleo kwa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla ndiyo itaonyesha mchango wa Mwanamke na kumfanya athaminiwe na kumuwezesha kupata nafasi kubwa na nzuri zaidi za kutumikia Taifa ikiwa ni pamoja na kufuta dhana potofu ya kuwa Mwanamke hawezi.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Wajumbe wa Jukwaa la Akademia katika kuadhimisha siku ya Wanawake Duniani shughuli ambayo  imefanyika jijini Dar es salaam.

Waziri Ndalichako amesema hayo wakati wa maadhimisho ya siku ya Wanawake Duniani yaliyoandaliwa na  Taasisi ya Akademia ya Sayansi Tanzania walati wa Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ili kujadili mchango wa Mwanamke katika kuleta Maendeleo Endelevu ambalo limeshirikisha Wanawake na Wadau wengine kutoka nchi mbalimbali.

Kwa upande wake Spika Mstaafu Anne Makinda amesema wanawake wanapaswa kuhakikisha wanapata Elimu ambayo itawawezesha kujikwamua kiuchumi ikiwa ni pamoja na kuwa na uthubutu wa kufanya shughuli ambazo wanaamini watazifanya kwa umakini ili kuonyesha uwezo walionao katika jamii inayowazunguka.

Jumatano, 7 Machi 2018

Mloganzila yapokea msaada wa Dawa


Serikali ya Korea leo imeikabidhi  msaada wa dawa  zenye thamani ya Shilingi Milioni Mia Moja kwa Serikali ya Tanzania ikiwa ni ishara ya mahusiano mazuri kati ya nchi hizo mbili.
Msaada huo umekabidhiwa kwa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia  Profesa Joyce Ndalichako jijini Dar es Salaam ili zitumike katika Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi ya Tiba Muhimbili (MUHAS) Kampasi ya Mloganzila.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akiwa pamoja na Wajumbe wa Kamati za Bunge la Jamhuri ya Watu wa Korea wakisalimiana  na Wagonjwa katika Hospitali ya Taaluma na Tiba ya Mlongazila jijini Dar es Salaam mara baada ya Korea kutoa msaada wa  kwa ajili ya Hospitali hiyo.

Mara baada ya kupokea msaada huo Waziri Ndalichako ameishukuru Serikali ya Korea kwa msaada huo na kuwataka wanafunzi wanaosoma katika chuo hicho kutumia vema miundombinu ya Chuo kwa  kujifunzia na kufundishia ili kujijenga kitaaluma kwalengo la  kumaliza tatizo la uhaba wa Madaktari na Wataalam wa Afya hapa nchini.
Kiongozi wa Ujumbe wa  Kamati za Bunge la Jamhuri ya Watu wa Korea  Jun Hey Sook akimkabidhi rasmi Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako  msaada wa dawa uliotolewa na nchi hiyo kwa ajili ya Chuo cha Taaluma na Tiba cha MLOGANZILA kilichopo jijini Dar es Salaam.

Akizungumza mara baada ya makabidhiano ya dawa hizo Kiongozi wa Ujumbe wa Korea  wa Kamati ya Afya na Huduma za Jamii ya Bunge la nchi hiyo, Jun Hey Sook amesema msaada huo wa dawa ni ushirikiano katika kuboresha sekta ya Afya.

Serikali imesema haitasita kuvunja mkataba na Kampuni ya Skywards Construction


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mheshimiwa  Wiliam Ole Nasha, amesema Serikali haitasita kuvunja Mkataba na Kampuni ya Skywards Construction inayopaswa kujenga miundombinu ya ufundishaji na ujifunzaji katika Chuo cha Ualimu Ndala kilichopo Halmashauri ya Wilaya ya Nzega, mkoani Tabora.

Naibu Waziri ametoa Kauli hiyo baada ya Kampuni ya Skyward Construction  iliyopaswa kujenga Mabweni, Vyumba vya Madarasa, Ukumbi, Maktaba, Maabara na Matundu ya vyoo kutoonekana katika eneo la ujenzi tangu alipokabidhiwa kutekeleza mradi huo mapema mwezi Januari 27, 2018.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mheshimiwa  William Ole Nasha akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nzega Jacob Mtalitinya juu ya changamato zinazoikabili Shule ya Sekondari Kampala katika kukamilisha ujenzi wa Miundombinu ya ufundishaji na ujifunzaji.

Akizungumza akiwa kwenye ziara ya kukagua utekelezaji wa Miradi inayotekelezwa na Wizara yake kupitia Programu ya Lipa Kulingana na Matoke- EP4R, Naibu Waziri  Ole Nasha amesema Kampuni hiyo tangu ikabidhiwe Mradi haijawahi kufika eneo la mradi kuanza ujenzi na bila taarifa yoyote hivyo kuacha maswali mengi yasiyokuwa na majibu.
‘Kampuni hii ilipaswa kuanza kazi Februari 24, 2018 cha kushangaza hadi sasa haijaonekana eneo la Mradi bila taarifa yoyote. Kampuni hii ya Skyward Constuction inapaswa kujua imeingia mkataba na mikataba hii huwa ina taratibu zake, kama kuna jambo haliendi sawa ni bora akaeleza kwa kuwa Serikali haitasita kuvunja mkataba nae.’ Alisisitiza Naibu Waziri Ole Nasha.

Naibu Waziri Ole Nasha amezitaka Kampuni mbalimbali za ujenzi  kuhakikisha zinazingatia Mikataba, kwani kuchelewa kukabidhi Mradi kwa wakati  kunaisababishia Serikali gharama zisizo za lazima kwa kuwa vifaa vya ujenzi vitapanda bei lakini pia Mradi kushindwa kukidhi kusudio la kuwepo kwa wakati huo.

Nae Mkuu wa Chuo cha Ualimu Ndala Abinego Ndikumwe amesema pamoja na Serikali kukarabati na kujenga miundombinu ya ujifunzaji na ufundishaji bado Chuo hicho kina changamoto za upatikanaji wa Maji, ukosefu wa  usafiri kwa matumizi ya Chuo, Bwalo na ofisi za Wafanyakazi.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. William Ole Nasha akikagua ujenzi wa Miundombinu ya  Shule ya Sekondari Mwanzoli, iliyojengwa na Wizara hiyo kupitia Progamu ya Lipa kulingana na Matokeo, EP4R ambapo mara baada ya ukaguzi huo Naibu Waziri amekiri kuridhishwa na ukarabati huo na kuzitaka shule nyingine kuuga mfano huo.

Akiwa Wilayani Nzega Mhe. Ole Nasha ametemtembelea Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Nzega na Mwanhala, Shule ya Sekondari Kampala na Shule ya Sekondari Mwanhala ambapo akiwa kwenye Shule ya Sekondari Mwanzoli na amekiri kurdhishwa na namna Shule hiyo ilivyotekeleza mradi wa ujenzi wa miundombinu ya shule, ambapo ameahidi Wizara yake itahakikisha inakamilisha ujenzi wa Maabara, na  Nyumba mbili za Walimu.

Jumatatu, 5 Machi 2018

Naibu Waziri Ole Nasha: Sijaridhishwa na ukarabati uliofanyika Butimba


Naibu Waziri wa  Wizara ya  Elimu, Sayansi na Teknolojia Mheshimiwa William Ole Nasha ameitaka Wizara yake kufanya uchunguzi na kutoa ripoti ya namna ukarabati wa Miundombinu ulivyofanyika katika Chuo cha Ualimu Butimba ili kujiridhisha kama kweli ukarabati huo unaakisi kiasi cha fedha zilizotolewa.

Naibu Waziri Ole Nasha ametoa kauli hiyo Mjini Mwanza baada ya kufanya ziara katika chuo hicho hapo  ambapo amesema hajaridhishwa na ukarabati ulivyofanyika kwa kuwa Chuo hicho kilipatiwa kiasi cha takribani  Milioni Mia Nane Sitini na Tatu.    


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. William Ole Nasha akikagua moja ya Bweni la Wanafunzi katika Chuo cha Ualimu Butimba lililofanyiwa ukarabati na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia Programu ya Lipa Kulingana na Matokeo (EP4R).

Ole Nasha  amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha Vyuo vya Ualimu vinakuwa na mazingira mazuri ya kuwaandaa Walimu wanaokwenda kufundisha katika shule mbalimbali  hapa nchini hivyo ni jukumu la  Wakuu wa Taasisi na Vyuo vya Elimu kuhakikisha wanasimaia Miradi mbalimbali ya Elimu kwa ukamilifu  na kuwa Serikali haitasita kuchua hatua kwa yeyote atakayeshindwa kusimamia Miradi hiyo kwa weledi.

“Chuo hiki kimepatiwa takribani Milioni Mia Nane Sitini na Tatu kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu kama hivi ndivyo ukarabati uliofanyika hauonyeshi thamani ya fedha iliyotolewa kwa ajili ya Chuo hiki cha Ualimu Butimba, kwa kweli Sijaridhishwa”alisisitiza Naibu Waziri huyo.

Akitoa maelezo Mkuu wa Chuo hicho John Ole Meiludie amejitetea kuwa kazi hiyo ya ukarabati imefanyika kwa umakini isipokuwa wanafunzi wenyewe  ndiyo wanachana nyavu za madirisha lakini pia hali ya mvua zinaponyesha huondoa  rangi ambayo  inakuwa imepakwa katika majengo ya Chuo hicho.


1.      Naibu Waziri wa Elimu akipokea maelezo katika maabara ya baiolojia Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. William Ole akipokea maelezo kutoka kwa Mkufunzi Ramadhani Wenge kuhusiana na maabara ya Bailojia iliyopo katika Chuo cha Ualimu Butimba Mkoani Mwanza.


Akiwa Mkoani Mwanza Naibu Waziri Ole Nasha ametembelea Shule ya Sekondari Nyegezi iliyoko Wilaya ya Nyamagana na Chuo cha Ufundi Stadi na Huduma VETA kilichopo wilaya ya Ilemela na kuridhishwa na namna walivyotekeleza miradi ya Elimu.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. William Ole Nasha akiongea na Wanafunzi wa Shule ya sekondari Nyegezi Iliyopo Mkoani Mwanza alipofanya ziara shuleni hapo kukagua miradi inayotekelezwa na Programu ya Lipa Kulingana na Matokeo (EP4R).


Jumapili, 4 Machi 2018

Naibu Waziri Ole Nasha aahidi kushughulikia changamoto zilizopo Chuo Kikuu cha Mwalimu Nyerere cha Kilimo na Teknolojia Wilayani Butiama


Naibu Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Mheshimiwa William Ole Nasha ameahidi atashughulikia changamoto zinazokikabili Chuo Kikuu cha Mwalimu Julius K. Nyerere cha Kilimo na Teknolojia (MJNUAT) ili kukiwezesha Chuo hicho kuanza kudahili wanafunzi.

Naibu waziri Ole Nasha ametoa ahadi hiyo alipofanya ziara ya kukagua shughuli za Maedeleo zinazofanyika katika Chuo hicho kilichopo Wilayani Butiama mkoani Mara.

Ole Nasha amesema Chuo hicho kilianzishwa si tu kwa lengo la kumuenzi Baba wa Taifa Mwalimu Julius K. Nyerere lakini pia kuendeleza dhamira yake ya dhati aliyokuwa nayo  kuhusu kilimo.

Akiwa Chuoni hapo Naibu Waziri huyo amebaini kuwepo kwa baadhi ya Watumishi wa Wizara yake wanaosaidia mchakato wa watumishi wa Chuo Kikuu cha Mwalimu Nyerere kuhama kwa madai kuwa katika Chuo hicho hakuna kazi za kufanya  jambo ambalo linazidi kurudisha nyuma juhudi za Serikali za kuhakikisha kuwa Chuo hicho kinaanza kazi mapema iwezekanavyo.

Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Chuo hicho Profesa Dominick Kambarage amesema Chuo hicho  kimeshindwa kuanza kazi kutokana na kukosa Miundombinu inayokidhi vigezo vya Tume ya Vyuo Vikuu.

Awali kabla ya kutembelea Chuo Kikuu hicho  Naibu Waziri huyo alitembelea  Shule ya Msingi Mwisenge, Shule ambayo amesoma hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius K. Nyerere ambapo akiwa shuleni hapo  aliahidi kuwajengea vyumba vitatu vya madarasa.
 Naibu Waziri wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Mheshimiwa William Ole Nasha akifuatilia namna Wanafunzi wa darasa la Tatu katika Shule ya Msingi Mwisenge wanavyopata Elimu kupitia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, TEHAMA 

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mheshimiwa William Ole Nasha akiwa amekaa kwenye dawati ambalo hayati Baba wa Taifa Mwalimu Jullius Kambarage Nyerere aliwahi Kukalia dawati hilo.

Ijumaa, 2 Machi 2018

Naibu Waziri Ole Nasha: Kuna ubadhirifu wa fedha za Serikali.


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe.william Ole Nasha ameitaka  ofisi ya Mkuu wa wilaya, Musoma, Polisi na Takukuru kuhakikisha ndani ya wiki mbili inafanya  uchunguzi wa namna fedha za  ujenzi wa Miundombinu ya  Shule ya Sekondari Kasoma zilivyotumika kwa kuwa kuna harufu ya ubadhirifu wa fedha hizo.

Naibu Waziri Ole Nasha ametoa agizo hilo  mkoani Mara baada ya kufanya ziara ya kukagua ujenzi na ukarabati wa Miundombinu ya Shule inayonengwa na Wizara hiyo kupitia programu ya Lipa kulingana na matokeo, (P4R).

Mheshimiwa Ole Nasha amekiri kuridhishwa na ujenzi uliofanyika katika baadhi ya shule za mkoa ambazo amezitembelea ni  pamoja na Shule ya Msingi Kamuguruki  na Shule Sekondari na  Nyasho.

Waziri Ole Nasha pia amewataka walimu  wote nchini kuhakikisha wanafuata maadili yao ya kazi pamoja na kuacha mara moja  kujihusisha na vitendo vya kimapenzi na wanafunzi.

Amesema kuwa wizara yake imepokea taarifa juu ya baadhi ya walimu kujihusisha kimapenzi na wanafunzi  jambo ambalo ni kinyume cha sheria za nchi pamoja na maadili ya utumishi wa umma.

Naibu Waziri huyo amesisitiza kuwa  serikali haitamvumilia mwalimu yeyote mwenye tabia kama hizo na kuongeza kuwa mwalimu atakayebainika kushiriki vitendo hivyo atashtakiwa kwa mujibu wa sheria za nchi.

Katika hatua nyingine Naibu Waziri  Ole Nasha ameahidi kutoa mabati Mia Tano kwa ajili ya  shule ya sekondari kiara na kujenga madarasa matatu katika shule  Msingi ya Kiara zilizoezuliwa kufuatia mvua kali iliyonyesha jana usiku na kufanya uharibifu wa madarasa mawili ya shule hiyo.

Pia Naibu Waziri Ole Nasha ametembelea chuo cha Maendeleo ya Wananchi Bweri
Kilichopo Wilayani Musoma mkoani Mara.

 Naibu Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Mhe. William Ole Nasha akipata maelezo kutoka kwa wanafunzi wanaosomea  fani ya ufundi umeme kutoka kwenye Chuo cha  Maendeleo ya Wananchi Bweri kilichopo Mkoani Mara.

Naibu Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Mhe.William  Ole Nasha akipata maelezo juu ya hatua za ujenzi wa shule ya Sekondari Kasoma ambapo Naibu Waziro ametoa Wiki mbili kwa Wilaya ya Musoma, Takukuru na Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi mara baada ya kubaini kuwepo kwa ubadhirifu wa fedha za ujenzi katika shule hiyo.

Wakufunzi watakiwa kuzingatia uadilifu na kuweka mbele maslahi ya Taifa.


Naibu Katibu Mkuu Dk.Ave Maria Semakafu amewataka Wakufunzi nchini kuwa waadilifu na kutanguliza maslahi ya Taifa mbele siku zote wanapotekeleza majukumu yao ya kazi.

Dk.Semakafu ametoa rai hiyo mkoani Mwanza wakati akifungua mafunzo ya TEHAMA kwa wakufunzi wa Vyuo vya Ualimu yaliyofanyika katika Chuo cha Ualimu Butimba mkoani humo.

Naibu Katibu Mkuu huyo amesema lengo la mafunzo ni kuwa na maudhui yenye viwango vya ubora unaotakiwa ili kuleta ufanisi katika kujifunza na kufundisha hususan katika  kuandaa Walimu. 

Dk. Semakafu amesisitiza kuwa  mafunzo hayo yatawajengea umahiri na hatimaye kuwa na rasilimali watu yenye maarifa na umahiri kwa ajili ya uzalishaji na hatimaye kukuza uchumi na kufikia malengo ya nchi kwa kuwa na uchumi wa kati na Uchumi wa Viwanda ifikapo 2025. 

" Zipo  changamoto katika Sekta  ya Elimu, sasa lazima tuzitafutie ufumbuzi wa  namna ya kuzikabili kwa kutumia mfumo wa kidigitali ili kuboresha ufundishaji na pia kubadilishana taarifa na maarifa," amesema Dk. Semakafu.

Kwa upande wake mratibu wa Mradi huo  Ignas Chonya amesema Mradi wa Teacher Education Support Project (TESP) utawezesha kufanikisha  umahiri wa mwalimu kupitia mafunzo kazini ya wakufunzi katika maeneo mbali mbali ikiwemo mafunzo ya TEHAMA, mafunzo endelevu katika masomo wanayofundisha, mafunzo ya Uongozi wa Elimu,  ambayo ndiyo nguzo muhimu katika kufanikisha upatikanaji wa Elimu bora hapa nchini.

Wakufunzi walioshiriki Mafunzo hayo ya Siku Tisa ni kutoka katika Chuo cha Ualimu Butimba,Tabora, Shinyanga, Ndala,Murutunguru, Bunda, Katoke, Tarime,Kasulu na Kabanga.

Mradi wa TESP unatekelezwa na Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Canada kupitia Idara yake DFATD kwa ajili ya kugharamia mradi huo kwa kuweka kipaumbele cha kuleta mabadiliko chanya katika Elimu ya Ualimu.
 Naibu Katibu Mkuu Dk. Avemaria Semakafu akisalimiana na viongozi mbalimbali baada ya kuwasili katika Chuo cha Ualimu Butimba kilichopo mkoani Mwanza.

 Baadhi ya Wakufunzi kutoka Vyuo 10 vya Ualimu hapa nchini wakishiriki mafunzo ya TEHAMA, yanayoendeshwa na  TESP.

Naibu Katibu Mkuu Dk. Avemaria Semakafu akionyesha rasimu ya kitabu ambacho ndiyo mwongozo katika kujifunzia TEHAMA kwa Wakufunzi.